KIVUKO CHA MNEPO CHA KIYUNGI KUFANYIWA UKARABATI JUMAMOSI

Posted by Arusha by day and by night On 08:15 No comments

Mkuu wa wilaya ya Hai Novatus Makunga(Katikati) akiwa na Afisa mtendaji mkuu wa kiwanda cha TPC,,Jaffari Ally(Mbele) na diwani wa kata ya Machame Weruweru,Adris Mandrai baada ya kukagua daraja la Mnepo la Kiyungi.

.Mkuu wa wilaya ya Hai Novatus Makunga(aliyekunja mikono kifuani) akijadili jambo kwa pamoja na viongozi wa kata ya Weruweru,kiwanda na TPC na wahandisi wa ujenzi jinsi ya kukarabati daraja la mnepo la Kiyungi.

Baadhi ya wananchi wakivuka mto kwa kutumia kivuko cha mnepo cha Kiyungi.
Diwani wa kata ya Machame Weruweru Adris Mandrai akipita katika kivuko cha mnepo cha Kiyungi

Wananchi wanaotumia kivuko cha Kiyungi
Mwana Mama akivuka mto kwa kutumia kivuko cha mnepo

NA Richard Mwangulube,Hai
 Mkuu wa wilaya ya Hai,Novatus Makunga amekagua kivuko cha mnepo cha Kiyungi na kuagiza kifanyiwe ukarabati wa dharura baada ya kuathiriwa vibaya na mvua zinazoendelea kunyesha na hivyo kuhatarisha maisha ya wananchi wanaokitumia.

Mkuu huyo wa wilaya ameeleza kuwa kutokana na hali hiyo ukarabati huo utafanyika Jumamosi ijayo kwa kushirikiana kati ya viongozi wa kijiji cha Kikavu Chini,Kata ya Machame Weruweru,wahandisi wa wilaya na wale wa kiwanda cha sukari cha TPC.

Makunga ameeleza kuwa kiwanda cha TPC kimekubali kutoa baadhi ya vifaa ambavyo vitasaidia kukarabati daraja hilo hili liweze kuwa salama kwa watumiaji wanaovuka kutoka upande mmoja kwenda mwingine.

Ameeleza kuwa wilaya imeingiza katika bajeti ya mwaka ujao ya kujenga kivuko kipya ambacho kitakuwa cha vyuma kinachokadiriwa kuwa na urefu wa mita thelathini kutoka kingo moja ya mto hadi nyingine kikigharimu zaidi ya shilingi milioni 70

Ameeleza kuwa baada ya mazungumzo na kiwanda cha TPC,walikubali kutoa sehemu ya mchango wa kivuko hicho na kwamba wataalamu wa ujenzi katika wilaya ya Hai watawasilisha michoro na gharama za daraja hilo kwa uongozi wa kiwanda hicho.

Naye Ofisa Mtendaji mkuu wa TPC Jaffari Ally ameahidi kutoa ushirikiano wa ujenzi wa kivuko hicho kutokana na idadi kubwa ya wafanyakazi wa kiwanda hicho kutegemea kivuko hicho kwa ajili ya kufuata mahitaji yao katika eneo la Kikavu Chini.

Aidha ameongeza pia sehemu ya wafanyakazi wanaishi katika ng'ambo ya pili ya mto ho na hivyo kivuko hicho kuwa muhimu kwa kiwanda hicho.

Awali diwani wa kata ya machame Wereweru Adris Mandrai ameeleza kuwa kutokana na mvua kubwa zilizonyesha wakati wa Pasaka ziliathiri daraja hilo na kusababisha baadhi ya wanafunzi hususani wanaosoma madarasa ya chini ya shule za msingi kushindwa kwenda shule kutokana na umri wa mdogo kushindwa kuvuka daraja hilo.

Aidha waumini wa dini ya kikristo walishindwa kwenda kusali katika kanisa lililopo upande wa pili wa Mto Kiyungi lililopo kanisa lao na kulazimika kusali pembeni ya mto na kusikiliza ibada kwa mbali.

0 comments:

Post a Comment