RC-KILIMANJARO AWAFARIJI WALIOPATWA NA MAAFA WILAYANI HAI

Posted by Arusha by day and by night On 02:05 No comments


Na Richard Mwangulube,Bomang'ombe

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro,Mhe Leonidas Gama,Mwanzoni mwa wiki hii alitembelea vijiji vitano vya ukanda wa tambarare vilivyokumbwa na maafa ya mvua kubwa na upepo mkali katika wilaya ya Hai kwa lengo la kuwafariji waliokumbwa na maafa hayo.

Mhe Gama aliwafariji wananchi wa vijiji hivyo vya Shirimgungani,Mijongweni,Kwatito,Ngosero na Kikavu Chini.

Mkuu huyo wa mkoa aliwahakikishia wananchi hao kuwa serikali ipo pamoja nao katika kuhakikisha kuwa wanajikimu kimaisha kwa kuwa na mahitaji ya msingi ya chakula ambacho kitawapa nguvu ya kujipanga upya kwa maisha.

Aliuagiza uongozi wa wilaya kuangalia uwezekano wa kuwa na mbegu fupi za mahindi zinazokomaa kwa muda mfupi ili wananchi hao ambao hivi sasa wanajiandaa kwa msimu wa kilimo wawe na uhakika wa kupata mavuno ya kutosha.

Alisema kutokana na mazingira yanayojitokeza ya mvua za sasa kuja kwa kasi lolote linaweza kutokea likiwemo la mvua hizo kukata kwa muda mfupi.

Aidha Mheshimiwa Gama aliutaka uongozi wa wilaya sasa kuwa na programu ya kuhakikisha wananchi wanakuwa na nyumba imara ili kuepukana na maafa ya kila mwaka pale zinapojitokeza mvua kubwa zinazoambanatana na upepo

0 comments:

Post a Comment