KATIBA INAYOPENDEKEZWA KWA WATANZANIA

Posted by Arusha by day and by night On 04:20 No comments


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

BUNGE MAALUM
KATIBA INAYOPENDEKEZWA
OKTOBA, 2014

KATIBA INAYOPENDEKEZWA
_________
YALIYOMO
_________
UTANGULIZI

SURA YA KWANZA
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

Ibara
SEHEMU YA KWANZA

JINA, MIPAKA, ALAMA, LUGHA NA TUNU ZA TAIFA
1. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
2. Eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
3. Alama na Sikukuu za Taifa
4. Lugha ya Taifa na mawasiliano mbadala
5. Tunu za Taifa
6. Misingi ya utawala bora

SEHEMU YA PILI

MAMLAKA YA WANANCHI, UTII NA HIFADHI YA KATIBA
7. Mamlaka ya Wananchi
8. Watu na Serikali
9. Ukuu na utii wa Katiba
10. Hifadhi ya Utawala wa Katiba

SURA YA PILI
MALENGO MUHIMU, MISINGI YA MWELEKEO WA SHUGHULI ZA SERIKALI NA SERA ZA TAIFA

SEHEMU YA KWANZA

MALENGO MAKUU
11. Malengo Makuu

SEHEMU YA PILI

MALENGO YA KISIASA
12. Lengo la Taifa Kisiasa

SEHEMU YA TATU
MALENGO YA KIUCHUMI, KIJAMII NA KIUTAMADUNI
13. Lengo la Taifa Kiuchumi
14. Lengo la Taifa Kijamii
15. Lengo la Taifa Kiutamaduni

SEHEMU YA NNE
UTAFITI, DIRA YA MAENDELEO, MIPANGO NA UTEKELEZAJI WA MALENGO YA TAIFA
16. Utafiti wa Maendeleo
17. Dira ya Taifa ya Maendeleo
18. Tume ya Mipango ya Jamhuri ya Muungano
19. Utekelezaji wa Malengo ya Taifa
20. Tume ya Sayansi na Teknolojia
21. Matumizi ya masharti ya Sura ya Pili

SEHEMU YA TANO
SERA YA MAMBO YA NJE
22. Sera ya Mambo ya Nje

SURA YA TATU
ARDHI, MALIASILI NA MAZINGIRA
23. Ardhi katika Jamhuri ya Muungano
24. Matumizi bora ya ardhi
25. Fidia
26. Maliasili
27. Mazingira

SURA YA NNE
MAADILI NA MIIKO YA UONGOZI NA UTUMISHI WA UMMA

SEHEMU YA KWANZA
MAADILI YA UONGOZI NA UTUMISHI WA UMMA
28. Dhamana ya uongozi wa umma
29. Kanuni za uongozi wa umma

SEHEMU YA PILI
MIIKO YA UONGOZI WA UMMA
30. Utii wa miiko ya uongozi wa umma
31. Marufuku kwa baadhi ya vitendo

SURA YA TANO
HAKI ZA BINADAMU, WAJIBU WA RAIA, JAMII NA MAMLAKA YA NCHI

SEHEMU YA KWANZA
HAKI ZA BINADAMU
32. Uhuru, utu na usawa wa binadamu
33. Haki ya kuishi
34. Haki ya kutobaguliwa
35. Haki ya kutokuwa mtumwa
36. Uhuru wa mtu binafsi
37. Haki ya faragha na usalama wa mtu
38. Uhuru wa mtu kwenda anakotaka
39. Uhuru wa maoni
40. Uhuru wa habari na vyombo vya habari
41. Uhuru wa imani ya dini
42. Uhuru wa mtu kujumuika na kushirikiana na wengine
43. Uhuru wa kushiriki shughuli za utawala wa nchi
44. Haki ya kufanya kazi
45. Haki za wafanyakazi na waajiri
46. Haki za wakulima, wafugaji, wavuvi na wachimbaji madini
47. Haki ya kumiliki mali
48. Haki ya mtuhumiwa na mfungwa
49. Haki ya mtu aliye chini ya ulinzi au kizuizi
50. Uhuru na haki ya mazingira safi na salama
51. Haki ya afya na maji safi na salama
52. Haki ya elimu
53. Haki za mtoto
54. Haki na wajibu wa vijana
55. Haki za watu wenye ulemavu
56. Haki za makundi madogo katika jamii
57. Haki za wanawake
58. Haki za wazee
59. Uhuru wa taaluma, ubunifu, ugunduzi na usanii

SEHEMU YA PILI
WAJIBU WA RAIA, JAMII NA MAMLAKA YA NCHI NA MIPAKA YA HAKI ZA BINADAMU
(a) Wajibu wa Raia na Jamii kwa Taifa
60. Wajibu wa raia na jamii
61. Wajibu wa kushiriki kazi
62. Ulinzi wa mali ya umma
63. Haki na wajibu muhimu
(b) Wajibu wa Mamlaka ya Nchi
64. Hifadhi ya haki za binadamu
65. Usimamizi wa haki za binadamu
(c) Mipaka ya Haki za Binadamu
66. Mipaka ya haki za binadamu
67. Sheria kuhusu haki, uhuru na wajibu

SURA YA SITA
URAIA KATIKA JAMHURI YA MUUNGANO
68. Uraia wa Jamhuri ya Muungano
69. Haki ya uraia
70. Uraia wa kuzaliwa
71. Uraia wa kuandikishwa
72. Hadhi maalum ya watu wenye asili au nasaba ya Tanzania

SURA YA SABA
MUUNDO WA JAMHURI YA MUUNGANO
73. Muundo wa Muungano
74. Utekelezaji wa shughuli za Mamlaka ya Nchi
75. Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano
76. Mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mambo yasiyo ya muungano
77. Mahusiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
78. Wajibu wa viongozi wakuu kulinda Muungano

SURA YA NANE
SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO

SEHEMU YA KWANZA
SERIKALI, RAIS NA MAKAMU WA RAIS
(a) Serikali
79. Serikali ya Jamhuri ya Muungano

(b) Rais
80. Rais wa Jamhuri ya Muungano
81. Madaraka na majukumu ya Rais
82. Utekelezaji wa madaraka ya Rais
83. Rais kuzingatia ushauri
84. Rais kushindwa kumudu majukumu yake
85. Utaratibu wa kujaza nafasi ya Rais kabla ya kumaliza muda wake
86. Utekelezaji wa majukumu ya Rais akiwa hayupo

(c) Uchaguzi wa Rais
87. Uchaguzi wa Rais
88. Sifa za Rais
89. Utaratibu wa uchaguzi wa Rais
90. Malalamiko kuhusu uhalali wa uchaguzi wa Rais
91. Kiapo cha Rais na muda wa kushika madaraka
92. Haki ya kuchaguliwa tena
(d) Masharti Mahsusi kuhusu Mamlaka ya Rais
93. Madaraka ya kutangaza vita
94. Madaraka ya Rais kutangaza hali ya hatari
95. Mamlaka ya Rais kutoa msamaha
96. Kinga ya mashtaka dhidi ya Rais
97. Bunge kumshtaki Rais
98. Maslahi ya Rais
(e) Makamu wa Rais
99. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano
100. Upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais
101. Majukumu ya Makamu wa Kwanza wa Rais
102. Muda wa Makamu wa Kwanza wa Rais kushika madaraka
103. Bunge kumshtaki Makamu wa Kwanza wa Rais
104. Makamu wa Kwanza wa Rais kushindwa kumudu majukumu yake
105. Upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais wakati nafasi hiyo inapokuwa wazi
106. Kiapo cha Makamu wa Kwanza wa Rais
107. Makamu wa Pili wa Rais
108. Makamu wa Tatu wa Rais
109. Maslahi ya Makamu wa Rais

SEHEMU YA PILI
(a) Waziri Mkuu
110. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano
111. Kazi na Mamlaka ya Waziri Mkuu

WAZIRI MKUU NA BARAZA LA MAWAZIRI LA SERIKALI YA
JAMHURI YA MUUNGANO
112. Uwajibikaji wa Serikali
113. Kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu

(b) Baraza la Mawaziri
114. Baraza la Mawaziri
115. Uteuzi wa Mawaziri na Naibu Mawaziri
116. Sifa za Waziri na Naibu Waziri
117. Kiapo, muda na masharti ya kazi ya Waziri na Naibu Waziri

(c) Mwanasheria Mkuu wa Serikali
118. Mwanasheria Mkuu wa Serikali
119. Naibu Mwanasheria Mkuu

(d) Mkurugenzi wa Mashtaka
120. Mkurugenzi wa Mashtaka
(e) Katibu Mkuu Kiongozi
121. Katibu Mkuu Kiongozi

(f) Utekelezaji wa Shughuli za Baraza la Mawaziri
122. Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri

(g) Wakuu wa Mikoa
123. Wakuu wa Mikoa

SEHEMU YA TATU
MADARAKA YA UMMA
124. Serikali za Mitaa
125. Mamlaka ya Serikali za Mitaa
126. Uongozi katika Serikali za Mitaa

SURA YA TISA
UHUSIANO NA URATIBU WA MAMBO YA MUUNGANO
127. Tume ya Usimamizi na Uratibu wa Mambo ya Muungano
128. Majukumu ya Tume ya Mambo ya Muungano

SURA YA KUMI
BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO

SEHEMU YA KWANZA
MUUNDO NA MADARAKA YA BUNGE
129. Bunge
130. Muda wa Bunge
131. Madaraka ya Bunge
132. Mipaka ya Bunge katika kutumia madaraka yake
133. Madaraka ya kutunga Sheria
134. Utaratibu wa kubadilisha Katiba
135. Utaratibu wa kutunga sheria
136. Utaratibu wa kutunga sheria kuhusu mambo ya fedha
137. Madaraka ya Rais kuhusu muswada wa sheria
138. Kupitishwa kwa Bajeti ya Serikali

SEHEMU YA PILI

WABUNGE
139. Uchaguzi wa Wabunge
140. Sifa za kuchaguliwa kuwa Mbunge
141. Utaratibu wa uchaguzi wa Wabunge
142. Kiapo na masharti ya kazi ya Ubunge
143. Kupoteza sifa za Ubunge
144. Uamuzi wa suala kama mtu ni Mbunge
145. Tamko rasmi la Mbunge kuhusu mali na madeni

SEHEMU YA TATU

UONGOZI WA BUNGE
146. Spika na mamlaka yake
147. Ukomo wa Spika
148. Naibu Spika
149. Sifa za mtu kuchaguliwa kuwa Spika au Naibu Spika
150. Utaratibu wa uchaguzi na kiapo cha Spika na Naibu Spika
151. Katibu wa Bunge
152. Sekretarieti ya Bunge

SEHEMU YA NNE

UTARATIBU WA SHUGHULI ZA BUNGE
153. Kanuni za kudumu za Bunge
154. Rais kulihutubia Bunge
155. Mikutano ya Bunge
156. Uongozi wa kikao cha Bunge
157. Akidi ya kikao cha Bunge
158. Kamati za Bunge

SEHEMU YA TANO
 MADARAKA NA HAKI ZA BUNGE
159. Uhuru wa majadiliano Bungeni

SEHEMU YA SITA
TUME YA UTUMISHI WA BUNGE NA MFUKO WA BUNGE
(a) Tume ya Utumishi wa Bunge

160. Tume ya Utumishi wa Bunge
161. Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Bunge

(b) Mfuko wa Bunge
162. Mfuko wa Bunge

SURA YA KUMI NA MOJA

SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR, BARAZA LA MAPINDUZI LA ZANZIBAR NA BARAZA LA WAWAKILISHI LA ZANZIBAR

SEHEMU YA KWANZA
(a) Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
163. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na mamlaka yake

(b)Rais wa Zanzibar
164. Rais wa Zanzibar na mamlaka yake

(c) Baraza la Mapinduzi la Zanzibar

165. Baraza la Mapinduzi la Zanzibar na kazi zake

SEHEMU YA PILI
BARAZA LA WAWAKILISHI LA ZANZIBAR
166. Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

SURA YA KUMI NA MBILI
MAHAKAMA YA JAMHURI YA MUUNGANO

SEHEMU YA KWANZA
MISINGI YA UTOAJI HAKI NA UHURU WA MAHAKAMA
167. Kuanzishwa kwa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano
168. Misingi ya utoaji haki
169. Uhuru wa Mahakama

SEHEMU YA PILI
MUUNDO WA MAHAKAMA
(a) Mahakama ya Jamhuri ya Muungano
170. Muundo wa Mahakama

(b) Mahakama ya Juu ya Jamhuri ya Muungano
171. Mahakama ya Juu
172. Akidi ya kikao cha Mahakama ya Juu
173. Mamlaka ya Mahakama ya Juu
174. Madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu

(c) Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Juu
175. Uteuzi wa Jaji Mkuu
176. Uteuzi wa Naibu Jaji Mkuu
177. Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Juu
178. Kiapo cha Jaji wa Mahakama ya Juu
179. Muda wa Jaji wa Mahakama ya Juu kuwa madarakani
180. Utaratibu wa kukaimu nafasi ya Jaji wa Mahakama ya Juu
181. Utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Juu

(d) Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano
182. Mahakama ya Rufani
183. Akidi ya kikao cha Mahakama ya Rufani
184. Mamlaka ya Mahakama ya Rufani
185. Madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Rufani

(e) Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Rufani
186. Uteuzi wa Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani
187. Uteuzi wa Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani
188. Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Rufani
189. Kiapo cha Jaji wa Mahakama ya Rufani
190. Muda wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Jaji wa Mahakama ya Rufani kuwa madarakani
191. Utaratibu wa kukaimu nafasi ya Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani
192. Utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Rufani

(f) Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano
193. Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano na Mamlaka yake
194. Uteuzi wa Jaji wa Mahakama Kuu
195. Muda wa Jaji wa Mahakama Kuu kushika madaraka
196. Utaratibu wa kushughulikia nidhamu kwa Jaji wa Mahakama Kuu
197. Kiapo cha Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano

(g) Mahakama Kuu ya Zanzibar
198. Mahakama Kuu ya Zanzibar
199. Mamlaka ya Mahakama Kuu ya Zanzibar
(h) Usimamizi wa Shughuli za Mahakama
200. Msajili Mkuu wa Mahakama
201. Majukumu ya Msajili Mkuu wa Mahakama
202. Mtendaji Mkuu wa Mahakama
203. Majukumu ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama

SEHEMU YA TATU
TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA NA MFUKO WA MAHAKAMA
(a) Tume ya Utumishi wa Mahakama
204. Tume ya Utumishi wa Mahakama
205. Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama
206. Uanachama katika vyama vya siasa

(b) Mfuko wa Mahakama
207. Mfuko wa Mahakama

SURA YA KUMI NA TATU
UTUMISHI WA UMMA KATIKA JAMHURI YA MUUNGANO
208. Misingi mikuu ya utumishi wa umma
209. Ajira na uteuzi wa kiongozi na mtumishi wa umma katika taasisi za Muungano
210. Tume ya Utumishi wa Umma
211. Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma
212. Mamlaka na Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Umma
213. Tume ya Mishahara
214. Tume za kisekta

SURA YA KUMI NA NNE
UCHAGUZI KATIKA VYOMBO VYA UWAKILISHI NA VYAMA VYA SIASA

SEHEMU YA KWANZA
UWAKILISHI WA WANANCHI
215. Ushiriki katika uchaguzi na kura ya maoni
216. Mgombea huru

SEHEMU YA PILI
TUME HURU YA UCHAGUZI
(a) Tume Huru ya Uchaguzi
217. Kuundwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi
218. Kamati ya Uteuzi
219. Muda wa Mjumbe wa Tume kushika madaraka
220. Wajibu wa Tume Huru ya Uchaguzi
221. Malalamiko kuhusu uchaguzi

(b) Mkurugenzi wa Uchaguzi
222. Uteuzi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi
223. Majukumu ya Mkurugenzi wa Uchaguzi

SEHEMU YA TATU
USAJILI NA USIMAMIZI WA VYAMA VYA SIASA
(a) Vyama vya Siasa
224. Usajili wa vyama vya siasa

(b) Msajili wa Vyama vya Siasa
225. Uteuzi wa Msajili wa Vyama vya Siasa
226. Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa
227. Wajibu wa Msajili na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa

SURA YA KUMI NA TANO
TAASISI ZA UWAJIBIKAJI

SEHEMU YA KWANZA
TUME YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA
228. Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma
229. Uteuzi na sifa za Mjumbe
230. Kamati ya Uteuzi
231. Majukumu ya Tume
232. Muda wa Mjumbe wa Tume kushika madaraka
233. Uhuru wa Tume
234. Uwezeshaji wa nyenzo na rasilimali

SEHEMU YA PILI
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
235. Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
236. Sifa za Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Kamishna wa Tume
237. Kamati ya Uteuzi
238. Kazi na majukumu ya Tume
239. Muda wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Kamishna wa Tume kushika madaraka
240. Kuondolewa madarakani kwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Kamishna wa Tume
241. Uhuru wa Tume
242. Uwezeshaji wa nyenzo na rasilimali

SEHEMU YA TATU
MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
243. Uteuzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
244. Sifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
245. Kazi na majukumu ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
246. Muda wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kushika madaraka
247. Kuondolewa madarakani kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
248. Uwezeshaji wa nyenzo na rasilimali

SEHEMU YA NNE
CHOMBO CHA KUZUIA NA KUPAMBANA NA RUSHWA
249. Udhibiti wa rushwa

SURA YA KUMI NA SITA
MASHARTI KUHUSU FEDHA ZA JAMHURI YA MUUNGANO
(a) Mfuko Mkuu wa Hazina na Fedha za Jamhuri ya Muungano
250. Misingi ya matumizi ya fedha za umma
251. Akaunti ya Fedha ya Pamoja
252. Tume ya Pamoja ya Fedha
253. Mfuko Mkuu wa Hazina
254. Masharti ya kutoa fedha za matumizi katika Mfuko Mkuu wa Hazina
255. Utaratibu wa kuidhinisha matumizi ya fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina
256. Utaratibu wa kuidhinisha matumizi ya fedha kabla ya sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali kuanza kutumika
257. Mfuko wa Matumizi ya Dharura
258. Mishahara ya baadhi ya watumishi kudhaminiwa na Mfuko Mkuu wa Hazina

(b) Deni la Taifa na Mikopo ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano
259. Deni la Taifa
260. Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kukopa
261. Mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kukopa
262. Mamlaka ya kutoza kodi
263. Ununuzi wa umma
264. Benki Kuu ya Jamhuri ya Muungano

SURA YA KUMI NA SABA
ULINZI NA USALAMA WA JAMHURI YA MUUNGANO
(a) Ulinzi na Usalama wa Taifa
265. Usalama wa Taifa
266. Vyombo vya Ulinzi na Usalama wa Taifa
267. Baraza la Usalama la Taifa
268. Majukumu ya Baraza la Usalama la Taifa

(b) Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
269. Kuanzishwa kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
270. Uteuzi wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi
271. Madaraka ya Amiri Jeshi Mkuu

(c) Jeshi la Polisi
272. Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Muungano
273. Uteuzi wa Mkuu wa Jeshi la Polisi
274. Uanzishwaji wa huduma nyingine za ulinzi
(d) Idara ya Usalama wa Taifa ya Jamhuri ya Muungano
275. Kuanzishwa kwa Idara ya Usalama wa Taifa
276. Uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa

SURA YA KUMI NA NANE
MENGINEYO
277. Utaratibu wa kujiuzulu katika utumishi wa umma
278. Masharti kuhusu kukabidhi madaraka
279. Ufafanuzi
280. Jina la Katiba, kuanza kutumika na matumizi
281. Kufutwa kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977

SURA YA KUMI NA TISA
MASHARTI YATOKANAYO NA MASHARTI YA MPITO

SEHEMU YA KWANZA
MASHARTI YATOKANAYO
282. Matumizi ya baadhi ya masharti ya Katiba

SEHEMU YA PILI
MASHARTI KIKATIBA NA SHERIA ZA NCHI
283. Kuendelea kutumika masharti ya Katiba
284. Kuendelea kutumika kwa sheria za nchi

SEHEMU YA TATU
UTUMISHI WA UMMA
Serikali ya Jamhuri ya Muungano
285. Kuendelea kuwepo kwa Rais madarakani
286. Kuendelea kuwepo kwa Makamu wa Rais madarakani
287. Kuendelea kuwepo kwa Waziri Mkuu, Mawaziri na Naibu Mawaziri
288. Kuendelea kwa utumishi wa umma

SEHEMU YA NNE
BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO
289. Kuendelea kwa Ubunge na Uongozi wa Bunge
290. Kuvunjwa kwa Bunge

SEHEMU YA TANO
MAHAKAMA YA JAMHURI YA MUUNGANO
291. Kuendelea kwa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu
292. Kuendelea kwa mashauri yaliyopo mahakamani

SEHEMU YA SITA
MASHARTI YA MPITO
293. Muda wa Mpito
294. Utekelezaji wa masharti ya Katiba Mpya
295. Kamati ya Utekelezaji wa Katiba
296. Kufutwa kwa Masharti Yatokanayo na Masharti ya Mpito
________
NYONGEZA
________

UTANGULIZI
KWA KUWA, sisi wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga katika nchi yetu jamii inayoheshimu na kuzingatia misingi ya utu na udugu, uhuru, kujitegemea, haki, usawa, amani na utulivu, umoja na mshikamano katika nyanja zote za maisha yetu;

NA KWA KUWA, tunaamini kuwa misingi hiyo inaweza tu kutekelezwa katika jamii yenye mfumo wa demokrasia na misingi ya utawala bora ambayo Serikali yake inasimamiwa na Bunge lenye Wabunge waliochaguliwa na wanaowakilisha wananchi, na Mahakama huru inayozingatia misingi ya utoaji haki na kuhakikisha kuwa haki za binadamu zinalindwa na kudumishwa na kwamba uhuru na wajibu wa kila mtu unatekelezwa kwa uaminifu;

NA KWA KUWA, tunatambua umuhimu wa kutunza mali za Mamlaka ya Nchi na ya pamoja, kupiga vita aina zote za uharibifu na ubadhirifu, na kuhimiza matumizi bora na endelevu ya rasilimali na maliasili zetu pamoja na kulinda na kuhifadhi mazingira yetu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo;

NA KWA KUWA, tunatambua umuhimu na faida za kujenga, kukuza na kuendeleza amani, umoja, ujirani mwema na ushirikiano na mataifa mbalimbali ya Afrika na dunia kwa ujumla;

NA KWA KUWA, azma ya kujenga Umoja wa Bara la Afrika inadhihirishwa na Muungano wa iliyokuwa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar;

NA KWA KUZINGATIA, urithi tulioachiwa na Waasisi wa Taifa letu wa kujenga nchi yenye umoja wa watu wake ambao hawabaguani kwa misingi ya ukabila, dini, rangi, jinsi, ulemavu au ubaguzi wa aina nyingine yoyote;

NA KWA KUWA, ni muhimu kulinda, kuimarisha na kuudumisha Muungano, kujenga Taifa huru na linalojitegemea, kuimarisha na kuendeleza misingi ya utawala bora na maadili ya viongozi, kujenga umoja na mshikamano utakaowezesha kutimiza malengo ya Taifa, kujenga na kuendeleza ukuu wa mamlaka ya wananchi, utii wa mamlaka ya Katiba na kuimarisha na kudumisha uzalendo kwa Taifa miongoni mwa Watanzania;

NA KWA KUZINGATIA, uzoefu wa zaidi ya Miaka Hamsini ya Muungano, na umuhimu wa ushiriki wa wananchi katika utungaji wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

HIVYO BASI, KATIBA HII YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, ILIYOPENDEKEZWA NA BUNGE MAALUM LA KATIBA, imetungwa na SISI WANANCHI WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA kupitia KURA YA MAONI kwa madhumuni ya kujenga jamii kama hiyo, na kuhakikisha kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaongozwa na Serikali yenye kufuata misingi ya demokrasia, utawala wa sheria, kujitegemea na isiyofungamana na dini.

SURA YA KWANZA
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

SEHEMU YA KWANZA
JINA, MIPAKA, ALAMA, LUGHA NA TUNU ZA TAIFA
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
1.-(1) Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi yenye mamlaka kamili ambayo imetokana na Muungano wa nchi mbili za Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ambazo kabla ya Hati ya Makubaliano ya Muungano ya tarehe 22 Aprili, 1964 zilikuwa nchi huru.
(2) Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi ya kidemokrasia inayofuata mfumo wa vyama vingi vya siasa, utawala wa sheria, inayoheshimu misingi ya haki za binadamu, isiyofungamana na dini yoyote na inayojitegemea.
(3) Hati ya Makubaliano iliyorejewa katika ibara ndogo ya (1) ndiyo msingi mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Katiba hii, kwa kadri itakavyorekebishwa, itakuwa ni mwendelezo wa Makubaliano hayo.

Eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
2.-(1) Eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni:
(a) eneo lote la Tanzania Bara, ikiwa ni pamoja na eneo lake la bahari ambalo kabla ya Muungano lilikuwa likiitwa Jamhuri ya Tanganyika pamoja na maeneo mengine yatakayoongezeka; na
(b) eneo lote la Zanzibar, ikiwa ni pamoja na eneo lake la bahari ambalo kabla ya Muungano lilikuwa likiitwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar pamoja na maeneo mengine yatakayoongezeka.
(2) Rais wa Jamhuri ya Muungano atakuwa na mamlaka ya kuigawa Jamhuri ya Muungano katika mikoa, wilaya na maeneo mengine:
Isipokuwa kwa upande wa Tanzania Zanzibar, Rais atashauriana na Rais wa Zanzibar kabla ya kuigawa Tanzania Zanzibar katika mikoa, wilaya au maeneo mengine.
(3) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), Bunge litatunga sheria itakayoainisha na kufafanua mipaka ya eneo la Jamhuri ya Muungano.

Alama na Sikukuu za Taifa
3.-(1) Alama za Taifa zitakuwa ni:
(a) Bendera ya Taifa;
(b) Wimbo wa Taifa; na
(c) Nembo ya Taifa,
kama zitakavyoainishwa katika sheria za nchi.
(2) Sikukuu za kitaifa zitakuwa:
(a) Siku ya Uhuru wa Tanganyika, itakayoadhimishwa tarehe
9 Disemba;
(b) Siku ya Mapinduzi ya Zanzibar, itakayoadhimishwa tarehe
12 Januari;
(c) Siku ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, itakayoadhimishwa tarehe 26 Aprili; na
(d) sikukuu nyingine zitakazoainishwa na sheria za nchi.
(3) Kila sikukuu ya kitaifa itakuwa ni siku ya mapumziko.

Lugha ya Taifa na mawasiliano mbadala
4.-(1) Lugha ya Taifa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Kiswahili na itatumika katika mawasiliano rasmi ya kitaifa na kiserikali.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), lugha ya Kiingereza au lugha nyingine yoyote ya kimataifa inaweza kutumika kama lugha rasmi ya mawasiliano ya kiserikali, pale itakapohitajika.
(3) Kwa mujibu wa Ibara hii, lugha ya alama kwa viziwi na lugha ya alama mguso kwa viziwi wasioona, zitakuwa lugha rasmi za mawasiliano.
(4) Serikali itaweka mazingira yatakayowezesha kuwepo kwa mawasiliano mbadala zikiwemo lugha ya alama, lugha ya alama mguso, maandishi yaliyokuzwa na nukta nundu kwenye sehemu muhimu za umma na katika vyombo vya habari vinavyotangaza habari zake kitaifa kwa ajili ya watu wenye ulemavu.

Tunu za Taifa
5. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaenzi na kuzingatia Tunu za Taifa zifuatazo:
(a) lugha ya Kiswahili;
(b) Muungano;
(c) utu na udugu; na
(d) amani na utulivu.

Misingi ya utawala bora
6.-(1) Katika utekelezaji wa mamlaka au shughuli zozote kwa mujibu wa Katiba hii au sheria za nchi, misingi ya utawala bora katika Ibara hii ni lazima izingatiwe na kufuatwa na taasisi ya Serikali, ofisa wa Serikali au mtu yeyote aliyepewa dhamana ya:
(a) kutumia au kutafsiri Katiba hii;
(b) kutunga, kutumia au kutafsiri sheria yoyote; na
(c) kufanya au kutekeleza maamuzi ya sera za kitaifa.
(2) Misingi ya utawala bora katika Jamhuri ya Muungano itajumuisha:
(a) uadilifu;
(b) demokrasia;
(c) uwajibikaji;
(d) utawala wa sheria;
(e) ushirikishwaji wa wananchi;
(f) haki za binadamu;
(g) usawa wa jinsia;
(h) umoja wa kitaifa;
(i) uwazi; na
(j) uzalendo.

SEHEMU YA PILI
MAMLAKA YA WANANCHI, UTII NA HIFADHI YA KATIBA

Mamlaka ya
7.-(1) Wananchi ndiyo msingi wa mamlaka yote, na kwa hiyo:

Wananchi
(a) Serikali itapata madaraka na mamlaka yake kutoka kwa wananchi ambao kwa umoja na ujumla wao wanaimiliki na kuipatia Katiba hii uhalali;
(b) lengo kuu la Serikali litakuwa ni maendeleo na ustawi wa wananchi;
(c) Serikali itawajibika kwa wananchi; na
(d) wananchi watashiriki katika shughuli za Serikali kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(2) Kwa mujibu wa Ibara hii, Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zitapata madaraka na mamlaka yake kutoka kwa wananchi kupitia uchaguzi wa kidemokrasia utakaoendeshwa na kusimamiwa na vyombo vitakavyopewa mamlaka na Katiba hii na Katiba ya Zanzibar, kwa kadri itakavyokuwa.

Watu na Serikali
8.-(1) Serikali na vyombo vyake, katika uendeshaji na utekelezaji wa shughuli zake, itazingatia azma ya kukuza umoja wa kitaifa na kudumisha heshima ya Taifa.
(2) Kwa madhumuni ya masharti ya ibara ndogo ya (1), Serikali na vyombo vyake vinawajibika kuelekeza sera, sheria na shughuli zake zote kwa lengo la kuhakikisha kwamba:
(a) utu, heshima na haki za binadamu zinalindwa, zinathaminiwa, zinahifadhiwa na kudumishwa kwa kuzingatia mila na desturi za Watanzania na mikataba ya kimataifa iliyoridhiwa na Jamhuri ya Muungano;
(b) sheria za nchi zinasimamiwa na kutekelezwa;
(c) utajiri wa Taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na kutumika kwa manufaa ya wananchi wote na kuzuia unyonyaji wa aina yoyote;
(d) ardhi ikiwa ni rasilimali kuu na msingi wa Taifa, inalindwa, inatunzwa na kutumiwa kwa manufaa, maslahi na ustawi wa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo;
(e) maendeleo ya uchumi wa Taifa yanapangwa na kukuzwa kwa ulinganifu na kwa namna ambayo inawanufaisha wananchi wote;
(f) kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi anafanya kazi, na “kazi” maana yake ni shughuli yoyote halali inayompatia mtu kipato chake;
(g) kunakuwepo fursa na haki zilizo sawa kwa wananchi wote, wanawake na wanaume, bila ya kujali rangi, kabila, nasaba, ulemavu, itikadi, dini au hali ya mtu;
(h) aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, ukatili, udhalilishaji, unyanyasaji, rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini;
(i) utajiri wa rasilimali na maliasili za Taifa unaelekezwa katika kuleta maendeleo, kuondoa umaskini, ujinga na maradhi; na
(j) nchi inaongozwa kwa kufuata misingi ya demokrasia, utawala wa sheria na kujitegemea.
Ukuu na utii wa Katiba
9.-(1) Katiba hii ni sheria kuu katika Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa na Katiba hii.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), endapo masharti ya sheria
yoyote itakayotungwa na vyombo vyenye mamlaka ya kutunga sheria yatatofautiana na masharti ya Katiba hii, masharti ya sheria hiyo yatakuwa batili na yatatenguka kwa kiwango kile kinachotofautiana na masharti ya Katiba hii.
(3) Mtu yeyote, chombo au taasisi ya Serikali, jumuiya, wakala yeyote na mamlaka binafsi zitakuwa na wajibu wa kuzingatia na kutii masharti ya Katiba hii na sheria za nchi.
(4) Sheria yoyote, mila, desturi au uamuzi wowote wa chombo cha dola au ofisa wa Serikali ni sharti ufuate na kuzingatia masharti yaliyomo kwenye Katiba hii na kwamba sheria, mila, desturi au uamuzi wowote ambao hautawiana au kwenda sambamba na masharti ya Katiba hii utakuwa batili.
(5) Serikali itaweka utaratibu wa kuwawezesha wananchi kuifahamu, kuilinda na kuitii Katiba hii.

Hifadhi ya Utawala wa Katiba
10.-(1) Mtu au kikundi cha watu hakitachukua au kushikilia mamlaka ya nchi isipokuwa kwa mujibu wa Katiba hii.
(2) Kitendo chochote kinachokiuka masharti ya ibara ndogo ya (1) ni batili na ni kitendo cha uhaini kama itakavyoelezwa katika sheria za nchi.

SURA YA PILI
MALENGO MUHIMU, MISINGI YA MWELEKEO WA SHUGHULI ZA SERIKALI NA SERA ZA TAIFA

SEHEMU YA KWANZA
MALENGO MAKUU
Malengo Makuu
11.-(1) Lengo la Katiba hii ni kulinda, kuimarisha na kudumisha haki, usawa, udugu, amani, umoja na utangamano wa wananchi wa Jamhuri ya Muungano kwa kuzingatia ustawi wa wananchi na kujenga Taifa huru lenye demokrasia, utawala bora, maendeleo endelevu na kujitegemea.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), lengo hilo kuu litaendelezwa na kuimarishwa katika nyanja zote kuu, ikijumuisha nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.
(3) Bunge litatunga sheria itakayofafanua juu ya utekelezaji wa malengo muhimu kwa mujibu wa Katiba hii.

SEHEMU YA PILI
MALENGO YA KISIASA
Lengo la Taifa Kisiasa
12.-(1) Lengo la Katiba hii kisiasa ni kudumisha demokrasia na kuondoa ubaguzi wa aina zote.
(2) Katika kuhakikisha utekelezaji wa lengo hilo, Serikali itachukua hatua zinazofaa ili:
(a) kuhakikisha kuwa inazuia na kuondoa dhuluma, vitisho, ubaguzi, unyanyasaji, rushwa, uonevu na upendeleo miongoni mwa wananchi kwa misingi ya itikadi, asili ya mtu, sehemu anayotoka,
nasaba, kabila, jinsi, dini au imani yake;
(b) kuhakikisha kuwepo kwa amani na utulivu na kujenga utamaduni wa kuenzi, kuheshimu na kudumisha uzalendo, amani, umoja, utangamano, ushirikiano na uvumilivu wa kisiasa kwa madhumuni ya kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi; na
(c) kuhakikisha kuwepo kwa usalama na ustawi wa watu na mali zao.

SEHEMU YA TATU
MALENGO YA KIUCHUMI, KIJAMII NA KIUTAMADUNI
Lengo la Taifa Kiuchumi
13.-(1) Lengo la Katiba hii kiuchumi ni kujenga uchumi wa kisasa utakaowezesha wananchi na Taifa kujitegemea kwa kuzingatia matumizi ya elimu ya sayansi na teknolojia katika nyanja zote za uzalishaji mali kwa kuhimiza mapinduzi ya kilimo, ufugaji na uvuvi, mapinduzi ya viwanda na kujenga sekta muhimu ya nishati, mawasiliano na miundo mbinu.
(2) Katika kuhakikisha utekelezaji wa lengo hilo, Serikali itachukua hatua zifuatazo:
(a) kuweka na kutekeleza mpango mkakati wa kutoa elimu ya kisasa yenye kusisitiza ubunifu, sayansi na teknolojia kuanzia ngazi ya msingi, sekondari, ufundi na amali hadi vyuo vikuu na katika shughuli za uchumi na maendeleo ya Taifa kwa ujumla;
(b) kuimarisha na kujenga uwezo wa vyama vya ushirika ili viwe vyombo madhubuti vya kueneza maarifa, mbinu na zana bora za kisasa katika kilimo, ufugaji na uvuvi ili kuongeza tija katika uzalishaji, kutoa mikopo, kutafuta na kuendeleza masoko ya mazao yao;
(c) kuweka utaratibu wa kujenga viwanda mama, viwanda vya kati na viwanda vidogo vitakavyosindika na kuchakata bidhaa za kilimo, ufugaji, uvuvi na madini ili kuziongezea thamani kwa ajili ya mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi;
(d) kuhakikisha kuwa wakulima, wafugaji na wavuvi wanakuwa na ardhi na nyenzo kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao katika kukuza mazingira yaliyo bora kwa ajili ya kuhamasisha sekta binafsi katika uchumi, upangaji na usimamizi wa mizania ya bei za mazao na pembejeo;
(e) kuweka mazingira bora ya kufanya biashara na kukuza fursa za uwekezaji;
(f) kuhamasisha uwekezaji wa pamoja baina ya raia na wasio raia katika miundombinu ya uchumi, uvunaji wa rasilimali na maliasili za Taifa;
(g) kuhakikisha kwamba shughuli za Serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo utajiri wa Taifa unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote na kuweka mazingira yatakayochochea maendeleo linganifu na kuwawezesha wananchi kuondokana na umaskini; na
(h) kuweka utaratibu wa usimamizi na udhibiti wa huduma za
kiuchumi na kijamii ili kuwezesha ushindani wenye haki na ubora wa viwango vya huduma zinazotolewa ili kuwalinda wananchi.

Lengo la Taifa Kijamii
14.-(1) Lengo la Katiba hii kijamii ni kujenga jamii yenye ustawi na uwezo wa kushiriki katika shughuli za kimaendeleo katika nyanja mbalimbali.
(2) Katika utekelezaji wa lengo hilo, Serikali itachukua hatua zinazofaa ili:
(a) kuhakikisha kwamba heshima ya binadamu inahifadhiwa na kudumishwa kwa kufuata mila, desturi na Kanuni za Tangazo la Dunia kuhusu Haki za Binadamu na mikataba mingine ya kimataifa iliyoridhiwa na Jamhuri ya Muungano;
(b) kuhakikisha kwamba Serikali na vyombo vyake vyote vya umma vinatoa nafasi na fursa sawa kwa raia wote, bila ubaguzi;
(c) kuhakikisha kuwa huduma na hifadhi ya jamii inatolewa kwa watu wasiojiweza, wazee, watoto na watu wenye ulemavu;
(d) kuwezesha upatikanaji na utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria kwa wananchi wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za mawakili;
(e) kuweka utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa haki ya mtu kujipatia elimu na kuwa huru kupata fursa sawa ya kutafuta elimu katika fani anayoipenda hadi kufikia upeo wowote kulingana na uwezo wake;
(f) kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora ya afya kwa watu wote ikiwa ni pamoja na afya ya uzazi salama;
(g) kuweka mazingira yatakayowezesha wasanii kutumia fursa zilizopo na vipaji vyao katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na mabadiliko katika jamii; na
(h) kuweka utaratibu na mazingira yanayofaa kwa ajili ya kukuza na kuendeleza michezo nchini.
Lengo la Taifa Kiutamaduni
15.-(1) Lengo la Katiba hii kiutamaduni ni kukuza, kudumisha na kuhifadhi lugha ya Kiswahili, urithi wa asili na utamaduni wa wananchi.
(2) Katika kuhakikisha utekelezaji wa lengo hilo, Serikali itachukua hatua zinazofaa ili:
(a) kulinda na kuendeleza lugha ya Kiswahili;
(b) kulinda na kuhifadhi urithi wa asili, malikale na sehemu zenye umuhimu wa kihistoria ili kuepuka uharibifu, wizi au utoroshaji nje ya nchi;
(c) kulinda, kuhifadhi na kuendeleza utamaduni wa jamii mbalimbali; na
(d) kujenga utamaduni wa kuwepo ushirikiano, maelewano, maridhiano, uvumilivu na kuheshimu mila, desturi na imani ya dini ya kila mtu.

SEHEMU YA NNE
UTAFITI, DIRA YA MAENDELEO, MIPANGO NA UTEKELEZAJI WA MALENGO YA TAIFA
Utafiti wa Maendeleo
16. Katika kuweka mipango ya Taifa, Serikali itatoa kipaumbele kwenye shughuli za utafiti wa maendeleo kwa lengo la kupata taarifa zitakazowezesha upatikanaji wa maendeleo ya kiuchumi nchini.

Dira ya Taifa ya Maendeleo
17.-(1) Kutakuwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo katika nyanja mbalimbali kwa kuzingatia haki na wajibu wa kila raia kupata maendeleo.
(2) Katika kutekeleza masharti ya ibara ndogo ya (1), Mamlaka za Serikali zitaweka mipango ya kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo.
Tume ya Mipango ya Jamhuri ya Muungano
18.-(1) Kutakuwa na Tume ya Mipango ya Jamhuri ya Muungano itakayoitwa “Tume ya Mipango” ambayo itakuwa ndicho chombo cha juu cha kupanga na kusimamia utekelezaji wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.
(2) Bunge litatunga sheria kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya Ibara hii.
Utekelezaji wa Malengo ya Taifa
19.-(1) Malengo ya Taifa yaliyoainishwa katika Katiba hii yatakuwa ni mwongozo kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na kwa wananchi katika matumizi au kutafsiri masharti ya Katiba hii au sheria nyingine yoyote au katika utekelezaji wa maamuzi ya kisera kwa madhumuni ya kujenga jamii iliyo bora, huru na makini.
(2) Serikali ya Jamhuri ya Muungano itawasilisha Bungeni mara moja kwa mwaka, taarifa ya hatua ilizozichukua katika utekelezaji wa malengo ya Taifa.

Tume ya Sayansi na Teknolojia
20.-(1) Kutakuwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia ambayo itakuwa ni chombo cha usimamizi, uratibu, utafiti na ushauri kuhusu masuala yote yanayohusu sayansi na teknolojia nchini.
(2) Muundo, majukumu na mamlaka ya Tume ya Sayansi na Teknolojia yatakuwa kama yatakavyoainishwa na sheria itakayotungwa na Bunge.

Matumizi ya masharti ya Sura ya Pili
21.-(1) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (2), Serikali na vyombo vyake vyote, watu au mamlaka yoyote yenye kutekeleza madaraka ya utawala, kutunga sheria au ya utoaji haki, vitakuwa na jukumu na wajibu wa kuzingatia na kutekeleza masharti yote ya Sura hii.
(2) Masharti ya Sura hii hayatatiliwa nguvu ya kisheria na mahakama yoyote. Mahakama yoyote nchini haitakuwa na uwezo wa kuamua juu ya suala kama kutenda au kukosa kutenda jambo kwa mtu au mahakama yoyote, au kama sheria, au hukumu yoyote, inaambatana na masharti ya Sura hii.

SEHEMU YA TANO
SERA YA MAMBO YA NJE
Sera ya Mambo ya Nje
22.-(1) Sera ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Muungano inalenga na kuzingatia maslahi ya Taifa na mamlaka kamili ya nchi na kwamba sera hiyo inatekelezwa kwa uwazi ili:
(a) kukuza ujirani mwema, ushirikiano wa kikanda na wa kimataifa;
(b) kukuza maendeleo na ushirikiano wa kiuchumi wenye tija kwa Taifa na raia wake;
(c) kuunga mkono na kuendeleza jitihada za kuimarisha Umoja wa Afrika, sera ya kutofungamana na upande wowote, na kukuza ushirikiano na nchi zinazoendelea duniani;
(d) kuheshimu sheria za kimataifa;
(e) kuzingatia mikataba ya kimataifa na ya kikanda yenye maslahi kwa Jamhuri ya Muungano na kutatua migogoro ya kimataifa kwa njia ya majadiliano, usuluhishi, maridhiano au mahakama;
(f) kukuza, kulinda na kuzingatia haki za binadamu na uhuru wa watu;
(g) kupambana na makosa ya kimataifa ya jinai; na
(h) kuheshimu uhuru wa mataifa mengine.
(2) Bunge litatunga sheria, pamoja na mambo mengine, itakayoelekeza na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje.

SURA YA TATU
ARDHI, MALIASILI NA MAZINGIRA
Ardhi katika Jamhuri ya Muungano
23.-(1) Ardhi katika Jamhuri ya Muungano ndiyo rasilimali kuu kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi, kijamii na ustawi wa nchi na watu wake wote. Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zitaweka mipango bora ya matumizi endelevu ya ardhi kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
(2) Ardhi yote itamilikiwa, itatumiwa na itasimamiwa kama itakavyoainishwa na sheria zitakazotungwa na Bunge au Baraza la Wawakilishi, kwa kadri itakavyokuwa, kwa kuzingatia misingi ifuatayo:
(a) raia wa Tanzania pekee ndiye atakayekuwa na haki ya kumiliki ardhi ya Tanzania, na haki hiyo italindwa kwa mujibu wa Katiba hii;
(b) mtu ambaye siyo raia wa Tanzania atakuwa na fursa ya kutumia ardhi kwa ajili ya uwekezaji na maendeleo mengine ya kiuchumi na makaazi;
(c) haki ya kumiliki, kutumia, kuendeleza na kuhifadhi ardhi kwa ajili ya mtu yeyote au makundi ya jamii yakiwemo wakulima, wavuvi, wafugaji, wachimbaji madini na makundi madogo itatambuliwa na kulindwa kwa mujibu wa Katiba hii; na
(d) kila mwanamke atakuwa na haki ya kupata, kumiliki, kutumia, kuendeleza na kusimamia ardhi kwa masharti yale yale kama ilivyo kwa mwanaume.
Matumizi bora ya ardhi
24. Bunge au Baraza la Wawakilishi, kwa kadri itakavyokuwa, litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu mgawanyo na matumizi bora ya ardhi kwa makundi mbalimbali ya jamii.

Fidia
25. Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 47(2), Serikali itaweka utaratibu wa kisheria kwa ajili ya malipo ya fidia stahiki endapo eneo au sehemu ya ardhi itachukuliwa kwa matumizi ya maendeleo ya kiuchumi na ya kijamii.

Maliasili
26. Maliasili zote za Taifa ikiwa ni pamoja na madini, gesi na mafuta ni mali ya umma, na Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaweka utaratibu wa kuhakikisha zinatumika kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.

Mazingira
27. Serikali itaweka mipango na mikakati mahsusi kwa ajili ya:
(a) kuhakikisha matumizi endelevu, usimamizi na uhifadhi wa mazingira na maliasili, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo;
(b) kusimamia na kutunza maeneo ya kihistoria na ya kale kwa manufaa ya wananchi wote;
(c) kuhakikisha kuwa taasisi za umma na asasi za kiraia zinawajibika kusimamia utekelezaji wa matakwa ya kisheria katika kulinda na kuhifadhi mazingira; na
(d) kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania ndio wenye haki ya kumiliki rasilimali za kijenetiki za Tanzania kwa manufaa ya Taifa.

SURA YA NNE
MAADILI NA MIIKO YA UONGOZI NA UTUMISHI WA UMMA

SEHEMU YA KWANZA
MAADILI YA UONGOZI NA UTUMISHI WA UMMA
Dhamana ya uongozi wa umma
28.-(1) Madaraka anayopewa kiongozi wa umma:
(a) ni dhamana na atatumia madaraka hayo na kutekeleza wajibu wake kwa:
(i) kuzingatia masharti ya Katiba hii;
(ii) kuheshimu wananchi;
(iii) kukuza hadhi ya Taifa na kulinda heshima ya ofisi anayoitumikia; na
(iv) kukuza heshima ya ofisi kwa wananchi;
(b) yanatoa wajibu kwa kiongozi kuwatumikia wananchi.
(2) Mtu mwenye dhamana ya uongozi wa umma atazingatia mambo yafuatayo:
(a) anapokuwa anafanya uamuzi wa uteuzi atahakikisha kwamba anafanya uteuzi bila ubaguzi ila kwa kuzingatia uwezo, sifa na mwenendo unaofaa;
(b) anakapokuwa anafanya uamuzi wowote katika jambo lolote la umma atahakikisha uamuzi wake hautokani na udugu, ukabila, udini, rushwa au ubaguzi wa aina yoyote;
(c) utoaji wa huduma pasipo upendeleo na kwa kufuata maslahi ya umma kwa kuonesha:
(i) uwazi, ukweli na uaminifu katika utekelezaji wa kazi za umma; na
(ii) wajibu wa kutangaza maslahi binafsi ili kuepuka mgongano wa maslahi;
(d) uwajibikaji kwa umma katika kufanya uamuzi na katika utendaji; na
(e) uadilifu, nidhamu na kujituma katika kutoa huduma kwa umma.

Kanuni za uongozi wa umma
29.-(1) Kiongozi wa umma, akiwa katika kazi za ofisi au kazi binafsi au wakati amejumuika na watu wengine, atahakikisha kwamba mwenendo wake:
(a) hauruhusu kutokea mgongano wa maslahi kati ya maslahi binafsi na maslahi ya utumishi wa umma;
(b) haushushi hadhi ya ofisi anayofanyia kazi; au
(c) hauruhusu matumizi ya ofisi ya umma kwa maslahi binafsi.
(2) Kwa madhumuni ya Katiba hii, Bunge litatunga sheria itakayoweka, pamoja na mambo mengine:
(a) tafsiri ya neno zawadi, aina, thamani, kiwango na uhifadhi wa zawadi ambayo kiongozi anapokea wakati akitekeleza majukumu yake;
(b) masharti ya kufungua akaunti za nje kwa kiongozi wa umma;
(c) masharti ya kumtaka kiongozi wa umma kutoa tamko la mali na thamani yake, madeni yake pamoja na ya mwenza wake wa ndoa na mtoto wake aliye chini ya umri wa miaka kumi na nane;
(d) masharti ya kuzuia kiongozi wa umma kutoshiriki kufanya uamuzi wa jambo au shughuli yoyote ambayo ana maslahi nayo yeye binafsi, mwenza wake wa ndoa, mtoto wake, jamaa au rafiki yake au mtu yeyote wa karibu;
(e) masharti ya matumizi ya mali ya umma;
(f) utaratibu wa utwaaji wa mali za kiongozi wa umma zinazopatikana kwa kukiuka sheria;
(g) utaratibu wa kumwajibisha kiongozi wa umma aliyekiuka maadili na miiko ya uongozi wa umma; na
(h) mambo yasiyotakiwa kwa watumishi wa umma.
(3) Wadhifa wa “kiongozi wa umma” kama ulivyotumika katika Sehemu hii utajumuisha kiongozi wa kuchaguliwa au kuteuliwa kama itakavyoainishwa kwenye sheria za nchi.
(4) Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu utakaowezesha kuanzishwa kwa mitaala inayohusu Katiba, maadili na uraia shuleni na vyuoni.

SEHEMU YA PILI
MIIKO YA UONGOZI WA UMMA
Utii wa miiko ya uongozi wa umma
30.-(1) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, kiongozi wa umma ataheshimu na kutii maadili ya uongozi wa umma na miiko ya uongozi.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoainisha:
(a) miiko inayopaswa kuzingatiwa na viongozi wa umma;
(b) utaratibu wa kumuondoa kazini kiongozi wa umma kutokana na kuvunja miiko na kukiuka maadili ya uongozi wa umma;
(c) vitendo ambavyo kiongozi wa umma hapaswi kuvitenda; na
(d) ngazi au orodha ya viongozi wa umma wanaofungwa na Sehemu hii.
Marufuku kwa baadhi ya vitendo
31.-(1) Mtumishi wa umma aliye katika ajira ya kudumu hataruhusiwa kuingia katika ajira nyingine yoyote ya kudumu yenye malipo ya mshahara.
(2) Mtumishi wa umma haruhusiwi kugombea au kuteuliwa kushika nafasi ya madaraka katika chama cha siasa au nafasi ya madaraka ya kisiasa ya aina yoyote chini ya Katiba hii.
(3) Endapo mtumishi wa umma anayefungwa na masharti ya Ibara ya 30(2)(d) ataamua kugombea au atateuliwa kushika:
(a) nafasi ya madaraka ya kisiasa ya aina yoyote chini ya Katiba hii; au
(b) uongozi wa ngazi yoyote katika chama cha siasa,
mtumishi huyo atachukuliwa kuwa utumishi wake umekoma tangu siku ya kuteuliwa kuwa mgombea au kuteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya kisiasa au uongozi katika chama cha siasa.

SURA YA TANO
HAKI ZA BINADAMU, WAJIBU WA RAIA, JAMII NA MAMLAKA YA NCHI

SEHEMU YA KWANZA
HAKI ZA BINADAMU
Uhuru, utu na usawa wa binadamu
32.-(1) Binadamu wote huzaliwa huru na wote ni sawa.
(2) Kila mtu anayo haki ya kuheshimiwa, kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.

Haki ya kuishi
33. Kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata hifadhi ya maisha yake kutoka katika Serikali na jamii kwa mujibu wa sheria za nchi.

Haki ya kutobaguliwa
34.-(1) Watu wote ni sawa na wanayo haki ya kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria.
(2) Ni marufuku kwa mtu yeyote kubaguliwa na mtu, mamlaka ya nchi
au mamlaka yoyote inayotekeleza madaraka yake chini ya sheria yoyote au katika kutekeleza kazi au shughuli yoyote ya mamlaka ya nchi.
(3) Ni marufuku kwa sheria yoyote iliyotungwa na mamlaka yoyote katika Jamhuri ya Muungano kuweka sharti lolote ambalo ni la ubaguzi ama wa dhahiri au kwa taathira yake.
(4) Haki ya raia, wajibu na maslahi ya kila mtu na jumuiya ya watu yatalindwa na kuamuliwa na mahakama na vyombo vinginevyo vya mamlaka ya nchi vilivyowekwa kwa mujibu wa sheria za nchi.
(5) Kwa madhumuni ya masharti ya Ibara hii, neno “kubagua” maana yake ni kutimiza utashi, haki au mahitaji mengineyo kwa watu mbalimbali kwa kuzingatia utaifa wao, kabila, mahali walipotokea, maoni yao ya kisiasa, rangi, dini, jinsi, ulemavu au hali yao katika jamii kwa namna ambayo watu wa aina fulani wanatendewa au kuhesabiwa kuwa dhaifu au duni na kuwekewa vikwazo au masharti ya vipingamizi ambapo watu wa aina nyingine wanatendewa tofauti au wanapewa fursa au faida iliyoko nje ya masharti au sifa za lazima.
(6) Neno “kubagua” lilivyotumiwa katika ibara ndogo ya (2), halitafafanuliwa kwa namna ambayo itaizuia mamlaka ya nchi kuchukua hatua za makusudi zenye lengo la kurekebisha matatizo mahsusi katika jamii.
(7) Kwa madhumuni ya kuhakikisha usawa mbele ya sheria, mamlaka ya nchi itaweka utaratibu unaofaa na unaozingatia misingi kwamba:
(a) wakati haki na wajibu kwa mtu yeyote vinapohitajika kufanyiwa uamuzi na mahakama au mamlaka nyingine inayohusika, basi mtu huyo atakuwa na haki ya kupewa fursa ya kusikilizwa kwa ukamilifu na pia atakuwa na haki ya kukata rufaa au kupata nafuu nyingine ya kisheria kutokana na uamuzi wa mahakama au mamlaka nyingine inayohusika;
(b) ni marufuku kwa mtu aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu aliyehukumiwa kwa kutenda kosa hilo isipokuwa tu kama itathibitika mahakamani kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo;
(c) ni marufuku kwa mtu kuadhibiwa kwa sababu ya kitendo chochote ambacho wakati alipotenda kitendo hicho hakikuwa ni kosa chini ya sheria;
(d) ni marufuku kwa mtu kupewa adhabu ambayo ni kubwa kuliko adhabu iliyokuwapo wakati kosa linalohusika lilipotendeka;
(e) kwa ajili ya kuhifadhi haki ya usawa wa binadamu, heshima ya mtu na faragha italindwa katika shughuli zote zinazohusu upelelezi wa tuhuma na uendeshaji wa mashtaka ya jinai na katika shughuli nyingine ambazo mtu anakuwa katika kizuizi cha mamlaka ya nchi au katika kuhakikisha utekelezaji wa adhabu; na
(f) ni marufuku kwa mtu kuteswa, kufanyiwa ukatili au kupewa adhabu zinazotweza au kudhalilisha utu wake.
Haki ya kutokuwa
35.-(1) Kila mtu ana haki ya kutotendewa au kutotumikishwa kama
mtumwa, kutofanyishwa kazi za kulazimisha au kutweza, na kwa msingi huo, ni marufuku kwa mtu:
(a) kufanywa au kutendewa kama mtumwa; na
(b) kusafirishwa kwa nia ya kufanywa mtumwa, kibiashara au kwa faida ya mtu mwingine.
(2) Biashara haramu ya kusafirisha na kuuza binadamu ni marufuku katika Jamhuri ya Muungano.
Uhuru wa mtu binafsi
36.-(1) Kila mtu ana haki ya kuwa huru na kuishi akiwa mtu huru.
(2) Kwa madhumuni ya kuhifadhi haki ya mtu kuwa huru na kuishi kwa uhuru, itakuwa ni marufuku kwa mtu yeyote kukamatwa, kufungwa, kufungiwa, kuwekwa kizuizini, kuhamishwa kwa nguvu au kunyang’anywa uhuru wake vinginevyo, isipokuwa tu katika:
(a) hali na kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria; au
(b) kutekeleza hukumu, amri au adhabu iliyotolewa na mahakama kutokana na shauri au kutiwa hatiani kwa kosa la jinai.
Haki ya faragha na usalama wa mtu
37.-(1) Kila mtu anastahili kuheshimiwa na kupata hifadhi kwa nafsi yake, maisha yake binafsi na familia yake na unyumba wake, na pia heshima na hifadhi ya maskani yake na mawasiliano yake ya binafsi.
(2) Kwa madhumuni ya kuhifadhi haki ya mtu kwa mujibu wa ibara hii, mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa sheria kuhusu hali, namna na kiasi ambacho haki ya mtu ya faragha na ya usalama wa nafsi yake, mali na maskani yake, yanaweza kuingiliwa bila kuathiri masharti ya Ibara hii.
Uhuru wa mtu kwenda anakotaka
38.-(1) Kila raia ana haki ya kwenda kokote katika Jamhuri ya Muungano na kuishi katika sehemu yoyote, kutoka nje ya nchi na kuingia, na pia haki ya kutoshurutishwa kuhama au kufukuzwa kutoka katika Jamhuri ya Muungano.
(2) Kitendo chochote halali au sheria yoyote yenye madhumuni ya:
(a) kupunguza uhuru wa mtu kwenda anakotaka na kumweka chini ya ulinzi au kifungoni; au
(b) kuweka mipaka kwa matumizi ya uhuru wa mtu kwenda anakotaka ili:
(i) kutekeleza hukumu au amri ya mahakama;
(ii) kumlazimisha kutimiza kwanza wajibu wowote anaotakiwa na sheria nyingine kuutimiza; au
(iii) kulinda maslahi ya umma kwa jumla au kuhifadhi maslahi mahsusi au maslahi ya sehemu fulani ya umma,
hakitahesabiwa au sheria hiyo haitahesabiwa kuwa ni kinyume cha masharti ya Ibara hii.
Uhuru wa maoni
39.-(1) Kila mtu:
(a) ana haki na uhuru wa:
(i) kuwa na maoni na kueleza fikra zake;
(ii) kufanya mawasiliano na kutoingiliwa katika mawasiliano yake;
(iii) kufanya ugunduzi, ubunifu na utafiti wa sanaa, sayansi na mapokeo ya asili;
(b) ana haki ya kupewa taarifa wakati wowote kuhusu:
(i) matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi;
(ii) utekelezaji wa mamlaka ya nchi kuhusu sera za kitaifa na shughuli za maendeleo ya jamii; na
(iii) masuala mengine muhimu kwa jamii.
(2) Utekelezaji wa haki zilizoainishwa katika ibara ndogo ya (1), hautajumuisha kuchochea vita, machafuko na chuki kwa misingi ya rangi, ukabila, jinsi, itikadi, dini au masuala yoyote yanayoweza kuleta madhara kwa Taifa.
Uhuru wa habari na vyombo vya habari
40.-(1) Kila mtu ana haki na uhuru wa:
(a) kutafuta, kupata, kutumia na kusambaza habari na taarifa sahihi; na
(b) kuanzisha vyombo vya habari na njia nyingine za upashanaji wa habari.
(2) Vyombo vya habari vitakuwa huru na vitakuwa na:
(a) haki ya kutafuta, kupata, kutumia na kusambaza habari na taarifa wanazozipata;
(b) wajibu wa:
(i) kusambaza habari na taarifa sahihi na za ukweli kwa wananchi;
(ii) kuheshimu faragha na kulinda utu, heshima, uhuru na staha ya wananchi katika habari na taarifa wanazozitumia, wanazozitayarisha na kuzisambaza; na
(iii) kuzingatia miiko ya taaluma ya uandishi na utangazaji wa habari.
(3) Serikali na taasisi zake, zitakuwa na wajibu wa kutoa taarifa kwa umma kuhusu shughuli za Serikali na utekelezaji wake, kwa kadri itakavyohitajika.
(4) Bunge litatunga sheria kwa ajili ya kusimamia na kulinda:
(a) haki, wajibu na uhuru wa vyombo vya habari na waandishi wa habari; na
(b) habari na taarifa kwa madhumuni ya usalama wa Taifa, amani, haki, staha na uhuru wa watu wengine.

Uhuru wa imani ya dini
41.-(1) Kila mtu ana uhuru wa mawazo, dhamiri, imani na uchaguzi katika mambo ya imani ya dini na anao uhuru pia wa kubadilisha dini, imani yake au kutokuwa na imani na dini.
(2) Kazi ya kutangaza dini, kufanya ibada na kueneza dini itakuwa ni huru na jambo la hiari kwa mtu binafsi ilimradi hakiuki sheria za nchi.
(3) Shughuli ya uendeshaji wa jumuiya za dini itakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya Serikali.
(4) Hifadhi ya haki zilizotajwa katika Ibara hii itakuwa chini ya utaratibu utakaowekwa na sheria ambazo ni muhimu katika jamii ya kidemokrasia kwa ajili ya usalama, amani, maadili na umoja wa jamii na wa kitaifa na vitasimamiwa kwa utaratibu utakaoainishwa kwenye sheria za nchi.
(5) Ni marufuku kwa mtu, kikundi au taasisi ya dini kutumia uhuru wa kutangaza dini kwa namna ambayo italeta uvunjifu wa amani, kujenga chuki au kuchochea vurugu na ghasia kwa madai ya kutetea imani au dini hiyo.
(6) Dini na imani ya dini haitatumika kwa namna yoyote itakayowagawa wananchi, kuleta uhasama au uvunjifu wa amani miongoni mwa wananchi.
(7) Neno “dini” kama lilivyotumika katika Ibara hii litatafsiriwa kwamba maana yake ni pamoja na madhehebu ya dini, na maneno mengine yanayofanana au kuambatana na neno hilo nayo yatatafsiriwa kwa maana hiyo.
Uhuru wa mtu kujumuika na kushirikiana na wengine
42. Kila mtu anastahili kuwa huru bila kuathiri sheria za nchi, kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kujumuika na kushirikiana na watu wengine, kutoa mawazo hadharani, na kwa ajili hiyo kuanzisha au kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo.

Uhuru wa kushiriki shughuli za utawala wa nchi
43.-(1) Kila raia wa Jamhuri ya Muungano ana haki ya kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi kwa hiari yake, ama moja kwa moja au kupitia wawakilishi waliochaguliwa na wananchi, kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria za nchi.
(2) Kila raia wa Jamhuri ya Muungano ana haki na uhuru wa kushiriki kwa ukamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomhusu, maisha yake au yanayolihusu Taifa.

Haki ya kufanya kazi
44.-(1) Kila mtu ana haki ya kufanya kazi ya kuajiriwa au kujiajiri mwenyewe na kupata ujira unaostahili.
(2) Kila raia ana haki na fursa sawa kushika nafasi yoyote ya kazi, uongozi au shughuli yoyote iliyo chini ya mamlaka ya nchi.

Haki za wafanyakazi na waajiri
45.-(1) Kila mfanyakazi ana haki zifuatazo:
(a) kufanya kazi bila ubaguzi wa aina yoyote;
(b) kupata ujira na malipo halali kulingana na kiasi na sifa za kazi anayofanya;
(c) kuunda au kujiunga na chama cha wafanyakazi mahali pa kazi;
(d) kushiriki katika shughuli za chama cha wafanyakazi;
(e) kupata hifadhi ya afya na usalama wake katika sehemu ya kazi; na
(f) kugoma kutokana na mgogoro wa kimaslahi kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge.
(2) Kila mwajiri ana haki ya:
(a) kujiunga na chama cha waajiri;
(b) kumfungia nje mfanyakazi kutokana na mgogoro wa kimaslahi kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge.
(3) Kila chama cha waajiri au wafanyakazi kitakuwa na haki ya:
(a) kuamua kuhusu uongozi, programu na shughuli zake; na
(b) kuanzisha, kujiunga na kusimamia shirikisho lao.
(4) Kila chama cha wafanyakazi kitakuwa na haki ya kufanya majadiliano ya pamoja na mwajiri na kuingia mikataba ya hali bora ya kazi.
(5) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), mfanyakazi katika kutekeleza haki yake ya mgomo kwa mujibu wa Ibara hii, atatakiwa asiwe:
(a) ameajiriwa katika huduma maalum zitakazoainishwa na sheria;
(b) amefungwa na makubaliano yanayotaka jambo linalobishaniwa kupelekwa kwenye usuluhishi;
(c) amefungwa na mkataba wa hiari au tuzo ya usuluhishi inayoratibu jambo linalobishaniwa; au
(d) anabanwa na uamuzi wa ajira unaoratibu suala hilo linalobishaniwa.
(6) Kwa madhumuni ya Ibara hii “mgogoro wa kimaslahi” maana yake ni mgogoro kuhusu haki zinazotarajiwa, ikiwa ni pamoja na ongezeko la mishahara au maslahi mengine zaidi ya yale yaliyokwishatolewa kisheria au yatokanayo na mkataba wa ajira.
(7) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu haki za waajiri na wafanyakazi na utaratibu utakaowezesha waajiri na wafanyakazi kutumia haki zao.

Haki za wakulima, wafugaji, wavuvi na wachimbaji madini
46.-(1) Wakulima, wafugaji, wavuvi na wachimbaji madini watakuwa na haki ya:
(a) kumiliki, kutumia na kuendeleza ardhi kwa ajili ya shughuli zao;
(b) kupata taarifa na maarifa kwa lengo la kuboresha kilimo, ufugaji, uvuvi na uchimbaji madini;
(c) kumiliki na kunufaika na rasilimali za kijenetiki za kilimo, mifugo na uvuvi; na
(d) kushirikishwa katika utungaji wa sera, sheria na mipango mbalimbali inayohusu shughuli zao.
(2) Mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa kisheria kwa madhumuni ya kubainisha na kutenga maeneo ya ardhi kwa ajili ya matumizi ya kila kundi lililoainishwa katika ibara ndogo ya (1).

Haki ya kumiliki mali
47.-(1) Kila mtu ana haki ya kumiliki mali na hifadhi ya mali yake kwa mujibu wa sheria za nchi.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), itakuwa ni marufuku kwa mtu yeyote kunyang’anywa mali yake kwa madhumuni ya kuitaifisha au madhumuni mengine bila ya idhini ya sheria ambayo inaweka masharti ya kutoa fidia inayolingana na thamani halisi.
(3) Kwa madhumuni ya masharti ya Ibara hii, haki ya umiliki na hifadhi ya mali haitahusu mali iliyothibitishwa kwamba haikupatikana kwa njia halali.

Haki ya mtuhumiwa na mfungwa
48.-(1) Mtu aliyekamatwa au aliyewekwa kizuizini ana haki ya:
(a) kuelezwa kwa lugha anayoifahamu:
(i) sababu ya kukamatwa kwake;
(ii) haki ya kutokutoa maelezo yoyote; na
(iii) matokeo ya kutoa maelezo;
(b) kuwasiliana na wakili au mtu mwingine ambaye msaada wake ni
muhimu kwa mtuhumiwa;
(c) kutolazimishwa kutoa maelezo ya kukiri kosa ambayo yatatumika kama ushahidi dhidi yake;
(d) kufikishwa mahakamani mapema iwezekanavyo kama itakavyoelekezwa katika sheria; na
(e) kuwekwa katika mazingira yanayozingatia haki za binadamu.
(2) Mtu anayetumikia kifungo ana haki ya:
(a) kuhifadhiwa katika mazingira yanayozingatia haki za binadamu;
(b) kupata nakala ya mwenendo wa mashtaka na nakala ya hukumu kwa madhumuni ya kukata rufaa;
(c) kuwasiliana na wakili au mtu mwingine ambaye msaada wake ni muhimu katika kukata rufaa.
(3) Bunge litatunga sheria itakayoweka utaratibu utakaowezesha:
(a) mtuhumiwa kupata nakala ya mashtaka yanayomkabili;
(b) mtuhumiwa kufikishwa mahakamani na kuomba dhamana kwa mujibu wa sheria; na
(c) mfungwa kupata kumbukumbu ya nakala ya mashtaka na hukumu baada ya shauri kukamilika mahakamani.
(4) Kwa ajili ya kuhifadhi haki zilizotajwa katika ibara hii, mamlaka ya nchi itazingatia masharti ya Ibara ya 34(7)(e).

Haki ya mtu aliye chini ya ulinzi au kizuizi
49.-(1) Mtu aliye katika kizuizi au ulinzi ataendelea kuwa na haki zote za msingi zilizoainishwa katika Katiba hii kwa kiwango anachostahiki katika mazingira ya kuwekwa kizuizini au katika ulinzi.
(2) Mtu aliye katika kizuizi au ulinzi ana haki ya kuiomba mahakama ili mamlaka ya nchi inayomhifadhi kueleza sababu za yeye kuwekwa au kuendelea kuwa katika kizuizi au ulinzi.
(3) Raia wa Jamhuri ya Muungano hatapelekwa katika nchi ya nje yoyote kujibu mashtaka au kufanyiwa mahojiano ya aina yoyote kinyume cha ridhaa yake, isipokuwa kwa mujibu wa sheria za nchi na mikataba ya kimataifa na wajibu wa nchi katika uhusiano wa kimataifa.

Uhuru na haki ya mazingira safi na salama
50.-(1) Kila mtu anayeishi katika Jamhuri ya Muungano ana haki ya kuishi katika mazingira safi, salama na ya kiafya.
(2) Haki ya kuishi katika mazingira safi, salama na ya kiafya inahusisha haki kwa kila mtu kutumia maeneo ya umma au sehemu mbalimbali za mazingira yaliyotengwa kwa madhumuni ya burudani, elimu, afya, ibada, utamaduni na shughuli za kiuchumi.
(3) Mtu yeyote anayeishi katika Jamhuri ya Muungano anao wajibu wa kutunza, kulinda na kuhifadhi mazingira na kutoa taarifa kwa mamlaka za nchi kuhusu shughuli au jambo lolote ambalo ni la hatari au lina uwezekano mkubwa wa kuharibu au kuathiri mazingira.

Haki ya afya na maji safi na salama
51.-(1) Kila mtu ana haki ya kupata huduma ya afya na maji safi na salama.
(2) Mamlaka ya nchi itahakikisha kwamba huduma zilizorejewa katika
ibara ndogo ya (1) zinapatikana kwa urahisi kwa kuzingatia mahitaji ya nchi na rasilimali zilizopo.

Haki ya elimu
52.-(1) Kila mtu ana haki ya kupata elimu bora ya msingi inayomtayarisha kikamilifu kuendelea na elimu ya ngazi inayofuatia au kuweka msingi wa kuanza kujitegemea.
(2) Kila mtu ana fursa ya kupata elimu ya juu ilimradi ana sifa stahiki.
(3) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (2), kila mtu ana haki ya kuchagua taaluma na ajira anayoitaka kwa mujibu wa elimu yake na ujuzi alionao.
(4) Serikali itahakikisha kuwepo kwa mfumo wa elimu unaozingatia uwezo na mahitaji ya Taifa.

Haki za mtoto
53.-(1) Kila mtoto ana haki ya:
(a) kupewa jina, uraia na kusajiliwa;
(b) kutoa mawazo, kusikilizwa na kulindwa dhidi ya uonevu, ukatili, udhalilishaji, utumikishwaji na mila potofu;
(c) kuwekewa mazingira bora ya kucheza na kupata elimu ya msingi;
(d) kuhifadhiwa katika mazingira mazuri, kwa walio katika ukinzani na sheria;
(e) kupata lishe bora, huduma ya afya, makaazi na mazingira yanayomjenga kimwili, kiakili na kimaadili;
(f) kushiriki katika shughuli zinazolingana na umri alionao; na
(g) kupata malezi na ulinzi kutoka kwa wazazi, walezi, jamii au mamlaka ya nchi, bila ya ubaguzi wowote.
(2) Itakuwa ni wajibu wa kila mzazi, mlezi, jamii na mamlaka ya nchi kuhakikisha kuwa watoto wanalelewa katika maadili stahiki kwa umri wao.
(3) Kwa madhumuni ya Ibara hii “mtoto” maana yake ni mtu mwenye umri wa chini ya miaka kumi na nane.

Haki na wajibu wa vijana
54.-(1) Kila kijana ana haki na wajibu wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya Jamhuri ya Muungano pamoja na jamii kwa ujumla, na kwa mantiki hiyo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano na jamii zitahakikisha kuwa vijana wanawekewa mazingira mazuri ya kuwa raia wema na kupatiwa fursa za kushiriki kikamilifu katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), Bunge litatunga sheria itakayosimamia, pamoja na mambo mengine, uanzishwaji, muundo, majukumu na uendeshaji wa Baraza la Vijana la Taifa.

Haki za watu wenye ulemavu
55. Mtu mwenye ulemavu ana haki ya:
(a) kuheshimiwa, kutambuliwa na kulindwa dhidi ya vitendo vinavyoshusha utu wake ikiwemo ubaguzi, uonevu, ukatili na mila potofu;
(b) kupata elimu kwa kutumia vifaa maalum na kushiriki katika nafasi za uwakilishi na shughuli za kijamii;
(c) kuwekewa miundombinu na mazingira yanayofaa yatakayomwezesha kwenda anapotaka, kutumia vyombo vya usafiri na kupata habari;
(d) kutumia lugha ya alama, alama mguso, maandishi ya nukta nundu, maandishi yaliyokuzwa au njia nyingine zinazofaa;
(e) kupata ajira na kufanya kazi; na
(f) kupata huduma bora za afya, uzazi salama, marekebisho na utengemao.

Haki za makundi madogo katika jamii
56.-(1) Mamlaka ya nchi kwa kuzingatia rasilimali na uwezo wa nchi, itaweka utaratibu wa sheria utakaowezesha makundi madogo katika jamii:
(a) kushiriki katika uongozi wa mamlaka za nchi;
(b) kupewa fursa maalum za elimu kujiendeleza kiuchumi na ajira; na
(c) kutengewa maeneo ya ardhi ambayo kwa desturi, makundi hayo huyatumia kama maeneo ya kuishi na kupata riziki ya chakula.
(2) Serikali na mamlaka ya nchi itachukua hatua za makusudi za kukuza na kuendeleza shughuli za kiuchumi na kuweka miundombinu ya makaazi, elimu, maji na afya kwa ajili ya kizazi cha sasa na vijavyo vya jamii ya watu walio katika makundi madogo.
(3) Kwa madhumuni ya Ibara hii, “makundi madogo” maana yake ni jamii za watu wanaoishi kwa kutegemea uoto wa asili na mazingira yanayowazunguka kwa ajili ya chakula, malazi na mahitaji mengine ya maisha.

Haki za wanawake
57. Kila mwanamke ana haki ya:
(a) kuheshimiwa, kuthaminiwa na kutambuliwa utu wake;
(b) kulindwa dhidi ya ubaguzi, udhalilishaji, dhuluma, unyanyasaji, ukatili wa kijinsia na mila potofu;
(c) kushiriki bila ya ubaguzi katika uchaguzi na ngazi zote za maamuzi;
(d) kupata fursa na ujira sawa na mwanaume katika kazi zenye sifa zinazofanana;
(e) kulindwa ajira yake wakati wa ujauzito na pale anapojifungua;
(f) kupata huduma bora ya afya ikiwemo afya ya uzazi salama; na
(g) kumiliki mali.

Haki za wazee
58. Mamlaka ya nchi itaweka utaratibu utakaowezesha wazee kupata haki ya:
(a) kushiriki katika shughuli za kimaendeleo na kijamii;
(b) kuendesha maisha yake na kujiendeleza kulingana na uwezo wake ikiwa ni pamoja na kufanya kazi;
(c) kupata huduma za matibabu;
(d) kulindwa dhidi ya unyonyaji, vitendo vya ukatili ikiwemo mateso na mauaji;
(e) kuwekewa miundombinu na mazingira bora yatakayowawezesha kwenda wanakotaka na kutumia vyombo vya usafiri wa umma kwa gharama nafuu; na
(f) kupata mahitaji ya msingi kutoka kwenye familia yake, jamii na inapobidi mamlaka ya nchi.
Uhuru wa taaluma, ubunifu, ugunduzi na usanii
59.-(1) Kila mtu atakuwa na uhuru wa kushiriki kwenye mambo yanayoendeleza na kukuza sanaa, taaluma, ubunifu na ugunduzi.
(2) Kila mtu atakuwa na uhuru wa kujifunza, kufundisha, kutafiti na kueneza matumizi ya matokeo ya utafiti kulingana na kanuni za kitaaluma na za kiutafiti.
(3) Serikali itakuza na kuendeleza utafiti, ubunifu na ugunduzi katika sanaa, sayansi na teknolojia kwa kutunga sheria ambazo:
(a) zitalinda hakimiliki na hataza na haki za wabunifu, watafiti na wasanii;
(b) zitawezesha taasisi za elimu na za utafiti kutumia ugunduzi wao kwa manufaa ya Taifa;
(c) zitasimamia uhamishaji wa sayansi na teknolojia;
(d) zitawezesha kukuza rasilimali watu kwenye nyanja za kitaaluma, sayansi, teknolojia na ubunifu;
(e) zitalinda na kusimamia ubora wa taaluma, utafiti na matumizi ya ugunduzi na ubunifu; na
(f) zitafafanua mambo mengine yanayohusu hakimiliki na hataza.

SEHEMU YA PILI
WAJIBU WA RAIA, JAMII NA MAMLAKA YA NCHI NA MIPAKA YA HAKI ZA BINADAMU
(a) Wajibu wa Raia na Jamii kwa Taifa
Wajibu wa raia na jamii
60.-(1) Kila raia ana wajibu wa:
(a) kuilinda na kuitetea Katiba ya Jamhuri ya Muungano; na
(b) kuilinda Jamhuri ya Muungano na kushiriki katika ulinzi wa Taifa.
(2) Kila mtu ana wajibu wa:
(a) kuitii Katiba hii na sheria za nchi;
(b) kulinda na kuheshimu Tunu za Taifa na vitu muhimu vya utambulisho na urithi wa Taifa;
(c) kulipa kodi kwa mujibu wa sheria; na
(d) kuheshimu haki, uhuru na maslahi ya watu wengine.

Wajibu wa kushiriki kazi
61.-(1) Kila mtu ana wajibu wa:
(a) kushiriki katika kazi halali ya uzalishaji mali; na
(b) kuwa na nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji wa mali yake binafsi na malengo ya pamoja yanayotakiwa au yaliyowekwa kwa mujibu wa sheria.
(2) Bila kujali masharti ya ibara ndogo ya (1), kazi yoyote ya shuruti, kikatili au kutweza ni marufuku katika Jamhuri ya Muungano.
(3) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (2), kazi yoyote haitahesabiwa kuwa ni kazi ya shuruti, kikatili au kutweza endapo kazi hiyo, kwa mujibu wa sheria za nchi ni:
(a) kazi ambayo haina budi ifanywe kutokana na hukumu au amri ya
mahakama;
(b) kazi ambayo haina budi kufanywa na mwanajeshi katika kutekeleza majukumu yake;
(c) kazi ambayo haina budi kufanywa kutokana na kuwapo hali ya hatari, baa au janga lolote linalotishia uhai na ustawi wa jamii; au
(d) kazi au huduma yoyote ambayo ni sehemu ya:
(i) majukumu ya kawaida ya kuhakikisha ustawi wa jamii;
(ii) ujenzi wa Taifa wa lazima kwa mujibu wa sheria za nchi; au
(iii) jitihada za Taifa za kutumia uwezo wa kila mtu kufanya kazi kwa ajili ya kuimarisha ustawi wa jamii na uchumi wa Taifa na kuhakikisha maendeleo na tija ya kitaifa.
Ulinzi wa mali ya umma
62.-(1) Kila raia anao wajibu wa kulinda na kutunza maliasili ya Taifa, mali ya mamlaka ya nchi na mali yoyote inayomilikiwa kwa pamoja na wananchi, na pia kuiheshimu mali ya mtu mwingine.
(2) Kila mtu ana wajibu wa:
(a) kupiga vita aina zote za uharibifu na ubadhirifu na kuendesha uchumi wa Taifa kwa makini kwa kuzingatia mipango endelevu na haki ya vizazi vijavyo;
(b) kutoa taarifa juu ya hujuma za maliasili za Taifa.

Haki na wajibu muhimu
63.-(1) Kila mtu anayo haki ya kufaidi haki za msingi za binadamu, na matokeo ya kila mtu kutekeleza wajibu wake kwa jamii, kama ilivyofafanuliwa katika Katiba hii.
(2) Kila mtu anayo haki ya kupata hifadhi sawa chini ya sheria za Jamhuri ya Muungano.
(3) Mtu yeyote katika Jamhuri ya Muungano hatakuwa na haki, hadhi au cheo maalum kwa misingi ya nasaba, jinsi, dini, kabila, jadi au urithi wake.
(4) Ni marufuku kwa sheria yoyote kutoa haki, hadhi au cheo maalum kwa mtu yeyote wa Jamhuri ya Muungano kwa misingi ya nasaba, jinsi, dini, kabila, jadi au urithi.
(5) Ili watu wote wafaidi haki na uhuru uliotajwa katika Katiba hii, kila mtu anao wajibu wa kutenda na kuendesha shughuli zake kwa namna ambayo haitaingilia haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma.

(b) Wajibu wa Mamlaka ya Nchi
Hifadhi ya haki za binadamu
64.-(1) Serikali na mamlaka ya nchi ina wajibu wa kuzingatia na kuhifadhi haki za binadamu ikiwa ni msingi wa uhuru kama ilivyoainishwa katika Katiba hii.
(2) Haki na uhuru wa kila mtu kama ilivyoainishwa katika Katiba hii utaheshimiwa, kuhifadhiwa na kudumishwa na mamlaka ya nchi, taasisi binafsi na kila mwananchi.

Usimamizi wa haki za binadamu
65.-(1) Katika kutafsiri masharti ya Sura hii ya Haki za Binadamu, Mahakama au chombo kingine chochote cha kufanya uamuzi kitazingatia mambo yafuatayo:
(a) sheria za kimataifa na haki za binadamu; na
(b) haki za jamii na maslahi ya jamii kwa ujumla.
(2) Mtu anayeamini kuwa masharti yaliyomo katika Sura hii yamekiukwa au yanaelekea kukiukwa na mamlaka, chombo cha uamuzi, sheria au sera yoyote dhidi yake, anaweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu kwa hati maalumu ya maombi kwa mujibu wa sheria za nchi ili kupata nafuu inayohitajika.
(3) Mahakama inaweza, kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1), kutoa maelekezo itakayoona yanafaa, kuweka zuio, katazo au kuamuru jambo lifanyike ambalo lilikuwa limezuiwa.
(4) Shauri katika Mahakama la kudai haki za kikatiba kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii laweza kufunguliwa na:
(a) Mwanasheria Mkuu;
(b) mtu anayejiwakilisha mwenyewe au taasisi inayowawakilisha wanachama wake;
(c) mtu anayemwakilisha mtu ambaye hawezi kujiwakilisha mwenyewe kwa mujibu wa sheria za nchi; au
(d) mtu anayewakilisha kundi la watu wenye malengo yanayofanana au jamii ya watu fulani ambao haki zao zimevunjwa.
(5) Endapo katika shauri lolote inadaiwa kwamba sheria yoyote iliyotungwa au hatua yoyote iliyochukuliwa na Serikali au mamlaka nyingine inafuta au inakataza haki, uhuru na wajibu muhimu utakaotokana na Ibara ya 32 hadi 59, na Mahakama Kuu kama inaridhika basi itatoa tamko kwamba sheria au hatua inayohusika ni batili au kinyume cha Katiba.
(6) Iwapo Mahakama Kuu itaona kuwa inafaa, hali au maslahi ya jamii yanahitaji hivyo, badala ya kutamka kuwa sheria au hatua hiyo ni batili, Mahakama Kuu itakuwa na uwezo wa kuamua au kutoa fursa kwa mamlaka nyingine yoyote inayohusika kurekebisha hitilafu iliyopo katika sheria au hatua inayolalamikiwa ndani ya muda utakaopangwa na Mahakama hiyo, sheria au hatua hiyo itaendelea kuwa ni halali hadi marekebisho yatakapofanywa au muda uliowekwa na Mahakama Kuu utakapokwisha, ili mradi muda mfupi zaidi ndiyo uzingatiwe.
 (c) Mipaka ya Haki za Binadamu

Mipaka ya haki za binadamu
66. Haki zote zilizoainishwa katika Sura hii endapo zitahitajika kuwekewa mipaka ni lazima mipaka hiyo itumike kwa uwazi na kidemokrasia kwa kuzingatia utu, usawa, uhuru na vigezo muhimu, ikijumuisha:
(a) aina ya haki;
(b) umuhimu na sababu za kuweka mipaka;
(c) asili na ukubwa wa mpaka husika;
(d) uhusiano baina ya mpaka husika na sababu yake;
(e) njia nyepesi ya kufikia madhumuni ya matumizi ya mpaka husika; na
(f) umuhimu wa kulinda usalama wa nchi.
Sheria kuhusu haki, uhuru na wajibu
67. Bila kuathiri masharti ya Sura hii, Bunge litatunga sheria, ambayo pamoja na mambo mengine, itasimamia matumizi na utekelezaji wa haki, uhuru na wajibu ulioainishwa katika Sura hii.

SURA YA SITA
URAIA KATIKA JAMHURI YA MUUNGANO
Uraia wa Jamhuri ya Muungano
68.-(1) Mtu ambaye, kabla ya Katiba hii kuanza kutumika, ni raia wa Jamhuri ya Muungano ataendelea kuwa raia wa Jamhuri ya Muungano.
(2) Uraia wa Jamhuri ya Muungano ni wa aina mbili na utapatikana kwa njia ya kuzaliwa au kuandikishwa.

Haki ya uraia
69. Kila raia ana haki ya kutambuliwa uraia wake na kwa madhumuni haya, mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa sheria utakaowezesha raia kupata hati ya kuzaliwa, kitambulisho cha uraia wake bila ya upendeleo na ubaguzi wa aina yoyote, na pale inapohitajika, nyaraka za kumwezesha kusafiri.

Uraia wa kuzaliwa
70.-(1) Kila mtu aliyezaliwa Tanzania Bara au Zanzibar atakuwa raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano iwapo, wakati wa kuzaliwa, mama au baba yake ni, au alikuwa raia wa Jamhuri ya Muungano.
(2) Kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, mtu aliyezaliwa nje ya Tanzania atakuwa ni raia wa Jamhuri ya Muungano wa kuzaliwa kuanzia tarehe ya kuzaliwa kwake ikiwa mama au baba yake ni raia wa Jamhuri ya Muungano.
(3) Endapo mmoja kati ya wazazi wake alifariki kabla ya mtu huyo kuzaliwa, uraia wa mzazi huyo wakati wa kifo chake utatumika kwa madhumuni ya kutambua uraia wa mtu huyo aliyezaliwa baada ya mzazi aliyefariki kana kwamba mzazi huyo alikuwa anaishi hadi kuzaliwa kwa mtu huyo.
(4) Mtoto mwenye umri chini ya miaka saba akikutwa ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano katika mazingira ambayo wazazi wake hawajulikani, atachukuliwa kuwa ni raia wa Jamhuri ya Muungano wa kuzaliwa.
(5) Endapo uraia wa wazazi wa mtoto aliyepewa uraia chini ya masharti ya ibara ndogo ya (4) utabainika kuwa si uraia wa Jamhuri ya Muungano, uraia wa mtoto huyo utasita.
(6) Bila kuathiri masharti ya Ibara hii, Bunge litatunga sheria ambayo itaweka masharti na utaratibu wa:
(a) upatikanaji wa uraia kwa watu waliozaliwa na raia wa Tanzania nje ya nchi;
(b) kurudisha uraia wa watu ambao uraia wao ulifutwa baada ya kupata uraia wa nchi nyingine; na
(c) mambo mengine ambayo yatatakiwa kutungiwa sheria.

Uraia wa kuandikishwa
71.-(1) Mara baada ya kuanza kutumika kwa Katiba hii, mtu ambaye amekuwa mkaazi wa Jamhuri ya Muungano na ambaye ametimiza masharti yote ya sheria za nchi anaweza kuomba kuandikishwa kuwa raia wa Jamhuri ya Muungano.
(2) Mtu aliyefunga ndoa na raia wa Jamhuri ya Muungano na ambaye:
(a) amedumu katika ndoa hiyo kwa kipindi cha miaka saba mfululizo; na
(b) ametimiza masharti yaliyoainishwa katika sheria kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1),
anaweza kuomba uraia wa kuandikishwa kuwa raia wa Jamhuri ya Muungano.
(3) Endapo ndoa iliyotajwa katika ibara ndogo ya (2) itavunjika, kama mtu huyo hakuukana uraia wake wa Tanzania, ataendelea kuwa raia wa Jamhuri ya Muungano.
(4) Mtoto aliyezaliwa katika ndoa iliyorejewa katika ibara ndogo ya (2), atakuwa raia wa Jamhuri ya Muungano wa kuzaliwa.
(5) Mtoto aliye na umri wa chini ya miaka kumi na nane ambaye wazazi wake si raia wa Tanzania, akiasiliwa na raia wa Jamhuri ya Muungano, kuasiliwa kwake, kutawezesha mtoto huyo kuwa raia wa Jamhuri ya Muungano wa kuandikishwa.
(6) Bunge litatunga sheria, pamoja na mambo mengine, kusimamia masuala yanayohusu uraia wa Jamhuri ya Muungano.
Hadhi maalum ya watu wenye asili au nasaba ya Tanzania
72. Bila kuathiri masharti yaliyomo kwenye Sura hii, mtu yeyote mwenye asili au nasaba ya Tanzania na ambaye ameacha kuwa raia wa Jamhuri ya Muungano kwa kupata uraia wa nchi nyingine, atakapokuwa katika Jamhuri ya Muungano, atakuwa na hadhi maalum kama itakavyoainishwa katika sheria za nchi.

SURA YA SABA
MUUNDO WA JAMHURI YA MUUNGANO
Muundo wa Muungano
73. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakuwa na muundo wa Serikali mbili ambazo ni:
(a) Serikali ya Jamhuri ya Muungano; na
(b) Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Utekelezaji wa shughuli za Mamlaka ya Nchi
74.-(1) Shughuli zote za Mamlaka ya Nchi katika Jamhuri ya Muungano zitatekelezwa na kudhibitiwa na vyombo viwili vyenye mamlaka ya utendaji, vyombo viwili vyenye mamlaka ya utoaji haki, na pia vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma.
(2) Vyombo vyenye mamlaka ya utendaji vitakuwa ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar; vyombo vyenye mamlaka ya utoaji haki vitakuwa ni Mahakama ya Jamhuri ya Muungano na Mahakama Kuu ya Zanzibar, na vyombo vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma vitakuwa ni Bunge na Baraza la Wawakilishi.
(3) Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za umma katika Jamhuri ya Muungano, na kwa ajili ya mgawanyo wa madaraka juu ya shughuli hizo baina ya vyombo vilivyotajwa katika Ibara hii, kutakuwa na Mambo ya Muungano kama yalivyoorodheshwa katika Nyongeza ya Kwanza ya Katiba hii na pia kutakuwa na mambo yasiyo ya Muungano, ambayo ni mambo mengine yote yasiyo ya Muungano.
(4) Kila chombo kilichotajwa katika Ibara hii kitaundwa na kutekeleza majukumu yake kwa kufuata masharti mengine yaliyomo katika Katiba hii.

Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano
75. Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na mamlaka ya utekelezaji katika Jamhuri ya Muungano kwa Mambo ya Muungano na kwa mambo yote yasiyo ya Muungano yanayohusu Tanzania Bara.
Mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mambo yasiyo ya Muungano
76.-(1) Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa na mamlaka na haki juu ya mambo yasiyo ya Muungano yanayohusu Zanzibar.
(2) Bila kuathiri mipaka iliyowekwa na Katiba hii, katika kutekeleza mamlaka yake chini ya ibara ndogo ya (1), Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa na uwezo na uhuru wa kuanzisha uhusiano au ushirikiano na jumuiya au taasisi yoyote ya kikanda au kimataifa.
(3) Endapo, katika kutekeleza mamlaka na majukumu yake kwa mujibu wa Ibara hii, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahitaji kupata ushirikiano kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya kufanikisha uhusiano au ushirikiano na jumuiya au taasisi ya kikanda au kimataifa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano yaweza kufanikisha uhusiano au ushirikiano huo kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii na sheria itakayotungwa na Bunge.
(4) Kwa madhumuni ya Ibara hii, Bunge litatunga sheria itakayoainisha na kufafanua:
(a) majukumu na mipaka ya utekelezaji wa mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu uhusiano au ushirikiano wa kikanda au kimataifa;
(b) utaratibu wa kushughulikia athari zinazotokana na uhusiano au ushirikiano wa kikanda au kimataifa;
(c) utaratibu wa utafutaji na upatikanaji wa mikopo na misaada kutokana na uhusiano au ushirikano huo;
(d) utaratibu au masharti ya kuvunja au kuimarisha uhusiano au ushirikiano huo;
(e) utaratibu wa mawasiliano na mashauriano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu uhusiano au ushirikiano wa kikanda au kimataifa;
(f) utaratibu wa utekelezaji wa masharti ya Ibara hii; na
(g) mambo mengine yatakayohusu uhusiano au ushirikiano wa kikanda au kimataifa chini ya Ibara hii.

Mahusiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
77.-(1) Katika kutekeleza majukumu yake katika maeneo mbalimbali, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itazingatia misingi ya kushirikiana na kushauriana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa lengo la kukuza na kulinda maslahi ya Taifa na maendeleo ya wananchi.
(2) Kwa madhumuni ya kukuza umoja na uhusiano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, zinaweza kushauriana na kushirikiana katika mambo yanayohusu uongozi, utawala, vyombo vya uwakilishi na mahakama.
(3) Utendaji wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar au chombo chochote cha Serikali hizo utatekelezwa kwa kuzingatia umoja wa Jamhuri ya Muungano na wajibu wa kukuza utaifa.
(4) Bila kuathiri masharti ya Ibara hii, Serikali ya Jamhuri ya Muungano, kwa makubaliano maalum baina yake na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, inaweza kutekeleza jambo lolote lililo chini ya mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mujibu wa makubaliano hayo.

Wajibu wa viongozi wakuu kulinda Muungano
78.-(1) Bila kuathiri wajibu wa kila raia uliotajwa katika Katiba hii, kila kiongozi mkuu mwenye mamlaka ya utendaji katika Jamhuri ya Muungano aliyetajwa katika ibara ndogo ya (3) atakuwa na wajibu, katika kutekeleza madaraka aliyopewa kwa mujibu wa Katiba hii, kuhakikisha kuwa anatetea, analinda, anaimarisha na kudumisha umoja wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
(2) Kwa madhumuni ya masharti ya ibara ndogo ya (1) kila kiongozi mkuu aliyetajwa katika ibara ndogo ya (3), kabla ya kushika madaraka yake, ataapa kuutetea, kuulinda na kuudumisha Muungano kwa mujibu wa Katiba hii.
(3) Viongozi wakuu wanaohusika na masharti ya Ibara hii ni:
(a) Rais wa Jamhuri ya Muungano;
(b) Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano;
(c) Rais wa Zanzibar;
(d) Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano; na
(e) Makamu wa Rais wa Zanzibar.

SURA YA NANE
SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO
SEHEMU YA KWANZA
SERIKALI, RAIS NA MAKAMU WA RAIS
(a) Serikali
Serikali ya Jamhuri ya Muungano
79.-(1) Kutakuwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambayo itaundwa na Rais, Makamu wa Rais na Baraza la Mawaziri.
(2) Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 74, madaraka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano yatatekelezwa na Rais mwenyewe au kwa kukasimu madaraka hayo kwa mtu yeyote mwenye madaraka katika utumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano.
(3) Ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika Ibara hii hayatahesabiwa kwamba:
(a) yanahamishia kwa Rais madaraka yoyote ya kisheria yaliyowekwa na sheria mikononi mwa mtu au mamlaka yoyote ambayo si Rais;
(b) yanalizuia Bunge kukabidhi madaraka yoyote ya kisheria mikononi mwa mtu au watu au mamlaka nyingine yoyote ambayo si Rais; au
(c) yanazuia Mahakama kukabidhi madaraka yoyote ya kisheria kwa mtu au watu wenye madaraka katika Mahakama za Jamhuri ya Muungano.
(b) Rais

Rais wa Jamhuri ya Muungano
80.-(1) Kutakuwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano.
(2) Rais wa Jamhuri ya Muungano atakuwa Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Amiri Jeshi Mkuu na atakuwa:
(a) alama na taswira ya Jamhuri ya Muungano na watu wake; na
(b) alama ya umoja, uhuru wa nchi na mamlaka yake.

Madaraka na majukumu ya Rais
81.-(1) Rais atatekeleza mamlaka ya Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali, Amiri Jeshi Mkuu kwa mujibu wa Katiba hii na atakuwa na madaraka na majukumu kama yatakavyoainishwa kwenye sheria zitakazotungwa na Bunge.
(2) Rais atakuwa na mamlaka ya kutekeleza majukumu mengine ambayo kwa asili yake yanatekelezwa na Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali au Amiri Jeshi Mkuu, ambayo hayakuainishwa katika Katiba hii na ambayo hayakiuki Katiba hii na sheria zitakazotungwa na

Bunge.
Utekelezaji wa madaraka ya Rais
82.-(1) Katika utekelezaji wa madaraka ya Rais kwa mujibu wa Sura hii, Rais atakuwa na mamlaka ya kuanzisha au kufuta nafasi za madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Rais atakuwa na madaraka ya kuteua watu wa kushika nafasi za madaraka ya viongozi wanaowajibika kuweka sera za idara na taasisi za Serikali, na watendaji wakuu wanaowajibika kusimamia utekelezaji wa sera za idara na taasisi hizo katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, nafasi ambazo zimetajwa katika Katiba hii au sheria zitakazotungwa na Bunge kwamba zitatajwa kwa uteuzi unaofanywa na Rais.
(3) Mamlaka ya kuwateua watu wengine wote wasiokuwa viongozi au watendaji wakuu kushika nafasi za madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, na mamlaka ya kuwapandisha vyeo watu hao, kuwaondoa katika madaraka, kuwafukuza kazi, kuwasimamisha kazi na mamlaka ya kudhibiti nidhamu ya watu waliokabidhiwa madaraka, yatakuwa mikononi mwa mamlaka husika za nidhamu na uteuzi kwa mujibu wa Katiba hii na Sheria.
(4) Masharti ya ibara ndogo ya (2) hayatamzuia Rais kuchukua hatua za kudhibiti nidhamu ya watumishi na utumishi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

Rais kuzingatia ushauri
83. Katika kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba na Sheria, Rais atakuwa huru katika utendaji wa kazi na shughuli zake na hatalazimika kufuata au kuzingatia ushauri atakaopewa na mtu yeyote au mamlaka yoyote isipokuwa pale tu anapotakiwa na Katiba hii au sheria nyingine yoyote kufanya jambo lolote kulingana na ushauri anaopewa na mtu au mamlaka yoyote.

Rais kushindwa kumudu majukumu yake
84.-(1) Endapo Baraza la Mawaziri litaridhika kuwa Rais hawezi kumudu kazi zake kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili linaweza kuwasilisha kwa Jaji Mkuu azimio la kumwomba Jaji Mkuu athibitishe kwamba Rais, kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili hawezi kumudu kazi zake.
(2) Baada ya kupokea azimio lililowasilishwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1), Jaji Mkuu atateua bodi ya utabibu ya watu wasiopungua watatu atakaowateua kutoka miongoni mwa madaktari bingwa wanaotambuliwa kisheria na bodi hiyo itachunguza suala hilo na kumshauri Jaji Mkuu ipasavyo.
(3) Jaji Mkuu anaweza, baada ya kutafakari ushauri na ushahidi wa kitabibu, kuwasilisha kwa Spika hati ya kuthibitisha kwamba, Rais kutokana na maradhi ya mwili au akili hamudu kazi zake, na iwapo Jaji Mkuu hatabatilisha hati hiyo ndani ya siku saba kutokana na Rais kupata nafuu na kurejea kazini, basi itahesabiwa kwamba nafasi ya madaraka ya Rais ipo wazi, na masharti yaliyomo katika Ibara ya 85(1)(d) yatatumika.

Utaratibu wa kujaza nafasi ya Rais kabla ya kumaliza muda wake
85.-(1) Endapo nafasi ya madaraka ya Rais itakuwa wazi kutokana na:
(a) Rais kufariki dunia;
(b) Rais kujiuzulu;
(c) Rais kupoteza sifa za uchaguzi katika nafasi ya madaraka ya Rais;
(d) Rais kutomudu kazi zake kutokana na maradhi;
(e) Rais kushtakiwa Bungeni na kuondolewa katika madaraka kwa mujibu wa Katiba hii,
basi Makamu wa Kwanza wa Rais ataapishwa na kushika nafasi ya madaraka ya Rais kwa muda uliobaki katika kipindi cha miaka mitano na kwa kuzingatia masharti yaliyoainishwa katika Ibara ya 92.
(2) Mara tu baada ya Rais kuapishwa na kushika madaraka kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1), na kwa vyovyote vile ndani ya kipindi kisichozidi siku kumi na nne tangu alipoapishwa:
(a) kwa Rais aliyepatikana kwa kupendekezwa na chama cha siasa, baada ya kushauriana na chama cha siasa anachotoka; au
(b) kwa Rais aliyepatikana kwa utaratibu wa mgombea huru, baada ya kushauriana na Tume Huru ya Uchaguzi,atapendekeza jina la mtu atakayekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na uteuzi huo utathibitishwa na Bunge kwa wingi wa kura za Wabunge wote.

Utekelezaji wa majukumu ya Rais akiwa hayupo
86.-(1) Ikitokea kwamba nafasi ya madaraka ya Rais ipo wazi kutokana na:
(a) masharti yaliyomo katika Ibara ya 84;
(b) masharti yaliyomo katika Ibara ya 97;
(c) kutokuwepo katika Jamhuri ya Muungano, kazi na shughuli za Rais zitatekelezwa na mmoja wa wafuatao, kwa kufuata orodha kama ilivyopangwa:
(i) Makamu wa Kwanza wa Rais au kama nafasi yake ipo wazi au kama naye hayupo au ni mgonjwa, basi;
(ii) Waziri Mkuu.
(2) Endapo mtu yeyote aliyetajwa katika ibara ndogo ya (1) atatekeleza kazi na shughuli za Rais kutokana na sababu kwamba mtu mwingine anayemtangulia katika orodha hiyo hayupo, basi mtu huyo ataacha kutekeleza kazi na shughuli hizo mara tu mtu huyo mwingine anayemtangulia katika orodha atakaporejea kazini.
(3) Mtu yeyote atakayekaimu nafasi ya madaraka ya Rais, kwa namna yoyote ile, hatakuwa na madaraka katika mambo yafuatayo:
(a) kuteua au kumuondoa madarakani kiongozi yeyote aliyeteuliwa na Rais kwa mujibu wa Katiba hii; au
(b) kufanya jambo jingine lolote lililokatazwa kama litakavyoainishwa na Rais katika hati ya kukasimu madaraka yake.
(4) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (2) na ya (3), Rais atakasimu madaraka yake kwa hati maalum aliyotia saini yake.
(c)Uchaguzi wa Rais

Uchaguzi wa Rais
87.-(1) Rais atachaguliwa na wananchi kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na kwa mujibu wa sheria.
(2) Uchaguzi wa Rais utafanyika kabla ya Rais kumaliza muda wake wa kuwa madarakani kwa mujibu wa Katiba hii.

Sifa za Rais
88.-(1) Mtu atakuwa na sifa ya kuchaguliwa kushika nafasi ya madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano ikiwa:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Katiba hii na sheria iliyotungwa na Bunge;
(b) ni mwenye akili timamu;
(c) wazazi wake wote wawili ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(d) wakati wa kugombea, ana umri usiopungua miaka arobaini;
(e) anayo shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa kwa mujibu wa sheria, au awe na ujuzi na uzoefu wa uongozi katika ngazi ya taifa utakaomwezesha kumudu madaraka ya Rais;
(f) ni mwanachama na mgombea aliyependekezwa na chama cha siasa au mgombea huru.
(2) Mtu hatakuwa na sifa za kugombea nafasi ya urais ikiwa mtu huyo:
(a) ana maslahi yoyote katika mkataba wa Serikali wa aina yoyote aliyowekewa miiko maalum kwa mujibu wa sheria, na iwapo amekiuka miiko hiyo;
(b) amewahi kuwa raia wa nchi nyingine; au
(c) amewahi kutiwa hatiani na chombo chenye mamlaka kwa kosa la kukwepa kulipa kodi na kosa lolote la jinai.

Utaratibu wa uchaguzi wa Rais
89.-(1) Katika uchaguzi wa Rais kila chama cha siasa kitakachotaka kushiriki katika uchaguzi wa Rais, kitawasilisha kwa Tume Huru ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano, kwa mujibu wa sheria, jina la mwanachama mmoja anayependekezwa kwa nafasi ya madaraka ya Rais.
(2) Endapo ni mgombea huru, kwa kuzingatia sifa zitakazoainishwa katika sheria itakayotungwa na Bunge atawasilisha jina lake kwenye Tume Huru ya Uchaguzi.
(3) Mapendekezo ya majina ya wagombea katika uchaguzi wa Rais yatawasilishwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi katika siku na kwa utaratibu utakaoainishwa katika sheria.
(4) Endapo itafika siku na saa iliyotajwa kwa ajili ya kuwasilisha mapendekezo ya majina ya wagombea, ni mgombea mmoja tu ambaye anapendekezwa kuwa halali, Tume Huru ya Uchaguzi itawasilisha jina lake kwa wananchi, nao watapiga kura ya kumkubali au kumkataa kwa mujibu wa masharti yaliyoainishwa katika Katiba hii na sheria.
(5) Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano utafanyika siku itakayoteuliwa na Tume Huru ya Uchaguzi kwa mujibu wa sheria.
(6) Mgombea wa nafasi ya madaraka ya Rais atatangazwa kuwa amechaguliwa kuwa Rais iwapo atapata kura zaidi ya asilimia hamsini ya kura zote halali zilizopigwa kwa nafasi ya madaraka ya Rais.
(7) Endapo katika uchaguzi wa Rais hakuna mgombea aliyekidhi masharti ya ibara ndogo ya (6), basi uchaguzi utarudiwa ndani ya siku sitini kwa wagombea walioshika nafasi ya kwanza na ya pili na mgombea atakayepata kura zaidi ya asilimia hamsini atatangazwa kuwa mshindi wa nafasi ya urais.
(8) Mambo mengine yote yahusuyo utaratibu wa uchaguzi wa Rais yatakuwa kama itakavyofafanuliwa katika sheria itakayotungwa na Bunge kwa ajili hiyo.

Malalamiko kuhusu uhalali wa uchaguzi wa Rais
90.-(1) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (2), endapo mtu yeyote aliyeshiriki kama mgombea katika nafasi ya madaraka ya Rais katika uchaguzi wa Rais hakuridhika na matokeo ya uchaguzi huo, anaweza kuwasilisha malalamiko katika Mahakama ya Juu kupinga matokeo ya uchaguzi wa Rais yaliyotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi.
(2) Malalamiko ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Rais yatawasilishwa Mahakama ya Juu ndani ya muda wa siku saba baada ya siku ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi wa Rais.
(3) Mahakama ya Juu itasikiliza na kutoa uamuzi wa shauri la kupinga matokeo ya uchaguzi wa Rais ndani ya siku kumi na nne tangu kupokea malalamiko yaliyowasilishwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (2) na uamuzi huo utakuwa wa mwisho.
(4) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (3), Mahakama ya Juu inaweza kutoa uamuzi wa kumthibitisha Rais bila kutoa sababu za uamuzi na sababu hizo zitatolewa ndani ya kipindi kisichozidi siku thelathini tangu siku ya kutoa uamuzi.
(5) Iwapo Mahakama ya Juu itaamua kuwa matokeo ya uchaguzi wa Rais si halali, uchaguzi wa Rais utarudiwa ndani ya siku sitini baada ya uamuzi kutolewa.

Kiapo cha Rais na muda wa kushika madaraka
91.-(1) Rais Mteule ataapishwa na Jaji Mkuu au Naibu Jaji Mkuu endapo Jaji Mkuu hayupo na atashika nafasi ya madaraka ya Rais siku saba baada ya kutangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi au mara baada ya kuthibitishwa na Mahakama ya Juu.
(2) Isipokuwa kama ataacha kushika nafasi ya madaraka ya Rais mapema zaidi, Rais atashika nafasi ya madaraka ya Rais kwa muda wa miaka mitano tangu siku alipoapishwa kuwa Rais.
(3) Rais atashika nafasi ya madaraka ya Rais hadi:
(a) siku ambapo Rais Mteule ataapa kushika nafasi ya madaraka ya Rais;
(b) siku ambapo atafariki dunia;
(c) siku atakapojiuzulu; au
(d) atakapoacha kushika nafasi ya madaraka ya Rais kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.

Haki ya kuchaguliwa tena
92.-(1) Mtu ambaye ni Rais anaweza kuchaguliwa tena kushika nafasi ya madaraka ya Rais kwa kipindi kingine cha miaka mitano.
(2) Mtu hatakuwa na sifa ya kugombea na kuchaguliwa zaidi ya vipindi viwili katika nafasi ya madaraka ya Rais.
(3) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, mtu aliyewahi kuwa Rais wa Zanzibar hatapoteza sifa za kugombea na kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano.
(4) Endapo Makamu wa Kwanza wa Rais atashika nafasi ya madaraka ya Rais kwa mujibu wa masharti ya Ibara ya 85 kwa kipindi cha chini ya miaka mitatu, ataruhusiwa kugombea nafasi ya Rais kwa vipindi viwili, lakini kama atashika nafasi ya madaraka ya Rais kwa muda wa miaka mitatu au zaidi ataruhusiwa kugombea nafasi ya madaraka ya Rais kwa kipindi kimoja tu.
(d) Masharti Mahsusi kuhusu Mamlaka ya Rais

Madaraka ya kutangaza vita
93.-(1) Kwa kuzingatia masharti ya Ibara hii, Rais atakuwa na mamlaka ya kutangaza kuwepo kwa vita kati ya Jamhuri ya Muungano na nchi nyingine au kundi lolote lile baada ya kupata idhini ya Bunge.
(2) Bila kujali masharti ya ibara ndogo ya (1), endapo Jamhuri ya Muungano itakuwa imevamiwa au kundi lolote limeanzisha vita ndani ya Jamhuri ya Muungano basi, Rais anaweza, baada ya kushauriana na Baraza la Usalama la Taifa, kutangaza kuwepo kwa vita katika Jamhuri ya Muungano.
(3) Baada ya kutoa tangazo kwa mujibu wa ibara ndogo ya (2), Rais atalitaarifu Bunge kwa kupeleka nakala ya tangazo hilo kwa Spika wa Bunge ambaye, ndani ya siku kumi na nne kuanzia tarehe ya tangazo, ataitisha Mkutano wa Bunge ili kulijulisha Bunge kuhusu tangazo lililotolewa na Rais.

Madaraka ya Rais kutangaza hali ya hatari
94.-(1) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii au sheria, Rais anaweza, baada ya kushauriana na Baraza la Usalama la Taifa, kutangaza hali ya hatari au hali ya kuzingirwa kwa eneo fulani la Jamhuri ya Muungano au katika sehemu yake yoyote.
(2) Rais anaweza tu kutangaza kuwa kuna hali ya hatari iwapo:
(a) Jamhuri ya Muungano iko katika vita;
(b) kuna hatari ya dhahiri kwamba Jamhuri ya Muungano inakaribia kuvamiwa na kuingia katika hali ya vita;
(c) kuna hali halisi ya kuvurugika kwa amani katika jamii au kutoweka kwa usalama wa jamii katika Jamhuri ya Muungano au sehemu yake yoyote kiasi kwamba ni lazima kuchukua hatua za pekee ili kurejesha amani na usalama;
(d) kuna hatari ya dhahiri na kubwa, kiasi kwamba amani katika jamii itavurugika na usalama wa raia kutoweka katika Jamhuri ya Muungano au sehemu yake yoyote ambayo haiwezi kuepukika isipokuwa kwa kutumia mamlaka ya pekee;
(e) kumetokea au kuna dalili ya kutokea janga ambalo linatishia jamii au sehemu ya jamii katika Jamhuri ya Muungano; au
(f) kuna aina nyingineyo ya hatari ambayo kwa dhahiri ni tishio kwa usalama wa nchi.
(3) Endapo inatangazwa kwamba kuna hali ya hatari katika Jamhuri ya Muungano au eneo lolote la Jamhuri ya Muungano, Rais atawasilisha nakala ya tangazo hilo kwa Spika wa Bunge ambaye, ndani ya siku zisizozidi kumi na nne tangu kutolewa kwa tangazo hilo, ataitisha mkutano wa Bunge ili kulijulisha juu ya taarifa ya hali ya hatari iliyotangazwa na Rais.
(4) Bunge linaweza kutunga sheria itakayoweka masharti kuhusu nyakati na taratibu ambazo zitawawezesha baadhi ya watu wenye kusimamia utekelezaji wa mamlaka ya Serikali katika sehemu mahsusi za Jamhuri ya Muungano kumuomba Rais kutumia madaraka aliyopewa na Ibara hii kuhusiana na yoyote kati ya sehemu hizo endapo katika sehemu hizo, kunatokea lolote kati ya hali zilizotajwa katika aya ya (c), (d) na (e) za ibara ndogo ya (2) na hali hiyo haivuki mipaka ya sehemu hizo, na pia, kwa ajili ya kufafanua utekelezaji wa mamlaka ya Serikali wakati wa hali ya hatari.
(5) Tangazo la hali ya hatari lililotolewa na Rais kwa mujibu wa Ibara hii litakoma kutumika iwapo litafutwa na Rais.
(6) Kwa madhumuni ya kuondoa mashaka juu ya ufafanuzi au utekelezaji wa masharti ya Ibara hii, masharti ya utangazaji wa hali ya hatari kama ilivyotajwa katika Ibara hii, yatatumika tu katika sehemu ya Jamhuri ya Muungano ambapo hali hiyo ya hatari imetangazwa.

Mamlaka ya Rais kutoa msamaha
95.-(1) Rais kwa mamlaka ya Mkuu wa Nchi, anaweza:
(a) kutoa msamaha kwa mtu yeyote aliyepatikana na hatia kwa kosa lolote mbele ya mahakama dhidi ya Jamhuri ya Muungano kwa masharti maalum kama yatakavyoainishwa katika sheria;
(b) kumwachilia kabisa au kwa muda maalum mtu yeyote aliyehukumiwa kuadhibiwa kwa ajili ya kosa lolote ili mtu huyo asitimize kabisa adhabu hiyo au asitimize adhabu hiyo wakati wa muda huo maalum;
(c) kubadilisha adhabu ya kifo kuwa adhabu ya kifungo cha maisha; au
(d) kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa ajili ya kosa lolote au kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu ya kutoza, au kuhodhi (au kuchukua) kitu cha mtu mwenye hatia ambacho vinginevyo kingechukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Masharti ya Ibara hii yatatumika kwa mtu aliyehukumiwa na kuadhibiwa akiwa Zanzibar na kwa adhabu zilizotolewa Zanzibar kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge inayotumika Zanzibar, hali kadhalika, masharti hayo yatatumika kwa mtu aliyehukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Bara kwa mujibu wa sheria.
(3) Kwa madhumuni ya Ibara hii, kutakuwa na Kamati ya Taifa ya Ushauri ambayo itakuwa na wajibu wa kumshauri Rais kuhusu kutoa msamaha kwa mtu yeyote aliyepatikana na hatia mahakamani na anatumikia adhabu.
(4) Utaratibu wa namna ya utekelezaji wa madaraka kwa mujibu wa Ibara hii, muundo, majukumu na utendaji kazi wa chombo kinachohusika na masuala ya msamaha wa wafungwa utaainishwa na sheria.

Kinga ya mashtaka dhidi ya Rais
96.-(1) Wakati Rais akiwa madarakani, hatashtakiwa wala mtu yeyote hataendesha mashtaka ya aina yoyote dhidi yake mahakamani kwa ajili ya kosa lolote la jinai.
(2) Wakati Rais ameshika madaraka kwa mujibu wa Katiba hii, haitaruhusiwa kufungua mahakamani shauri la madai kuhusu jambo lolote alilolitenda au alilokosa kulitenda yeye binafsi kama Rais ama kabla au baada ya kushika madaraka ya Rais, ila tu kama angalau siku thelathini kabla ya shauri kufunguliwa mahakamani, Rais atapewa au atatumiwa taarifa ya madai kwa maandishi kwa kufuata utaratibu utakaowekwa kwa mujibu wa sheria, na taarifa hiyo ikiwa inatoa maelezo kuhusu chanzo cha shauri hilo, kiini cha madai yenyewe, jina lake na anwani ya mahali anapoishi huyo mdai na jambo hasa analodai.
(3) Isipokuwa kama ataacha kushika madaraka ya Rais kutokana na kuondolewa madarakani na Bunge, haitakuwa halali kwa mtu kumshtaki au kufungua mahakamani shauri lolote la jinai au la madai dhidi ya mtu aliyekuwa anashika madaraka ya Rais baada ya kuacha madaraka hayo kutokana na jambo alilofanya wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya Rais.

Bunge kumshtaki Rais
97.-(1) Bunge linaweza kupitisha azimio la kumuondoa Rais madarakani endapo itatolewa hoja ya kumshtaki Rais na ikapitishwa kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii.
(2) Bila kuathiri masharti mengineyo ya Ibara hii, hoja yoyote ya kumshtaki Rais haitatolewa isipokuwa tu kama itadaiwa kwamba Rais ametenda mojawapo ya makosa yafuatayo:
(a) ukiukwaji mkubwa wa masharti ya Katiba hii;
(b) makosa makubwa ya jinai;
(c) kuzuia kwa namna yoyote ile yeye kuchunguzwa kwa mujibu wa Ibara hii;
(d) rushwa;
(e) amekuwa na mwenendo unaodhalilisha nafasi ya madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano;
(f) kupuuza au kukataa kutekeleza uamuzi au amri halali ya Mahakama; au
(g) amefanya kitendo ambacho kinakiuka kanuni za maadili au miiko ya uongozi.
(3) Bunge halitapitisha hoja ya kumshtaki Rais isipokuwa tu kama:
(a) hoja ya namna hiyo itatolewa baada ya miezi kumi na mbili tangu hoja kama hiyo ilipotolewa na ikakataliwa na Bunge; na
(b) taarifa ya maandishi, iliyotiwa saini na kuungwa mkono na Wabunge wasiopungua asilimia ishirini na tano ya Wabunge wote itawasilishwa kwa Spika siku kumi na nne kabla ya kikao ambapo hoja hiyo inakusudiwa kutolewa Bungeni.
(4) Taarifa itakayowasilishwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (3)(b) itafafanua makosa aliyoyatenda Rais, na itapendekeza kuwa Kamati Maalum ya Uchunguzi iundwe ili ichunguze tuhuma zilizotolewa dhidi ya Rais.
(5) Wakati wowote baada ya kupokea taarifa iliyotiwa saini na Wabunge na kujiridhisha kuwa masharti ya Katiba kwa ajili ya kuwasilisha hoja yametimizwa, Spika atamruhusu mtoa hoja kuiwasilisha mbele ya Bunge na kisha Spika atalitaka Bunge, bila ya kufanya majadiliano, lipige kura juu ya hoja ya kuunda Kamati Maalum ya Uchunguzi.
(6) Endapo hoja ya kuunda Kamati Maalum ya Uchunguzi itaungwa mkono na Wabunge wasiopungua asilimia sabini na tano ya Wabunge wote, Spika atatangaza majina ya wajumbe wa Kamati Maalum ya Uchunguzi.
(7) Kamati Maalum ya Uchunguzi, kwa madhumuni ya Ibara hii, itakuwa na wajumbe wafuatao:
(a) Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, ambaye atakuwa Mwenyekiti wa Kamati;
(b) Jaji Mkuu wa Zanzibar ambaye atakuwa Makamu Mwenyekiti; na
(c) Wabunge watano kutoka Bunge la Jamhuri ya Muungano, watakaoteuliwa na Spika kwa kuzingatia uwakilishi wa kila upande wa Muungano.
(8) Ndani ya siku saba baada ya Kamati Maalum ya Uchunguzi kuundwa, itachunguza na kuchambua mashtaka dhidi ya Rais, pamoja na kumpatia Rais fursa ya kujieleza, kwa kufuata utaratibu utakaowekwa na kanuni za kudumu za Bunge.
(9) Mapema iwezekanavyo, na kwa vyovyote vile katika muda usiozidi siku tisini, Kamati Maalum ya Uchunguzi itatoa taarifa yake kwa Spika.
(10) Baada ya Spika kupokea taarifa ya Kamati Maalum ya Uchunguzi, taarifa hiyo itawasilishwa Bungeni kwa kufuata utaratibu uliowekwa na kanuni za kudumu za Bunge.
(11) Baada ya taarifa ya Kamati Maalum ya Uchunguzi kuwasilishwa, Bunge litaijadili taarifa hiyo na kutoa fursa kwa Rais kujieleza, na kisha, kwa kura za Wabunge wasiopungua asilimia sabini na tano ya Wabunge wote, Bunge litapitisha azimio kuwa mashtaka dhidi ya Rais ama yamethibitika au hayakuthibitika.
(12) Endapo Bunge litapitisha azimio kuwa mashtaka dhidi ya Rais yamethibitika na kwamba hastahili kuendelea kushika madaraka ya Rais, Spika atamfahamisha Rais juu ya Azimio la Bunge na Rais atakuwa ameondolewa madarakani na Makamu wa Rais ataapishwa mara moja kushika madaraka ya Rais.
(13) Endapo Rais ataacha kushika madaraka ya Rais kutokana na mashtaka dhidi yake kuthibitika, hatakuwa na haki ya:
(a) kushika nafasi yoyote ya madaraka nchini; na
(b) kupata malipo yoyote ya uzeeni, posho wala kupata haki au nafuu nyingine anazopewa Rais au mtu aliyekuwa Rais kwa mujibu wa Katiba au sheria.
Maslahi ya Rais
98.-(1) Rais atalipwa mshahara na malipo mengine na atakapostaafu atapokea malipo ya uzeeni, kiinua mgongo au posho kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina.
(2) Mshahara na malipo mengine yote ya Rais hayatapunguzwa wakati Rais atakapokuwa ameshika madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(3) Bunge litatunga sheria kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya Ibara hii.
(e) Makamu wa Rais
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano
99. Kutakuwa na Makamu wa Rais watatu ambao watakuwa:
(a) Makamu wa Kwanza wa Rais;
(b) Rais wa Zanzibar ambaye atakuwa Makamu wa Pili wa Rais; na
(c) Waziri Mkuu ambaye atakuwa Makamu wa Tatu wa Rais.

Upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais
100.-(1) Mtu hatateuliwa kugombea au kushika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano isipokuwa tu kama anazo sifa za kuchaguliwa kuwa Rais.
(2) Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 88, Makamu wa Kwanza wa Rais atapatikana kwa kuchaguliwa katika uchaguzi pamoja na Rais, baada ya kupendekezwa na chama chake au mgombea huru wakati ule ule anapopendekezwa mgombea wa nafasi ya madaraka ya Rais na watapigiwa kura kwa pamoja.
(3) Chama cha siasa chochote au mtu yeyote anayekusudia kugombea nafasi ya madaraka ya Rais, akiwa mgombea huru, hatazuiwa kumpendekeza mtu yeyote kuwa mgombea nafasi ya madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa sababu tu kwamba mtu huyo kwa wakati huo ameshika nafasi ya madaraka ya Rais wa Zanzibar.
(4) Endapo mgombea wa madaraka ya Rais atachaguliwa basi na Makamu wa Kwanza wa Rais atakuwa amechaguliwa.
(5) Mtu atateuliwa kugombea nafasi ya Madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa kufuata kanuni kwamba endapo mgombea wa nafasi ya madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano atatoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano, basi Makamu wa Kwanza wa Rais atatoka upande wa pili wa Jamhuri ya Muungano.
(6) Katika utekelezaji wa madaraka yake, Makamu wa Kwanza wa Rais atatekeleza au atawezesha au kusimamia utekelezaji wa jambo lolote au mambo yoyote ambayo Rais ataagiza yatekelezwe.
Majukumu ya Makamu wa Kwanza wa Rais
101. Makamu wa Kwanza wa Rais atakuwa ni Msaidizi Mkuu wa Rais kuhusu mambo yote ya Jamhuri ya Muungano na:
(a) atafanya kazi zote atakazoagizwa na Rais;
(b) atafanya kazi za Rais kama Rais hayupo kazini au yupo nje ya nchi kwa kuzingatia masharti ya Ibara ya 86(3); na
(c) atakuwa Mwenyekiti wa Tume ya Usimamizi na Uratibu wa Mambo ya Muungano.
Muda wa Makamu wa Kwanza wa Rais kushika madaraka
102.-(1) Makamu wa Kwanza wa Rais atashika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais mara tu Rais anaposhika madaraka yake baada ya kuwa ameapishwa.
(2) Makamu wa Kwanza wa Rais atashika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais hadi:
(a) atakapofariki dunia akiwa katika madaraka;
(b) atakapojiuzulu;
(c) atakapoapishwa kuwa Rais baada ya nafasi ya madaraka ya Rais kuwa wazi;
(d) atakapoapishwa Rais mwingine kushika nafasi ya madaraka ya Rais pamoja na Makamu wake;
(e) atakaposhindwa kumudu majukumu yake kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili;
(f) atakapoondolewa madarakani baada ya kushtakiwa Bungeni kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii; au
(g) atakapoacha kushika madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais vinginevyo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.

Bunge kumshtaki Makamu wa Kwanza wa Rais
103.-(1) Bunge litakuwa na mamlaka ya kumshtaki na kumuondoa Makamu wa Kwanza wa Rais madarakani kwa utaratibu unaotumika kumshtaki Rais kwa mujibu wa Katiba hii, isipokuwa kwamba, hoja yoyote ya kumshtaki Makamu wa Kwanza wa Rais itatolewa tu iwapo:
(a) Rais amewasilisha hati kwa Spika inayoeleza kwamba Makamu wa Kwanza wa Rais ameacha au ameshindwa kutekeleza kazi za madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais;
(b) amekuwa na mwenendo unaodhalilisha madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania au nafasi ya madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais; au
(c) anadaiwa kutenda kosa lolote kati ya makosa yanayoweza kusababisha Rais kushtakiwa na Bunge kwa mujibu wa Katiba hii,
isipokuwa kwamba, haitatolewa hoja ya namna hiyo ndani ya miezi kumi na miwili tangu hoja kama hiyo ilipotolewa na ikakataliwa na Bunge.
(2) Masharti mengine kuhusu utaratibu wa kumshtaki Rais yatatumika wakati wa kumuondoa madarakani Makamu wa Kwanza wa Rais.
(3) Masharti mengine yote ya Ibara ya 96 yatatumika pia kwa Makamu wa Kwanza wa Rais isipokuwa tu kwamba Makamu wa Kwanza wa Rais aliyeondolewa madarakani chini ya ibara ndogo ya (1), hatakuwa na sifa tena za kushika nafasi ya Rais au Makamu wa Kwanza wa Rais.
(4) Endapo Makamu wa Kwanza wa Rais ataacha kushika madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais kutokana na mashtaka dhidi yake kuthibitika, hatakuwa na haki ya kupata malipo yoyote ya uzeeni, posho wala kupata haki au nafuu nyinginezo anazopewa Makamu wa Kwanza wa Rais au mtu aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais kwa mujibu wa Katiba hii au sheria.

Makamu wa Kwanza wa Rais kushindwa kumudu majukumu yake
104. Endapo Makamu wa Kwanza wa Rais hawezi kumudu kazi zake kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili, Rais anaweza, baada ya kushauriana na Baraza la Mawaziri, kuwasilisha kwa Jaji Mkuu azimio la kumwomba Jaji Mkuu athibitishe kwamba Makamu wa Kwanza wa Rais, kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili hawezi kumudu kazi zake na masharti mengine ya Ibara ya 84 yatatumika.

Upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais wakati nafasi hiyo inapokuwa wazi
105. Endapo nafasi ya Madaraka ya Makamu wa Kwanza wa Rais iko wazi kutokana na masharti yaliyomo katika Ibara ya 102 na 103, basi mapema iwezekanavyo na kwa vyovyote vile ndani ya siku zisizozidi kumi na nne tokea kifo au baada ya kuachia madaraka, Rais atamteua mtu atakayekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na uteuzi huo utathibitishwa na Bunge kwa wingi wa kura za Wabunge wote.

Kiapo cha Makamu wa Kwanza wa Rais
106. Makamu wa Kwanza wa Rais, kabla ya kushika madaraka yake ataapishwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano au Naibu Jaji Mkuu endapo Jaji Mkuu hayupo, kiapo cha uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa Sheria.

Makamu wa Pili wa Rais
107.-(1) Makamu wa Pili wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ambaye ni Rais wa Zanzibar, pamoja na majukumu mengine yaliyoainishwa katika Katiba ya Zanzibar, ataanza kushika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Pili wa Rais mara baada ya kuapishwa na Rais.
(2) Mtu atakuwa na sifa ya kuwa Makamu wa Pili wa Rais iwapo tu atakuwa ni Rais wa Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar.
(3) Endapo nafasi ya Makamu wa Pili wa Rais iko wazi kutokana na sababu yoyote ile, nafasi hiyo itajazwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Zanzibar.

Makamu wa Tatu wa Rais
108.-(1) Makamu wa Tatu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ambaye ni Waziri Mkuu, pamoja na majukumu mengine yaliyoainishwa katika Katiba hii, atashika madaraka baada ya kuapishwa na Rais.
(2) Mtu atakuwa na sifa ya kuwa Makamu wa Tatu wa Rais iwapo tu atakuwa ni Waziri Mkuu kwa mujibu wa Katiba hii.
(3) Endapo nafasi ya Makamu wa Tatu wa Rais iko wazi kutokana na masharti ya Katiba hii, nafasi hiyo itajazwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.

Maslahi ya Makamu wa Rais
109.-(1) Makamu wa Rais atalipwa mshahara na malipo mengine, na atakapostaafu atapokea malipo ya uzeeni, kiinua mgongo au posho kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina.
(2) Mshahara na malipo mengine yote ya Makamu wa Rais hayatapunguzwa wakati atakapokuwa ameshika madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(3) Bunge litatunga sheria kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya Ibara hii.

SEHEMU YA PILI
WAZIRI MKUU NA BARAZA LA MAWAZIRI LA SERIKALI YA
JAMHURI YA MUUNGANO

(a) Waziri Mkuu
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano
110.-(1) Kutakuwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano atakayeteuliwa na Rais kwa kufuata masharti ya Ibara hii na ambaye kabla ya kushika madaraka yake, ataapa mbele ya Rais kwa kiapo kinachohusika na nafasi ya madaraka ya Waziri Mkuu.
(2) Mapema iwezekanavyo na kwa vyovyote vile ndani ya siku kumi na nne, baada ya kushika madaraka yake, Rais atamteua Mbunge wa kuchaguliwa kutoka katika jimbo la uchaguzi anayetokana na chama cha siasa chenye Wabunge wengi zaidi Bungeni, au kama hakuna chama cha siasa chenye Wabunge wengi zaidi, anayeelekea kuungwa mkono na Wabunge walio wengi kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, naye hatashika madaraka hayo mpaka kwanza uteuzi wake uwe umethibitishwa na Bunge kwa azimio litakaloungwa mkono na kura za Wabunge walio wengi.
(3) Bila kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, Waziri Mkuu atashika nafasi ya madaraka ya Waziri Mkuu hadi:
(a) siku ambapo Rais mteule ataapa kushika nafasi ya madaraka yake;
(b) siku ambapo atafariki dunia akiwa katika madaraka;
(c) siku atakapojiuzulu;
(d) siku Rais atakapomteua Mbunge mwingine kuwa Waziri Mkuu; au
(e) atakapoacha kushika nafasi ya madaraka ya Waziri Mkuu kwa mujibu wa masharti mengineyo ya Katiba hii.

Kazi na Mamlaka ya Waziri Mkuu
111.-(1) Waziri Mkuu atakuwa na madaraka juu ya udhibiti, usimamizi na utekelezaji wa siku hadi siku wa kazi na shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Waziri Mkuu atakuwa Kiongozi wa shughuli za Serikali Bungeni.
(3) Katika utekelezaji wa madaraka yake, Waziri Mkuu atatekeleza, atawezesha au atasimamia utekelezaji wa jambo lolote au mambo yoyote ambayo Rais ataagiza kwamba yatekelezwe.

Uwajibikaji wa Serikali
112.-(1) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, Waziri Mkuu atawajibika kwa Rais kuhusu utekelezaji wa madaraka yake.
(2) Serikali ya Jamhuri ya Muungano chini ya mamlaka ya Rais, ndio itakuwa na uwezo wa kufanya maamuzi juu ya sera kwa ujumla, na Mawaziri, chini ya uongozi wa Waziri Mkuu, watawajibika kwa pamoja Bungeni kuhusu utekelezaji wa shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
Kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu
113.-(1) Bila ya kujali masharti ya Ibara ya 110, Bunge linaweza kupitisha azimio la kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu endapo itatolewa hoja kupendekeza hivyo na ikapitishwa kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii.
(2) Bila kuathiri masharti mengineyo ya Ibara hii, hoja yoyote ya kutaka kupitisha kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu haitatolewa Bungeni endapo:
(a) haina uhusiano na utekelezaji wa majukumu ya Waziri Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 111, au hakuna madai kwamba Waziri Mkuu amevunja sheria inayohusu maadili ya viongozi wa umma;
(b) haijapita miezi sita tangu alipoteuliwa; au
(c) haijapita miezi tisa tangu hoja ya namna hiyo ilipotolewa Bungeni na Bunge likakataa kuipitisha.
(3) Hoja ya kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu haitapitishwa na Bunge isipokuwa tu kama:
(a) taarifa ya maandishi iliyotiwa saini na kuungwa mkono na Wabunge wasiopungua asilimia ishirini na tano ya Wabunge wote itatolewa kwa Spika, siku angalau kumi na nne kabla ya siku inapokusudiwa kuwasilishwa Bungeni; na
(b) Spika atajiridhisha kuwa masharti ya Katiba kwa ajili ya kuleta hoja yametimizwa.
(4) Hoja ya kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu itapitishwa tu iwapo inaungwa mkono na zaidi ya asilimia hamsini ya Wabunge wote.
(5) Endapo hoja ya kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu itaungwa mkono na Wabunge walio wengi, Spika atawasilisha azimio hilo kwa Rais, na mapema iwezekanavyo, na kwa vyovyote vile ndani ya siku mbili tangu Bunge lililopitisha azimio la hoja ya kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Waziri Mkuu atatakiwa kujiuzulu, na Rais atamteua Mbunge mwingine kuwa Waziri Mkuu.

(b) Baraza la Mawaziri
Baraza la Mawaziri
114.-(1) Kutakuwa na Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano ambalo litakuwa na wajumbe wafuatao:
(a) Rais;
(b) Makamu wa Kwanza wa Rais;
(c) Rais wa Zanzibar ambaye ni Makamu wa Pili wa Rais;
(d) Waziri Mkuu ambaye ni Makamu wa Tatu wa Rais; na
(e) Mawaziri wote wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Rais ataongoza mikutano ya Baraza la Mawaziri, na endapo Rais hayupo, mikutano itaongozwa na Makamu wa Kwanza wa Rais na kama wote wawili hawapo, Waziri Mkuu ataongoza Mikutano hiyo.
(3) Mwanasheria Mkuu wa Serikali atahudhuria vikao vya Baraza la Mawaziri na atakuwa na haki zote za mjumbe wa vikao hivyo, isipokuwa hatakuwa na haki ya kupiga kura.

Uteuzi wa Mawaziri na Naibu Mawaziri
115.-(1) Kutakuwa na Mawaziri na Naibu Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano watakaoteuliwa na Rais kwa kushauriana na Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mkuu.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), idadi ya Mawaziri na Naibu Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano haitazidi arobaini.
(3) Majukumu ya Waziri yatakuwa kama yatakavyoainishwa na Rais kwenye Hati ya Uteuzi.
(4) Naibu Mawaziri watakuwa wasaidizi wa Mawaziri katika utekelezaji wa majukumu yao na hawatakuwa wajumbe wa Baraza la Mawaziri.
(5) Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na Wizara kwa kuzingatia mamlaka ya Serikali kwa mujibu wa Katiba hii.

Sifa za Waziri na Naibu Waziri
116.-(1) Mtu atateuliwa kuwa Waziri au Naibu Waziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ikiwa:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) ana shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambulika kwa mujibu wa sheria au ana elimu inayolingana;
(c) ana weledi au uzoefu; na
(d) ni mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano.
(2) Mtu aliyewahi kutiwa hatiani kwa makosa ya ubadhirifu wa mali za umma au utovu wa uaminifu, ama katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, hatakuwa na sifa ya kuteuliwa kuwa Waziri au Naibu Waziri katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
Kiapo, muda na
117.-(1) Waziri au Naibu Waziri hatashika nafasi ya madaraka hadi awe ameapa mbele ya Rais kiapo cha uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa na sheria.
(2) Muda wa kushika nafasi ya madaraka ya Waziri au Naibu Waziri utaanza tarehe ambayo Waziri au Naibu Waziri anayehusika ataapishwa.
(3) Waziri au Naibu Waziri atashika nafasi ya madaraka kwa muda wote isipokuwa kama:
(a) atajiuzulu au kufariki;
(b) Rais atatengua uteuzi wake;
(c) Rais mteule ameapishwa kushika madaraka ya Rais; au
(d) iwapo mtu huyo ataacha kuwa mbunge kwa mujibu wa Katiba hii.
(c) Mwanasheria Mkuu wa Serikali

Mwanasheria Mkuu wa Serikali
118.-(1) Kutakuwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambaye katika Katiba hii ataitwa kwa kifupi kama “Mwanasheria Mkuu” ambaye atateuliwa na Rais.
(2) Mtu ataweza kuteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ikiwa atakuwa na sifa zifuatazo:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) ana shahada ya sheria ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa kwa mujibu wa sheria za nchi;
(c) ni mweledi na mwenye sifa ya uwakili wa Mahakama Kuu ya Zanzibar au Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano;
(d) ni mtumishi mwandamizi katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano;
(e) ni mtu ambaye amedumu na sifa hizo kwa muda usiopungua miaka kumi na tano; na
(f) ni mwadilifu katika utekelezaji wa majukumu yake.
(3) Mwanasheria Mkuu atakuwa ndiye mshauri mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhusu mambo ya sheria na, kwa ajili hiyo, atawajibika kutoa ushauri kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhusu mambo yote ya kisheria, na kutekeleza shughuli nyinginezo zozote zenye asili ya au kuhusiana na sheria zitakazopelekwa kwake au atakazoagizwa na Rais kuzitekeleza, pia kutekeleza kazi au shughuli nyinginezo zilizokabidhiwa kwake na Katiba hii au na sheria yoyote.
(4) Mwanasheria Mkuu atakuwa Mbunge kutokana na wadhifa wake na atashika madaraka yake mpaka:
(a) uteuzi wake utakapofutwa na Rais; au
(b) mara tu kabla ya Rais mteule kushika madaraka ya Rais, na atalipwa mshahara, posho na malipo mengine kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge.
(5) Katika kutekeleza kazi na shughuli zake kwa mujibu wa Ibara hii, Mwanasheria Mkuu atakuwa na haki ya kuhudhuria na kusikilizwa katika Mahakama zote za Jamhuri ya Muungano.
(6) Mwanasheria Mkuu hatashika nafasi ya madaraka ya Mwanasheria Mkuu hadi awe ameapa mbele ya Rais kiapo cha utii na uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusu utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria.
(7) Mwanasheria Mkuu, isipokuwa kama ataacha kushika nafasi ya madaraka yake mapema zaidi, ataendelea kushika madaraka hadi Rais atakapomteua Mwanasheria Mkuu mwingine.

Naibu Mwanasheria Mkuu
119.-(1) Kutakuwa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali atakayeteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa zilizoainishwa katika ibara ndogo ya (2) ya Ibara ya 118.
(2) Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali atafanya kazi nyingine kama atakavyoelekezwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali na atakuwa ni afisa masuuli wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
(3) Bila ya kujali masharti ya Ibara hii, mtu anayestahili kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali atakuwa ni mtu ambaye amedumu katika sifa zilizoainishwa katika Ibara ya 118(2) kwa muda usiopungua miaka kumi.

(d) Mkurugenzi wa Mashtaka
Mkurugenzi wa Mashtaka
120-(1) Kutakuwa na Mkurugenzi wa Mashtaka ambaye atateuliwa na Rais, kutoka miongoni mwa watumishi wa umma wenye sifa ya kufanya kazi ya uwakili au mtu mwenye sifa ya kusajiliwa kuwa wakili na amekua na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka kumi.
(2) Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa na uwezo wa:
(a) kufungua na kuendesha mashtaka ya jinai dhidi ya mtu yeyote katika Mahakama yoyote isipokuwa Mahakama ya kijeshi kwa kosa analotuhumiwa kutenda;
(b) kuchukua na kuendesha mashtaka ya jinai yaliyoanzishwa na mtu au mamlaka yoyote; na
(c) kusitisha katika hatua yoyote kabla ya hukumu kutolewa mashtaka ya jinai yaliyoanzishwa au yanayoendeshwa na Mkurugenzi wa Mashtaka, mtu au mamlaka yoyote.
(3) Mkurugenzi wa Mashtaka anaweza kuondoka madarakani kutokana na:
(a) kifo;
(b) kujiuzulu;
(c) kushindwa kutekeleza majukumu yake kutokana na maradhi ya mwili au akili; au
(d) kuondolewa kazini kutokana na mwenendo na utendaji mbaya wa kazi.
(4) Bunge litatunga sheria itakayofafanua:
(a) masharti na utaratibu wa utekelezaji wa mamlaka ya Mkurugenzi wa Mashtaka chini ya Katiba hii;
(b) masharti na utaratibu wa kumuondoa madarakani Mkurugenzi wa Mashtaka; na
(c) mambo mengine yanayomhusu Mkurugenzi wa Mashtaka.

(e) Katibu Mkuu Kiongozi
Katibu Mkuu Kiongozi
121.-(1) Kutakuwa na Katibu Mkuu Kiongozi atakayeteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa Maafisa Waandamizi walio katika nafasi ya uteuzi katika utumishi wa umma.
(2) Katibu Mkuu Kiongozi atakuwa Katibu wa Baraza la Mawaziri, Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu, Katibu wa Baraza la Usalama la Taifa na Mkuu wa Utumishi wa Umma.
(3) Katika wadhifa wake wa Katibu wa Baraza la Mawaziri, Katibu Mkuu Kiongozi atakuwa Mtendaji Mkuu katika Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri, na atatekeleza shughuli zifuatazo kwa kufuata maagizo ya jumla au maalum atakayopewa na Rais, ikiwa ni pamoja na:
(a) kuandaa ratiba ya mikutano na kutayarisha orodha ya shughuli za Baraza la Mawaziri;
(b) kuandika na kuweka kumbukumbu za mikutano;
(c) kutoa taarifa na maelezo ya uamuzi wa Baraza la Mawaziri kwa kila mtu au chombo cha umma kinachohusika na uamuzi uliotolewa; na
(d) kutekeleza kazi na shughuli nyingine zozote ambazo Rais ameagiza.
(4) Akiwa Mkuu wa Utumishi wa Umma, Katibu Mkuu Kiongozi atakuwa na mamlaka ya kutoa maelekezo ya mara kwa mara kuhusiana na masuala ya utumishi wa umma.
(5) Katika nafasi ya madaraka ya Katibu wa Baraza la Usalama la Taifa, Katibu Mkuu Kiongozi atakuwa Mkuu na Mratibu wa Sekretarieti ya Baraza la Usalama la Taifa.
(6) Katibu Mkuu Kiongozi hatashika madaraka yake hadi awe ameapa mbele ya Rais, kiapo cha utii na uaminifu au kiapo kingine chochote kinachohusu utendaji wa kazi zake kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria.
(7) Kwa madhumuni ya Ibara hii, maneno “Afisa Mwandamizi aliye katika nafasi ya uteuzi” maana yake ni mtu anayeshika nafasi ya Katibu Mkuu au mwenye sifa ya kuwa Katibu Mkuu au cheo kingine kinachofanana na hicho.
(f) Utekelezaji wa shughuli za Baraza la Mawaziri

Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri
122.-(1) Kutakuwa na Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri ambayo itakuwa na jukumu la kuhudumia Baraza la Mawaziri na kutekeleza majukumu mengine kama itakavyopangiwa na Katibu wa Baraza la Mawaziri.
(2) Bunge linaweza kutunga sheria kuhusu utaratibu na utekelezaji wa shughuli za Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri.

(g) Wakuu wa Mikoa
Wakuu wa Mikoa
123.-(1) Kutakuwa na Mkuu wa Mkoa kwa kila mkoa katika Jamhuri ya Muungano ambaye, bila kuathiri ibara ndogo ya (3), atakuwa ni kiongozi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Wakuu wa Mikoa katika Tanzania Bara watateuliwa na Rais baada ya kushauriana na Waziri Mkuu.
(3) Wakuu wa Mikoa katika Zanzibar watateuliwa na Rais wa Zanzibar.
(4) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (5), kila Mkuu wa Mkoa, atakuwa na wajibu wa kusimamia utekelezaji wa kazi na shughuli zote za Serikali ya Jamhuri ya Muungano katika Mkoa aliokabidhiwa; na kwa ajili hiyo, atatekeleza kazi na shughuli zote zilizotajwa na sheria, au kwa mujibu wa sheria kama ni kazi au shughuli za Mkuu wa Mkoa na atakuwa na madaraka yote yatakayotajwa na Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge.
(5) Pamoja na wajibu na madaraka yake yaliyotajwa kwenye masharti yaliyotangulia ya Ibara hii, Mkuu wa Mkoa yeyote wa Zanzibar atatekeleza kazi na shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar atakazokabidhiwa na Rais wa Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya 1984 au sheria yoyote iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi.

SEHEMU YA TATU
MADARAKA YA UMMA
Serikali za Mitaa
124.-(1) Kutakuwa na Serikali za Mitaa katika kila mkoa, manispaa, wilaya, mji na kijiji katika Jamhuri ya Muungano ambazo zitakuwa za aina na majina yatakayowekwa na sheria itakayotungwa na Bunge au Baraza la Wawakilishi.
(2) Madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa ni kugatua madaraka kwa wananchi ili kuwapa haki na mamlaka ya kushiriki katika mipango na shughuli za utekelezaji wa maendeleo katika sehemu zao na nchini kote kwa ujumla.
(3) Bunge au Baraza la Wawakilishi, kwa kadri itakavyokuwa, litatunga Sheria, pamoja na mambo mengine itakayoweka miundo ya mabaraza na wajumbe wake, taratibu za uchaguzi, mamlaka, majukumu na vyanzo vya mapato vya Serikali za Mitaa.

Mamlaka ya Serikali za Mitaa
125. Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, Serikali za Mitaa, kwa kuzingatia masharti ya sheria za nchi zitakuwa na mamlaka ya kutekeleza shughuli zifuatazo:
(a) kuhakikisha ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao katika maeneo yao;
(b) kutoa huduma bora kwa wananchi wa eneo husika;
(c) kuwashirikisha wananchi katika kupanga, kuamua na kutekeleza mipango yao ya maendeleo; na
(d) kuimarisha na kutumia demokrasia kwa ajili ya kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Uongozi katika Serikali za Mitaa
126. Uongozi katika Serikali za Mitaa utakuwa na uwakilishi wa wananchi, na viongozi wa Serikali za Mitaa watapatikana kupitia mchakato wa uchaguzi au uteuzi kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge au Baraza la Wawakilishi.

SURA YA TISA
UHUSIANO NA URATIBU WA MAMBO YA MUUNGANO
Tume ya Usimamizi na Uratibu wa Mambo ya Muungano
127.-(1) Kutakuwa na Tume ya Usimamizi na Uratibu wa Mambo ya Muungano ambayo itajulikana kwa kifupi kama “Tume ya Mambo ya Muungano”.
(2) Tume ya Mambo ya Muungano itakuwa na wajumbe wafuatao:
(a) Makamu wa Kwanza wa Rais ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b) Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano;
(c) Kiongozi wa shughuli za Serikali katika Baraza la Wawakilishi; na
(d) Mawaziri wenye dhamana ya masuala ya Muungano.
(3) Mwenyekiti wa Tume ya Mambo ya Muungano anaweza kumwalika mtu yeyote atakayeona anafaa kwa ajili ya kufafanua jambo kwenye Tume kabla ya kufikia uamuzi.

Majukumu ya Tume ya Mambo ya Muungano
128.-(1) Tume ya Mambo ya Muungano itakuwa na jukumu maalum la kuwezesha uratibu na ushirikiano katika kutekeleza masharti ya Katiba hii, sera, sheria, mipango na mikakati baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na pia itakuwa chombo maalum kwa ajili ya:
(a) kuweka utaratibu bora na endelevu wa kushauriana na kushirikiana baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;
(b) kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya kuratibu na kusimamia, utekelezaji wa Mambo ya Muungano kwa manufaa ya ustawi wa wananchi wote;
(c) kupendekeza na kusimamia utaratibu utakaowezesha uwakilishi wa pande zote mbili za Muungano katika maeneo na masuala mbalimbali kwa nia ya kukuza umoja na mshikamano katika utekelezaji wa Mambo ya Muungano;
(d) kukuza na kuwezesha uratibu na ushirikiano baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika Mambo yasiyo ya Muungano kwa lengo la kuwezesha kufanana kwa kiwango cha utoaji huduma kwa wananchi wote;
(e) kuratibu masuala yenye maslahi kwa Taifa;
(f) kusimamia uwakilishi wa pande zote mbili za Muungano katika masuala ya ajira katika utumishi wa Jamhuri ya Muungano; na
(g) kusuluhisha na kutatua migogoro baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1)(g), endapo upande wowote haukuridhishwa na uamuzi uliotolewa na Tume, unaweza kupeleka shauri katika Mahakama ya Juu ambayo uamuzi wake utakuwa wa mwisho.
(3) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1)(f), Tume ya Mambo ya Muungano itaweka utaratibu utakaowezesha uteuzi wa viongozi na watumishi katika taasisi au wizara za Muungano kufanyika kwa kuzingatia uwakilishi wa pande zote mbili za Muungano.
(4) Bunge litatunga sheria itakayoainisha:
(a) utaratibu wa utekelezaji wa majukumu ya Tume;
(b) uanzishwaji, muundo na majukumu ya Sekretarieti ya Tume ya Mambo ya Muungano;
(c) utaratibu wa kusuluhisha na kutatua migogoro baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar; na
(d) mambo mengine yote yanayohusu Tume ya Mambo ya Muungano.

SURA YA KUMI
BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO
SEHEMU YA KWANZA

MUUNDO NA MADARAKA YA BUNGE
Bunge
129.-(1) Kutakuwa na Bunge ambalo litakuwa na sehemu mbili, yaani Rais na Wabunge.
(2) Kutakuwa na aina zifuatazo za Wabunge:
(a) wabunge wa kuchaguliwa kupitia majimbo ya uchaguzi yatakayotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi;
(b) wabunge watano wenye ulemavu watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa za kuchaguliwa kuwa wabunge;
(c) wabunge wasiozidi kumi watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa za kuwa wabunge;
(d) Spika iwapo hatakuwa amechaguliwa kutoka miongoni mwa Wabunge; na
(e) Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
(3) Wabunge waliotajwa katika ibara ndogo ya (2)(a) watapatikana kwa kupigiwa kura na wananchi kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na sheria itakayotungwa na Bunge.
(4) Bila kuathiri masharti ya Ibara hii, msingi wa uwakilishi katika ibara ndogo ya (2)(a), utazingatia uwakilishi ulio sawa kati ya wabunge wanawake na wanaume.
(5) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (2), idadi ya wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano waliochaguliwa au kuteuliwa haitapungua mia tatu na arobaini na haitazidi mia tatu na tisini.
(6) Bunge litatunga sheria itakayoainisha utaratibu wa utekelezaji wa masharti ya Ibara hii.
Muda wa Bunge
130.-(1) Bila kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, maisha ya kila Bunge yatakuwa ni muda wa miaka isiyozidi mitano.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), maneno “maisha ya Bunge” maana yake ni muda wote unaoanzia tarehe ambapo Bunge Jipya litaitishwa ili kukutana kwa mara ya kwanza baada ya uchaguzi wa wabunge na kuishia tarehe ya uchaguzi mwingine wa wabunge.
Madaraka ya Bunge
131.-(1) Rais kama sehemu ya Bunge atatekeleza mamlaka yote aliyokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba hii.
(2) Sehemu ya Pili ya Bunge ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano chenye madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii.
(3) Katika kutekeleza majukumu yake, Bunge litakuwa na madaraka yafuatayo:
(a) kutunga sheria pale ambapo utekelezaji unahitaji kutungiwa sheria;
(b) kujadili na kutoa ushauri katika mambo yote yenye maslahi kwa Taifa na umma wa Watanzania;
(c) kumuuliza Waziri yeyote suala lolote kuhusu mambo ya umma katika Jamhuri ya Muungano ambayo yako katika wajibu wake;
(d) kujadili mgawanyo na kuidhinisha matumizi ya fedha kwa Wizara, taasisi na mashirika ya Serikali;
(e) kujadili utekelezaji wa majukumu ya kila Wizara wakati wa Mkutano wa Bunge wa kila mwaka wa bajeti;
(f) kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu, muda wa kati au muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali katika Jamhuri ya Muungano;
(g) kujadili na kuridhia mikataba ya kimataifa inayohusu Jamhuri ya Muungano na ambayo kwa masharti yake inahitaji kuridhiwa; na
(h) kuthibitisha mapendekezo ya uteuzi wa viongozi kwa mujibu wa Katiba hii na Sheria.

Mipaka ya Bunge katika kutumia madaraka yake
132.-(1) Katika kutekeleza madaraka ya kuisimamia Serikali kwa mujibu wa Katiba hii, wajibu wa Bunge utakuwa ni kuishauri Serikali na endapo Bunge halitaridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Serikali katika utekelezaji wa suala lililotolewa ushauri, basi Bunge litakuwa na haki ya kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa madaraka lililopewa katika Katiba hii.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), Bunge halitachukua hatua yoyote ya kiutendaji ambayo, kwa desturi ni shughuli za Serikali, na halitatoa maagizo yoyote ya kiutendaji kwa Serikali na watumishi wa umma:
Isipokuwa kwamba, Bunge litashauri kuhusu suala lolote lililo katika dhamana ya Waziri anayehusika.

Madaraka ya kutunga Sheria
133.-(1) Mamlaka yote ya kutunga sheria juu ya Mambo ya Muungano na mambo mengine yote yahusuyo Tanzania Bara, yatakuwa mikononi mwa Bunge.
(2) Mamlaka yoyote ya kutunga sheria katika Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo ya Muungano yatakuwa mikononi mwa Baraza la Wawakilishi.
(3) Endapo sheria yoyote iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi inahusu jambo lolote katika Zanzibar ambalo liko chini ya mamlaka ya Bunge, sheria hiyo itakuwa batili na itatenguka na pia endapo sheria yoyote iliyotungwa na Bunge inahusu jambo lolote ambalo liko chini ya mamlaka ya Baraza la Wawakilishi, sheria hiyo itakuwa batili na itatenguka.
(4) Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kuhusu jambo lolote haitatumika Zanzibar isipokuwa kwa mujibu wa masharti yafuatayo:
(a) sheria hiyo iwe imetamka wazi kwamba itatumika Tanzania Bara na
vilevile Zanzibar au iwe inabadilisha, kurekebisha au kufuta sheria inayotumika Zanzibar;
(b) sheria hiyo iwe inabadilisha au kurekebisha au kufuta sheria iliyokuwa inatumika tangu zamani Tanzania Bara ambayo ilikuwa inatumika pia Zanzibar kwa mujibu wa Mapatano ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ya mwaka 1964, au kwa mujibu wa sheria yoyote ambayo ilitamka wazi kwamba itatumika Tanzania Bara na vilevile Zanzibar; na
(c) sheria hiyo iwe inahusu Mambo ya Muungano, na kila inapotajwa Tanzania katika Sheria yoyote ifahamike kuwa sheria hiyo itatumika katika Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa ufafanuzi uliotolewa na masharti ya Ibara hii.
(5) Bila kuathiri kutumika kwa Katiba ya Zanzibar kwa mujibu wa Katiba hii kuhusu mambo yote ya Zanzibar yasiyo Mambo ya Muungano, Katiba hii itakuwa na nguvu ya sheria katika Jamhuri nzima ya Muungano na endapo sheria nyingine yoyote itakiuka masharti yaliyomo katika Katiba hii, Katiba ndiyo itakuwa na nguvu, na sheria hiyo nyingine, kwa kiasi inachokiuka Katiba, itakuwa batili.

Utaratibu wa kubadilisha Katiba
134.-(1) Bunge linaweza kutunga sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii kwa kufuata kanuni zifuatazo:
(a) Muswada wa sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti ya Katiba hii au masharti yoyote ya sheria yanayohusu jambo lolote isipokuwa mambo yanayohusu aya ya (b) au (c), utapitishwa kwa kuungwa mkono kwa wingi wa kura za Wabunge wote;
(b) Muswada wa sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii au masharti yoyote ya sheria yoyote yanayohusika na jambo lolote kati ya mambo yaliyotajwa katika Nyongeza ya Pili, utapitishwa tu iwapo utaungwa mkono kwa kura za wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote wa Tanzania Bara na theluthi mbili ya Wabunge wote wa Zanzibar;
(c) Muswada wa sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote yanayohusika na jambo lolote kati ya mambo yaliyotajwa katika Nyongeza ya Tatu iliyoko mwishoni mwa Katiba hii, utapitishwa tu iwapo utaungwa mkono kwa zaidi ya nusu ya kura halali zilizopigwa na wananchi wa Tanzania Bara, na zaidi ya nusu ya kura halali zilizopigwa na wananchi wa Tanzania Zanzibar katika kura ya maoni itakayoendeshwa na kusimamiwa na Tume Huru ya Uchaguzi kwa mujibu wa sheria.
(2) Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya ibara ndogo ya (1) kubadilisha masharti ya Katiba hii maana yake ni pamoja na kurekebisha au kusahihisha masharti haya au kufuta na kuweka masharti mengine badala yake au kusisitiza au kubadilisha matumizi ya masharti hayo.

Utaratibu wa kutunga sheria
135.-(1) Bunge litatumia madaraka yake ya kutunga sheria kwa kujadili na kupitisha muswada wa sheria.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (3), muswada wa sheria unaweza kuandikwa na Serikali, Kamati ya Bunge, kikundi cha Wabunge au Mbunge.
(3) Wakati wa kuandaa muswada wa sheria, Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Kamati ya Bunge, Kikundi cha Wabunge au Mbunge atahakikisha kwamba anawashirikisha wananchi kwa ajili ya kupata maoni na mapendekezo juu ya muswada huo.
(4) Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 134, muswada utahesabiwa kuwa umepitishwa na Bunge iwapo utaungwa mkono kwa wingi wa kura za Wabunge wote.
(5) Bunge litatunga kanuni za kudumu zitakazoweka utaratibu wa:
(a) kuwasilisha, kujadili na kupitisha muswada wa sheria; na
(b) utekelezaji bora wa masharti ya ibara ndogo ya (3).
Utaratibu wa kutunga sheria kuhusu mambo ya fedha
136.-(1) Bunge halitashughulikia jambo lolote kati ya mambo yanayohusika na Ibara hii isipokuwa kama Rais amependekeza kwamba jambo hilo lishughulikiwe na Bunge na pendekezo hilo la Rais liwe limewasilishwa kwenye Bunge na Waziri.
(2) Mambo yanayohusika na Ibara hii ni yafuatayo:
(a) muswada wa sheria kwa ajili ya jambo lolote kati ya mambo yafuatayo:
(i) kutoza kodi au kubadilisha kodi kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza;
(ii) kuagiza kwamba malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko Mkuu wa Hazina au mfuko mwingine wowote wa Serikali au kubadilisha kiwango hicho na namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza;
(b) kuagiza kwamba malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko Mkuu wa Hazina au mfuko mwingine wowote wa Serikali wakati ikifahamika kwamba fedha iliyomo katika mifuko hiyo haikupangiwa itolewe kwa ajili ya malipo au matumizi hayo, au kuagiza kwamba malipo au matumizi yanayofanywa kutokana na mifuko hiyo yaongezwe;
(c) kufuta au kusamehe deni lolote linalotakiwa lilipwe kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano; au
(d) hoja au mabadiliko yoyote ya hoja kwa ajili ya lolote kati ya mambo yaliyoelezwa katika aya ya (a).

Madaraka ya Rais kuhusu muswada wa sheria
137.-(1) Bila kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Katiba hii, Bunge litatumia madaraka yake ya kutunga sheria kwa kufuata utaratibu wa kujadili na kupitisha miswada ya sheria, na muswada hautakuwa sheria mpaka uwe umepitishwa na Bunge na kukubaliwa na Rais kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii.
(2) Muswada wa sheria uliowasilishwa kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali utawekewa saini na Rais ndani ya siku zisizozidi thelathini kutoka siku ambayo muswada huo uliwasilishwa na kupokelewa na Katibu wa Baraza la Mawaziri.
(3) Baada ya muswada wa sheria kuwasilishwa kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali chake, Rais anaweza kukubali au kukataa muswada huo, na iwapo Rais atakataa kuukubali Muswada huo basi ataurudisha Bungeni pamoja na maelezo ya sababu za kukataa Muswada huo.
(4) Baada ya muswada wa sheria kurudishwa Bungeni na Rais kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii, muswada huo hautapelekwa tena kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali chake kabla ya kumalizika muda wa miezi sita tangu uliporudishwa Bungeni.
(5) Endapo katika kujadiliwa tena Bungeni kabla haujapelekwa tena kwa Rais, muswada uliorudishwa Bungeni na Rais umeungwa mkono na Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote, basi muswada huo unaweza kuwasilishwa mapema zaidi kwa Rais.
(6) Iwapo muswada uliorudishwa Bungeni na Rais na katika kuujadili ukaungwa mkono na Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote na kupelekwa tena kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali chake, basi Rais atatakiwa kuukubali muswada husika kabla ya kumalizika muda wa miezi sita na endapo miezi sita itafika tangu muswada huo ulipopelekwa tena kwa Rais pasipo Rais kuukubali, basi Rais atatakiwa kuukubali muswada huo la sivyo itabidi alivunje Bunge.

Kupitishwa kwa Bajeti ya Serikali
138.-(1) Endapo Bunge halitaridhishwa na hoja kuhusu Bajeti ya Serikali, Bunge linaweza kurudisha hoja hiyo pamoja na mapendekezo mahsusi kuhusiana na upungufu uliobainika.
(2) Serikali inawajibika kuyafanyia kazi mapendekezo ya Bunge kwa kadri itakavyowezekana na kuiwasilisha tena hoja hiyo Bungeni pamoja na maelezo ya utekelezaji wa mapendekezo ya Bunge na endapo Bunge litaikataa kwa mara ya pili basi Rais atalivunja Bunge na kuitisha Uchaguzi Mkuu.

SEHEMU YA PILI
WABUNGE
Uchaguzi wa Wabunge
139.-(1) Kila baada ya Bunge kumaliza muda wa maisha yake, kutakuwa na uchaguzi wa Wabunge katika majimbo ya uchaguzi kama itakavyotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi utakaofanyika kwa mujibu wa sheria.
(2) Kutakuwa na uchaguzi wa mbunge katika Jimbo la Uchaguzi ikiwa kiti cha Mbunge aliyechaguliwa kuwakilisha jimbo la uchaguzi kitakuwa wazi kwa sababu nyingine yoyote isiyohusika na Bunge kumaliza muda wake.
(3) Endapo tarehe ya Bunge kumaliza muda wake imetangazwa au inafahamika, hakutakuwa na uchaguzi mdogo wa Mbunge kwa mujibu wa ibara ndogo ya (2) ndani ya kipindi cha miezi kumi na miwili kabla ya tarehe hiyo.

Sifa za kuchaguliwa kuwa Mbunge
140.-(1) Bila kuathiri masharti yaliyomo katika Ibara hii, mtu yeyote atakuwa na sifa za kuchaguliwa au kuteuliwa kuwa mbunge endapo:
(a) ni raia wa Jamhuri ya Muungano aliyetimiza umri wa miaka ishirini na moja wakati wa kugombea;
(b) anajua kusoma na kuandika lugha ya Kiswahili au Kingereza; na
(c) ni mwanachama aliyependekezwa na chama cha siasa au mgombea huru.
(2) Mtu hatakuwa na sifa za kugombea au kuchaguliwa kuwa mbunge ikiwa:
(a) imethibitishwa rasmi na Bodi ya Utabibu kwamba ana ugonjwa wa akili;
(b) mtu huyo amehukumiwa na mahakama yoyote katika Jamhuri ya Muungano na kupewa adhabu ya kifo au ya kifungo gerezani kwa muda unaozidi miezi sita kwa kosa lolote linalohusu kukwepa kulipa kodi.
(c) Katika kipindi cha miaka mitano kabla ya tarehe ya uchaguzi amepata kuhukumiwa na kupewa adhabu ya kifungo kwa kosa linaloambatana na kukosa uaminifu au kwa kuvunja sheria inayohusiana na maadili ya uongozi.
(3) Bunge linaweza kutunga sheria itakayoweka masharti yatakayomzuia mtu asichaguliwe kuwa mbunge wa kuwakilisha jimbo la uchaguzi ikiwa mtu huyo ni mwenye madaraka yanayohusika na shughuli za kuongoza au kusimamia uchaguzi wa wabunge au shughuli za uandikishaji wa wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa wabunge.
(4) Kwa madhumuni ya kutoa fursa ya kukata rufani kwa mtu yeyote:
(a) aliyethibitishwa rasmi kisheria kuwa ana ugonjwa wa akili;
(b) aliyehukumiwa na kupewa adhabu ya kifo au kifungo; au
(c) aliyepatikana na hatia ya kosa lolote lililotajwa katika sheria kwa mujibu wa ibara ndogo ya (2),
mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa sheria kwa ajili ya kuweka masharti kwamba hukumu inayopingwa haitakuwa na nguvu kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya ibara ndogo ya (2) hadi upite muda uliotajwa katika sheria hiyo.

Utaratibu wa uchaguzi wa wabunge
141.-(1) Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi, watachaguliwa na wananchi kwa kufuata masharti ya Katiba hii na sheria kwa mujibu wa Katiba hii, inayoweka masharti kuhusu uchaguzi wa Wabunge.
(2) Wagombea uchaguzi katika majimbo ya Uchaguzi, watatakiwa kuwasilisha majina yao kwa Tume Huru ya Uchaguzi kwa mujibu wa utaratibu utakaowekwa na sheria.
Kiapo na masharti ya kazi ya Ubunge
142.-(1) Kila Mbunge ataapishwa kiapo cha uaminifu na Spika katika Bunge kabla hajaanza kushiriki katika shughuli za Bunge, lakini Mbunge anaweza kushiriki katika uchaguzi wa Spika hata kabla hajaapishwa.
(2) Mbunge atashika madaraka kwa mujibu wa Katiba hii, na atalipwa mshahara, posho na malipo mengine kwa mujibu wa sheria.

Kupoteza sifa za Ubunge
143.-(1) Mbunge atakoma kuwa Mbunge ikiwa litatokea lolote kati ya mambo yafuatayo:
(a) tukio lolote ambalo, kama asingekuwa Mbunge lingemfanya asiwe au apoteze sifa za kuchaguliwa au kuteuliwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii;
(b) atakosa kuhudhuria Mkutano mmoja wa Bunge bila ya ruhusa ya Spika;
(c) itathibitishwa kwamba amevunja masharti ya sheria inayohusu maadili ya viongozi wa umma;
(d) atashindwa kufanya kazi za Mbunge kwa muda wa miezi sita mfululizo kutokana na kizuizi ndani ya gereza;
(e) atashindwa kutoa tamko rasmi kuhusu sifa za kuwa Mbunge au taarifa rasmi kuhusu mali kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii katika muda uliowekwa mahsusi na sheria;
(f) atajiuzulu ubunge;
(g) kwa ridhaa yake atajiondoa au kujivua uanachama wa chama chake cha siasa, atafukuzwa au kuvuliwa uanachama na chama chake cha siasa;
(h) Mbunge aliyetokana na mgombea huru, atajiunga na chama chochote cha siasa;
(i) ataondolewa madarakani kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii; au
(j) kufariki dunia.
(2) Mbunge anaweza kufungua shauri mahakamani kupinga uamuzi wa kuthibitishwa kwake kuwa ana ugonjwa wa akili au kupinga kufukuzwa au kuvuliwa uanachama wake wa chama cha siasa au kupatikana na hatia kwa kosa la aina iliyotajwa katika ibara ndogo ya (1).
Uamuzi wa suala kama mtu ni Mbunge
144.-(1) Kila shauri kwa ajili ya kupata uamuzi kama:
(a) uchaguzi wa Mbunge ulikuwa halali au sivyo; au
(b) Mbunge amekoma kuwa Mbunge na nafasi ya madaraka ya Ubunge iko wazi au hapana,
litafunguliwa na kusikilizwa kwanza katika Mahakama Kuu.
(2) Bunge linaweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti kuhusu mambo yafuatayo:
(a) watu wanaoweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu kwa ajili ya kupata uamuzi juu ya suala lolote kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii;
(b) sababu na nyakati za kufungua shauri la namna hiyo, utaratibu wa kufungua shauri na masharti yanayotakiwa yatimizwe kwa kila shauri kama hilo; na
(c) kutaja mamlaka ya Mahakama Kuu juu ya shauri kama hilo.
Tamko rasmi la Mbunge kuhusu mali na madeni
145.-(1) Kila Mbunge kabla ya kumalizika siku thelathini tangu aapishwe kushika nafasi ya madaraka ya Mbunge sharti awasilishe kwa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma nakala mbili za tamko rasmi kuhusu mali na madeni kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(2) Tamko rasmi lililotajwa katika ibara ndogo ya (1), litatolewa katika fomu maalum itakayoandaliwa kwa mujibu wa sheria.

SEHEMU YA TATU
UONGOZI WA BUNGE
Spika na mamlaka yake
146.-(1) Kutakuwa na Spika wa Bunge ambaye atachaguliwa na Wabunge kutoka miongoni mwa watu ambao ni Wabunge au wenye sifa za kuwa Wabunge na atakuwa ndiye Kiongozi wa Bunge na atawakilisha Bunge katika vyombo na vikao vingine vyote nje ya Bunge.
(2) Waziri, Naibu Waziri au mtu mwenye madaraka ya aina nyingine yoyote yatakayotajwa na sheria kwa madhumuni ya Ibara hii, hataweza kuchaguliwa kuwa Spika.
(3) Mtu yeyote atakayechaguliwa kuwa Spika atatakiwa, kabla ya kumaliza siku kumi na tano tangu kuchaguliwa kwake, kuwasilisha kwa Rais tamko rasmi kwamba hajapoteza sifa za uchaguzi kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na Tamko hilo litatolewa kwa kutumia fomu maalum itakayowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

Ukomo wa Spika
147.-(1) Spika atakoma kushika nafasi ya madaraka ya Spika iwapo:
(a) kutatokea jambo lolote ambalo, kama asingekuwa Spika, lingemfanya mtu huyo asiwe na sifa za uchaguzi au apoteze sifa za uchaguzi wa Spika;
(b) ataondolewa kwenye madaraka ya Spika kwa Azimio la Bunge lililoungwa mkono na Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote;
(c) atashindwa kuwasilisha tamko rasmi kuhusiana na mali na madeni yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii;
(d) atapatikana na hatia kwa kosa la kutoa habari za uongo, kwa kiapo kinyume cha sheria kuhusu tamko rasmi lolote lililotolewa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii;
(e) atashindwa kuwasilisha tamko la mali na madeni kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii kabla ya kumalizika muda uliowekwa kwa ajili hiyo;
(f) itathibitika kuwa amevunja masharti ya sheria inayohusu maadili ya uongozi wa umma;
(g) atajiuzulu; au
(h) atafariki dunia.
(2) Hakuna shughuli yoyote itakayotekelezwa katika Bunge wakati wowote ambao nafasi ya madaraka ya Spika itakuwa wazi, isipokuwa shughuli ya kumchagua Spika.

Naibu Spika
148.-(1) Kutakuwa na Naibu Spika wa Bunge ambaye atachaguliwa na Wabunge kutoka miongoni mwao.
(2) Waziri, Naibu Waziri au mtu mwenye madaraka ya aina nyingine yoyote yatakayotajwa na sheria kwa madhumuni ya Ibara hii, hataweza kuchaguliwa kuwa Naibu Spika.
(3) Wabunge watamchagua Naibu Spika nyakati zifuatazo:
(a) Bunge litakapokutana kwa mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu au mapema iwezekanavyo baada ya wakati huo; na
(b) katika kikao cha kwanza cha Bunge baada ya nafasi ya madaraka ya Naibu Spika, kuwa wazi kwa sababu yoyote isiyohusika na Bunge kuvunjwa au mapema iwezekanavyo baada ya kikao hicho.
(4) Naibu Spika atakoma kushika nafasi ya madaraka ya Naibu Spika litokeapo lolote kati ya mambo yaliyoainishwa katika Ibara ya 147(1).

Sifa za mtu kuchaguliwa kuwa Spika au Naibu Spika
149. Mtu atastahili kuchaguliwa kuwa Spika au Naibu Spika endapo wakati wa kugombea, atakuwa mwenye umri usiopungua miaka arobaini na usiozidi miaka sabini.
Utaratibu wa uchaguzi na kiapo cha Spika na Naibu Spika
150.-(1) Kutakuwa na uchaguzi wa Spika katika kikao cha kwanza cha Mkutano wa Kwanza wa Bunge Jipya, na katika kikao cha kwanza chochote mara baada ya kutokea nafasi ya madaraka ya Spika kuwa wazi.
(2) Kutakuwa na uchaguzi wa Naibu Spika wakati wowote katika Mkutano wa Kwanza wa Bunge Jipya na vile vile katika kikao cha kwanza cha Bunge kitakachofuata mara baada ya kutokea nafasi ya madaraka ya Naibu Spika kuwa wazi.
(3) Uchaguzi wa Spika na Naibu Spika, utafanywa kwa kura ya siri, na utaendeshwa kwa kufuata utaratibu utakaowekwa na kanuni za Bunge.
(4) Spika na Naibu Spika watachaguliwa kwa misingi kwamba, endapo Spika atatoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano, Naibu Spika atatoka upande wa pili wa Jamhuri ya Muungano.
(5) Isipokuwa kama ataacha madaraka yake, Spika na Naibu Spika watakaa madarakani kwa vipindi visivyozidi viwili vya miaka mitano.
(6) Mtu yeyote atakayechaguliwa kuwa Spika au Naibu Spika atatakiwa, kabla ya kuanza kutekeleza madaraka yake, kuapa kiapo cha uaminifu.

Katibu wa Bunge
151.-(1) Kutakuwa na Katibu wa Bunge ambaye atateuliwa na Rais.
(2) Katibu wa Bunge atakuwa ndiye Mtendaji Mkuu wa Ofisi ya Bunge na atawajibika kwa utendaji bora wa shughuli za Bunge kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii na sheria.
Sekretarieti ya Bunge
152.-(1) Kutakuwa na Sekretarieti ya Bunge itakayokuwa na watumishi kutoka pande zote za Jamhuri ya Muungano kwa kuzingatia sifa za kitaaluma na ngazi za utumishi kwa mujibu wa mahitaji ya shughuli za Bunge kama itakavyoamuliwa na Tume ya Utumishi wa Bunge.
(2) Sekretarieti ya Bunge chini ya uongozi wa Katibu wa Bunge, itatekeleza kazi na shughuli zote zilizowekwa au zitakazokuwa ni muhimu kwa ajili ya kuhakikisha utekelezaji bora wa shughuli za Bunge, Wabunge na madaraka ya Bunge.

SEHEMU YA NNE
UTARATIBU WA SHUGHULI ZA BUNGE
Kanuni za kudumu za Bunge
153. Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, Bunge litatunga kanuni za kudumu kwa ajili ya kuweka utaratibu wa kutekeleza shughuli zake.

Rais kulihutubia Bunge
154.-(1) Rais atalihutubia Bunge Jipya katika Mkutano wa Kwanza na kulifungua rasmi.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), Rais anaweza wakati wowote kulihutubia Bunge au kupeleka kwenye Bunge taarifa ambayo itasomwa na Waziri Mkuu.

Mikutano ya Bunge
155.-(1) Bunge litafanya mikutano yake mahali ambapo ni desturi kufanya Mikutano hiyo au mahali pengine popote katika Jamhuri ya Muungano patakapotajwa na Spika kwa ajili hiyo.
(2) Mkutano wa Kwanza wa Bunge Jipya katika maisha ya Bunge utaitishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano na utaanza siku ile ambayo Bunge limeagizwa kukutana, na kila Mkutano unaofuata utaanza siku yoyote itakayopangwa na Bunge au siku yoyote itakayopangwa kwa mujibu wa kanuni za Bunge.
(3) Rais anaweza kuitisha Mkutano wa Bunge wakati wowote kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
Uongozi wa kikao cha Bunge
156. Kila kikao cha Bunge kitaongozwa na mmoja wapo wa watu wafuatao:
(a) Spika;
(b) ikiwa Spika hayupo, Naibu Spika; au
(c) ikiwa Spika na Naibu Spika wote hawapo, Mbunge yeyote aliyechaguliwa na Bunge kwa ajili hiyo.
Akidi ya kikao cha Bunge
157.-(1) Akidi ya kila kikao cha Bunge ni nusu ya Wabunge wote, isipokuwa kama imeelezwa vinginevyo katika Katiba hii.
(2) Kila suala litakalowasilishwa kwa ajili ya kupata uamuzi wa Bunge litaamuliwa kwa kufuata wingi wa kura za Wabunge waliohudhuria na kupiga kura, isipokuwa kwa masuala yaliyowekewa masharti mahsusi chini ya Katiba hii.

Kamati za Bunge
158.-(1) Bunge linaweza kuunda Kamati za Bunge za aina mbalimbali kadri litakavyoona inafaa kwa ajili ya utekelezaji bora wa madaraka yake.
(2) Kanuni za Bunge zinaweza kufafanua muundo na shughuli za Kamati za Bunge zitakazoundwa kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii.

SEHEMU YA TANO
MADARAKA NA HAKI ZA BUNGE
Uhuru wa majadiliano Bungeni
159.-(1) Kutakuwa na uhuru wa mawazo, majadiliano na utaratibu katika Bunge na uhuru huo hautavunjwa wala kuhojiwa na chombo chochote katika Jamhuri ya Muungano, au katika Mahakama au mahali penginepo nje ya Bunge.
(2) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii au masharti ya sheria nyingine yoyote inayohusika, Mbunge yeyote hatashitakiwa au kufunguliwa shauri lolote la madai mahakamani kutokana na jambo lolote alilolisema au kulifanya ndani ya Bunge au alilolileta Bungeni kwa njia ya maombi, muswada, hoja au vinginevyo.
(3) Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti ya kuwezesha mahakama na sheria kuhifadhi na kutilia nguvu uhuru wa mawazo, majadiliano na utaratibu wa shughuli katika Bunge ambao kwa mujibu wa Ibara hii umedhaminiwa na Katiba hii.

SEHEMU YA SITA
TUME YA UTUMISHI WA BUNGE NA MFUKO WA BUNGE
(a) Tume ya Utumishi wa Bunge
Tume ya Utumishi wa Bunge
160.-(1) Kutakuwa na Tume ya Utumishi wa Bunge ambayo itakuwa na Wajumbe wafuatao:
(a) Spika wa Bunge ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b) Naibu Spika wa Bunge ambaye atakuwa Makamu mwenyekiti;
(c) Waziri mwenye dhamana ya Bunge;
(d) Wabunge watano wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, kwa kuzingatia uwakilishi wa pande mbili za Muungano; na
(e) Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni.
(2) Katibu wa Bunge atakuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Bunge.
(3) Tume inaweza kumualika mtu mwingine yeyote mwenye utaalam mahsusi kushiriki kikao chochote cha Tume, isipokuwa mtu huyo hatakuwa na haki ya kupiga kura.
(4) Bunge linaweza kutunga sheria ambayo pamoja na mambo mengine itaeleza namna ya kuwapata wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Bunge na majukumu ya Tume hiyo.
Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Bunge
161.-(1) Tume ya Utumishi wa Bunge itakuwa na wajibu wa kuendeleza, kuwezesha na kuhakikisha utekelezaji wa kazi na shughuli za Bunge, kwa ufanisi na uwazi.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Tume ya Utumishi wa Bunge.

(b) Mfuko wa Bunge
Mfuko wa Bunge
162.-(1) Kutakuwa na Mfuko wa Bunge la Jamhuri ya Muungano ambao utakuwa chini ya usimamizi wa Katibu wa Bunge.
(2) Mfuko wa Bunge utatumika kwa ajili ya kugharamia shughuli za uendeshaji, pamoja na shughuli nyingine muhimu katika utekelezaji wa majukumu ya Bunge.
(3) Serikali itahakikisha kwamba, katika kila bajeti ya mwaka wa fedha wa Serikali, inatenga kwa kiwango kinachotosha kadri hali itakavyoruhusu, fedha ambazo zitaingizwa katika Mfuko wa Bunge.
(4) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu uendeshaji wa Mfuko wa Bunge.

SURA YA KUMI NA MOJA
SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR, BARAZA LA MAPINDUZI LA ZANZIBAR NA BARAZA LA WAWAKILISHI LA ZANZIBAR

SEHEMU YA KWANZA
(a) Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na mamlaka yake
163.-(1) Kutakuwa na Serikali ya Zanzibar itakayojulikana kama “Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar” ambayo itakuwa na mamlaka katika Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo ya Muungano kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(2) Bila kuathiri masharti yaliyomo katika ibara hii na katika ibara zifuatazo katika Sura hii, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaundwa na kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na Katiba ya Zanzibar ya 1984.

(b) Rais wa Zanzibar
Rais wa Zanzibar na mamlaka yake
164.-(1) Kutakuwa na Rais wa Zanzibar ambaye atakuwa Kiongozi Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi la Zanzibar atakayechaguliwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya 1984.
(2) Rais wa Zanzibar kabla ya kushika madaraka yake ataapa mbele ya Jaji Mkuu wa Zanzibar kiapo cha kuilinda na kuitetea Katiba ya Jamhuri ya Muungano, na kiapo kingine chochote kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar kinachohusika na utendaji wa kazi yake, kisha atashika na kutekeleza madaraka hayo kwa mujibu wa Katiba hii na Katiba ya Zanzibar ya 1984.
(c) Baraza la Mapinduzi la Zanzibar
Baraza la Mapinduzi la Zanzibar na kazi zake
165.-(1) Kutakuwa na Baraza la Mapinduzi la Zanzibar litakalokuwa na wajumbe wa aina na idadi itakayowekwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Zanzibar ya 1984.
(2) Bila kuathiri madaraka ya Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kama Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Baraza la Mapinduzi litakuwa ndicho chombo kikuu cha kumsaidia na kumshauri Rais wa Zanzibar katika masuala ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuratibu utekelezaji wa shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na pia utekelezaji wa madaraka yake juu ya shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu mambo yote yasiyo Mambo ya Muungano, kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na yale ya Katiba ya Zanzibar ya 1984.

SEHEMU YA PILI
BARAZA LA WAWAKILISHI LA ZANZIBAR
Baraza la Wawakilishi la Zanzibar
166.-(1) Kutakuwa na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kama litakavyoundwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya 1984.
(2) Madaraka yote ya kutunga sheria katika Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo Mambo ya Muungano yatakuwa mikononi mwa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

SURA YA KUMI NA MBILI
MAHAKAMA YA JAMHURI YA MUUNGANO

SEHEMU YA KWANZA
MISINGI YA UTOAJI HAKI NA UHURU WA MAHAKAMA
Kuanzishwa kwa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano
167.-(1) Kutakuwa na Mahakama ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Mahakama ya Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Katiba hii na sheria nyingine yoyote, itatekeleza mamlaka yake kupitia Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani.
(3) Mahakama ya Jamhuri ya Muungano itakuwa ni chombo chenye mamlaka ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano.
Misingi ya utoaji haki
168. Katika kutoa uamuzi wa mashauri ya madai na jinai kwa kuzingatia sheria, Mahakama ya Jamhuri ya Muungano itafuata kanuni zifuatazo:
(a) kutenda haki kwa wote bila ubaguzi wowote;
(b) kutochelewesha haki bila sababu ya msingi;
(c) kutoa fidia ipasayo kwa watu wanaoathirika kutokana na makosa ya watu wengine, na kwa mujibu wa sheria zilizotungwa mahsusi kwa ajili hiyo;
(d) kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro; na
(e) kutenda haki bila kufungwa na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka.
Uhuru wa Mahakama
169.-(1) Katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, Mahakama zote zitaongozwa na masharti ya Katiba hii na hazitaingiliwa ama kwa kudhibitiwa, kushinikizwa au kupewa maelekezo na mtu au chombo chochote.
(2) Nafasi ya madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano haitafutwa wakati wowote ule ikiwa kuna mtu ambaye kwa wakati huo anashikilia nafasi hiyo.
(3) Mishahara na malipo mengine ya Majaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano yatalipwa kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina.
(4) Mshahara na malipo mengine yanayolipwa kwa Jaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano hayatabadilishwa kwa maana ya kumuondolea faida Jaji husika.
(5) Malipo ya mafao ya kustaafu ya Jaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani au Mahakamu Kuu ya Jamhuri ya Muungano hayatabadilishwa kwa maana ya kumuondolea faida Jaji husika wakati wote wa uhai wake.
(6) Jaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani, Mahakamu Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar hatashtakiwa kwa jambo lolote alilolifanya au kutolifanya kwa nia njema katika utekelezaji wa shughuli ya utoaji haki kwa mujibu wa Katiba hii na sheria.

SEHEMU YA PILI
MUUNDO WA MAHAKAMA
(a) Mahakama ya Jamhuri ya Muungano
Muundo wa Mahakama
170.-(1) Bila kuathiri masharti yoyote yaliyotangulia katika sehemu hii, kutakuwa na Muundo wa Mahakama katika Jamhuri ya Muungano utakaokuwa kama ifuatavyo:
(a) Mahakama ya Juu;
(b) Mahakama ya Rufani; na
(c) Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii au sheria nyingine yoyoye iliyotungwa na Bunge, iwapo sheria yoyote iliyotungwa na Bunge inayotumika Tanzania Bara na vile vile Zanzibar imekabidhi madaraka yoyote kwa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano, basi Mahakama Kuu ya Zanzibar yaweza kutekeleza madaraka hayo kwa kiasi kile kile inavyoweza kutekeleza Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano.
(b) Mahakama ya Juu ya Jamhuri ya Muungano
Mahakama ya Juu
171. Kutakuwa na Mahakama ya Juu ya Jamhuri ya Muungano au kwa kifupi kama “Mahakama ya Juu” na ambayo itakuwa na:
(a) Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano ambaye atakuwa Rais wa Mahakama ya Juu;
(b) Naibu Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano ambaye atakuwa Makamu wa Rais wa Mahakama ya Juu; na
(c) Majaji wengine wa Mahakama ya Juu wasiopungua saba.
Akidi ya kikao cha
172.-(1) Akidi ya kikao cha Mahakama ya Juu itakuwa ni Majaji wa Mahakama ya Juu

Mahakama ya Juu watano.
(2) Kila shauri na rufani inayohitaji uamuzi wa Mahakama ya Juu itaamuliwa kwa kufuata kauli ya walio wengi kati ya Majaji wa Mahakama ya Juu waliosikiliza shauri hilo.
Mamlaka ya Mahakama ya Juu
173.-(1) Mahakama ya Juu itakuwa ni ngazi ya mwisho ya rufani katika Jamhuri ya Muungano na itakuwa na madaraka ya:
(a) pekee na ya awali ya:
(i) kusikiliza na kuamua mashauri yanayohusu matokeo ya uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano;
(ii) kusikiliza na kuamua mashauri yatakayowasilishwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu tafsiri au utekelezaji wa Katiba hii; na
(iii) kusuluhisha mashauri yatakayowasilishwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu utekelezaji wa Katiba hii;
(b) kusikiliza na kuamua rufani kutoka Mahakama ya Rufani;
(c) kutoa ushauri kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, pale itakapohitajika; na
(d) kusikiliza na kuamua shauri lolote litakalowasilishwa mbele yake kwa mujibu wa Katiba hii au sheria nyingine yoyote itakayoipa Mahakama hiyo mamlaka.
(2) Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano na Mahakama Kuu ya Zanzibar, zitalazimika kufuata maamuzi ya Mahakama ya Juu.
(3) Bila kujali masharti ya ibara ndogo ya (2), Mahakama ya Juu haitafungwa na uamuzi wake wa awali.
(4) Bunge litatunga sheria itakayoweka utaratibu zaidi kuhusu uendeshaji wa Mahakama ya Juu.
(5) Mahakama ya Juu itaandaa kanuni kwa ajili ya utekelezaji wa mamlaka yake.
Madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu
174.-(1) Jaji wa Mahakama ya Juu atakuwa na madaraka ya kusikiliza na kuamua shauri lolote katika Mahakama ya Juu.
(2) Bila kujali masharti ya ibara ndogo ya (1), iwapo Jaji wa Mahakama ya Juu, kabla ya kuteuliwa kwake alikuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar, Jaji huyo anaweza kuendelea kufanya kazi zake katika Mahakama aliyotoka hadi amalize kutayarisha na kutoa hukumu au hadi akamilishe shughuli nyingine yoyote inayuhusika na mashauri ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla hajateuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Juu.
(3) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (2), itakuwa ni halali kwa Jaji wa Mahakama ya Juu kutoa hukumu au uamuzi mwingine wowote unaohusika kwa kutumia na kutaja nafasi ya madaraka aliyokuwa akishika kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Juu na endapo hukumu hiyo au uamuzi huo utapingwa kwa njia ya rufani itakayofikishwa mbele ya Mahakama ya Juu, Jaji huyo hatakuwa na madaraka ya kusikiliza rufani hiyo.
(c) Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Juu

Uteuzi wa Jaji Mkuu
175.-(1) Jaji Mkuu atateuliwa na Rais kutoka orodha ya majina ya watu watatu yaliyopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(2) Jaji Mkuu ndiye atakuwa Mkuu wa Mhimili wa Mahakama katika Jamhuri ya Muungano.
(3) Mtu ataweza kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu endapo atakuwa amefikisha umri wa miaka arobaini na tano au zaidi na mwenye sifa ya uadilifu na uaminifu katika utekelezaji wa majukumu yake na awe:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) na shahada ya sheria kutoka chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na mamlaka inayoshughulikia elimu ya juu katika Jamhuri ya Muungano; na
(i) amefanya kazi ya ujaji katika Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar; au
(ii) amefanya kazi ya utumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano au ana utaalamu akiwa na sifa ya kusajiliwa kuwa wakili na amekuwa na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka ishirini.

Uteuzi wa Naibu Jaji Mkuu
176.-(1) Naibu Jaji Mkuu atateuliwa na Rais kutoka orodha ya majina ya watu watatu yaliyopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(2) Mtu atateuliwa kuwa Naibu Jaji Mkuu endapo atakuwa na sifa zilizoainishwa katika Ibara ya 175.
(3) Naibu Jaji Mkuu atakuwa ndiye Msaidizi Mkuu wa Jaji Mkuu katika utekelezaji wa majukumu yake.

Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Juu
177.-(1) Jaji wa Mahakama ya Juu atateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa majina yatakayopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(2) Mtu ataweza kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Juu endapo atakuwa amefikisha umri wa miaka arobaini na tano au zaidi na mwenye sifa ya uadilifu na uaminifu katika utekelezaji wa majukumu yake na awe:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) na shahada ya sheria kutoka chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na mamlaka inayoshughulikia elimu ya juu katika Jamhuri ya Muungano; na
(i) awe amefanya kazi ya ujaji katika Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu; au
(ii) awe wakili, mtumishi wa umma au mwana taaluma akiwa na sifa ya kusajiliwa kuwa wakili na amekuwa na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka kumi na tano.

Kiapo cha Jaji wa Mahakama ya Juu
178. Jaji Mkuu, Naibu Jaji Mkuu au Jaji wa Mahakama ya Juu atashika madaraka yake mara tu atakapokuwa ameapishwa na Rais kiapo cha uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria.
Muda wa Jaji wa Mahakama ya Juu kuwa madarakani
179.-(1) Jaji Mkuu atashika nafasi ya madaraka ya Jaji Mkuu hadi atakapofikisha umri wa miaka sabini, isipokuwa tu kama:
(a) atajiuzulu;
(b) atashindwa kutekeleza majukumu yake kutokana na maradhi;
(c) atafariki dunia; au
(d) atavuliwa madaraka ya Jaji Mkuu kwa mujibu wa Katiba hii.
(2) Masharti ya ibara ndogo ya (1) yatatumika pia kwa Naibu Jaji Mkuu na Jaji wa Mahakama ya Juu.
(3) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1) na ya (2), Jaji Mkuu, Naibu Jaji Mkuu na Jaji wa Mahakama ya Juu aliyetimiza umri wa kustaafu atalazimika kuendelea kufanya kazi baada ya kutimiza umri huo hadi amalize kutayarisha na kutoa hukumu au hadi akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla hajatimiza umri wa kustaafu.
(4) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (3), Jaji Mkuu au Naibu Jaji Mkuu aliyetimiza umri wa kustaafu, ataachia nafasi ya madaraka yake, isipokuwa ataendelea kutekeleza shughuli ambazo hajazikamilisha akiwa katika nafasi ya madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu hadi atakapokamilisha shughuli hizo.
Utaratibu wa kukaimu nafasi ya Jaji wa Mahakama ya Juu
180.-(1) Iwapo itatokea kwamba:
(a) nafasi ya madaraka ya Jaji Mkuu itakuwa wazi;
(b) Jaji Mkuu hayupo katika Jamhuri ya Muungano; au
(c) Jaji Mkuu atashindwa kumudu kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote iliyoainishwa katika Katiba hii,
(d) Naibu Jaji Mkuu atatekeleza kazi za Jaji Mkuu hadi atakapoteuliwa Jaji Mkuu mwingine au hadi Jaji Mkuu ambaye alikuwa hayupo au alikuwa hamudu kazi zake atakaporejea kazini.
(2) Ikitokea kwamba nafasi ya madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu itakuwa wazi au endapo Jaji wa Mahakama ya Juu yeyote ameteuliwa kutekeleza kazi za Naibu Jaji Mkuu au kama Jaji wa Mahakama ya Juu atashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, au Jaji Mkuu atamshauri Rais kuwa kazi za Mahakama ya Juu zilivyo kwa wakati huo zinahitaji ateuliwe Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu, basi Rais aweza kumteua Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu kutoka miongoni mwa watu wenye sifa za kuteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama ya Juu watakaopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(3) Mtu atakayeteuliwa kuwa Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu atafanya kazi kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu kwa muda wote utakaotajwa kwenye hati ya kuteuliwa kwake.
(4) Bila kujali masharti ya ibara ndogo ya (2), mtu aliyeteuliwa kuwa Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu ataendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu hadi amalize kutayarisha na kutoa hukumu au hadi amalize shughuli nyingine yoyote inayohusika na rufani au mashauri mengine ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla ya muda wake wa uteuzi haujamalizika au uteuzi wake haujafutwa.
(5) Kwa madhumuni ya masharti ya Ibara hii, Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu atakuwa na mamlaka kamili ya Jaji wa Mahakama ya Juu na atatekeleza kazi zote za Jaji wa Mahakama ya Juu na kwamba idadi ya Majaji wa Mahakama ya Juu iliyotajwa katika Ibara ya 172 haitaathirika kwa sababu tu mmoja au zaidi ya Majaji wa Mahakama ya Juu katika kikao chochote ni Kaimu Jaji wa Mahakama ya Juu.
Utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Juu
181.-(1) Jaji wa Mahakama ya Juu ataondolewa katika nafasi ya madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu kwa sababu ya kushindwa kutekeleza madaraka yake ama kutokana na maradhi ya mwili au akili au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya inayoathiri maadili ya kazi ya Jaji au sheria inayohusu maadili ya uongozi wa umma, na hataondolewa madarakani isipokuwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2).
(2) Endapo Rais anaona kuwa suala la kumuondoa Jaji madarakani linahitaji kuchunguzwa, basi katika hali hiyo utaratibu utakuwa kama ifuatavyo:
(a) Rais anaweza, baada ya kushauriana na Jaji Mkuu, kumsimamisha kazi Jaji huyo;
(b) Rais atateua Tume ambayo itakuwa na Mwenyekiti na Wajumbe wengine wasiopungua wawili na angalau nusu ya wajumbe hao wawe ni Majaji wa Mahakama ya Juu au Mahakama ya Rufani kutoka nchi yoyote iliyomo kwenye Jumuiya ya Madola; na
(c) Tume hiyo itachunguza shauri hilo kisha itatoa taarifa kwa Rais kuhusu maelezo ya shauri hilo na itamshauri Rais kama Jaji huyo anayehusika aondolewe madarakani kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya.
(3) Jaji aliyesimamishwa kazi kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2), ataendelea kulipwa mshahara na maslahi yake mengine hadi Jaji huyo atakapoondolewa kazini na Rais chini ya masharti ya ibara ndogo ya (4).
(4) Endapo Tume iliyoteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2) itamshauri Rais kwamba Jaji ambaye mwenendo wake umechunguzwa na Tume hiyo aondolewe kazini kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote, Rais atamuondoa kazini Jaji huyo na utumishi wake utakuwa umekoma.
(5) Endapo Tume iliyoteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2) itamshauri Rais kwamba Jaji ambaye mwenendo wake umechunguzwa na Tume hiyo asiondolewe, Rais atafuta uamuzi wa kumsimamisha kazi na utumishi wa Jaji huyo utaendelea.
(6) Masharti ya Ibara hii hayatawahusu watu walioteuliwa kukaimu nafasi ya ujaji.
(d) Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano
Mahakama ya Rufani
182.-(1) Kutakuwa na Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano, itakayojulikana kwa kifupi kama “Mahakama ya Rufani” na ambayo itakuwa na:
(a) Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani;
(b) Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani; na
(c) Majaji wengine wasiopungua kumi na saba.
(2) Jaji wa Mahakama ya Rufani atateuliwa kwa kuzingatia sifa zitakazoainishwa katika Katiba hii na uwakilishi wa kila upande wa Jamhuri ya Muungano.
(3) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu utaratibu wa kuwasilisha rufaa mbele ya Mahakama ya Rufani.

Akidi ya kikao cha Mahakama ya Rufani
183.-(1) Akidi ya kila kikao cha Mahakama ya Rufani itakuwa ni Majaji wa Mahakama ya Rufani watatu.
(2) Kila shauri linalohitaji uamuzi wa Mahakama ya Rufani litaamuliwa kwa kufuata kauli ya walio wengi kati ya Majaji wa Mahakama ya Rufani waliosikiliza shauri husika.
Mamlaka ya Mahakama ya Rufani
184.-(1) Mahakama ya Rufani itakuwa na mamlaka ya:
(a) kusikiliza na kuamua kuhusu rufaa inayowasilishwa mbele ya Mahakama ya Rufani kutokana na hukumu au uamuzi wowote wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar au Mahakama yoyote ya chini iliyopewa mamlaka maalum ya kusikiliza mashauri ambayo kwa kawaida husikilizwa na Mahakama Kuu;
(b) kufanya mapitio ya maamuzi ya Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar au Mahakama yoyote ya chini iliyopewa mamlaka maalum ya kusikiliza mashauri ambayo kwa kawaida husikilizwa na Mahakama Kuu; na
(c) kufanya jambo jingine kama itakavyoainishwa katika sheria iliyotungwa na Bunge.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti zaidi kuhusu uendeshaji wa Mahakama ya Rufani.

Madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Rufani
185.-(1) Jaji wa Mahakama ya Rufani atakuwa na madaraka ya kusikiliza na kuamua rufaa yoyote katika Mahakama ya Rufani.
(2) Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (1), iwapo Jaji wa Mahakama ya Rufani kabla ya kuteuliwa kwake alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar, Jaji huyo anaweza kuendelea kufanya kazi katika Mahakama aliyotoka hadi amalize kutayarisha na kutoa hukumu au hadi akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla hajateuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani.
(3) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (2), itakuwa ni halali kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kutoa hukumu au uamuzi mwingine wowote unaohusika kwa kutumia na kutaja nafasi ya madaraka aliyokuwa akishika kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani na endapo hukumu hiyo au uamuzi huo utapingwa kwa njia ya rufani itakayowasilishwa mbele ya Mahakama ya Rufani, Jaji huyo hatakuwa na mamlaka ya kusikiliza rufani hiyo.

(e) Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Rufani
Uteuzi wa Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani
186.-(1) Kutakuwa na Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani ambaye atateuliwa na Rais kutoka orodha ya majina ya watu watatu yaliyopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(2) Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani atakuwa ndiye Mkuu wa Mahakama ya Rufani na msaidizi wa Jaji Mkuu katika utendaji wa kazi katika Mahakama ya Rufani, na katika madaraka hayo, Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani atatekeleza kazi na shughuli atakazopangiwa mara kwa mara na Jaji Mkuu.
(3) Mtu ataweza kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani endapo atakuwa amefikisha umri wa miaka arobaini na tano au zaidi na mwenye sifa ya uadilifu na uaminifu katika utekelezaji wa majukumu yake na:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano mwenye tabia njema, uadilifu na uaminifu;
(b) awe na shahada ya sheria kutoka chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na mamlaka inayoshughulikia elimu ya juu katika Jamhuri ya Muungano; na
(i) awe amefanya kazi ya ujaji katika Mahakamu Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar; au
(ii) awe wakili, mtumishi wa umma au mwanataaluma akiwa na sifa ya kusajiliwa kuwa wakili na amekuwa na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka kumi na tano.
Uteuzi wa Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani
187.-(1) Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani atateuliwa na Rais kutoka katika orodha ya majina ya watu watatu yatakayopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama na atakuwa ndiye Msaidizi Mkuu wa Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani.
(2) Mtu atateuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani endapo atakuwa na sifa zilizoainishwa katika Ibara ya 186(3).

Uteuzi wa Jaji wa Mahakama ya Rufani
188.-(1) Jaji wa Mahakama ya Rufani atateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa majina yatakayopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(2) Mtu anaweza kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani endapo atakuwa na sifa zilizoainishwa katika Ibara ya 186(3).
Kiapo cha Jaji wa Mahakama ya
189. Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani, Makamu Mwenyekiti au Jaji wa Mahakama ya Rufani atashika madaraka yake mara tu atakapoapishwa na Rais kiapo cha uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria.
Muda wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Jaji wa Mahakama ya Rufani kuwa madarakani
190.-(1) Mwenyekiti au Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani atashika nafasi ya madaraka yake hadi atakapofikisha umri wa miaka sabini, isipokuwa kama:
(a) atajiuzulu;
(b) atashindwa kumudu kazi kutokana na maradhi;
(c) ataondolewa katika nafasi ya madaraka ya Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani kwa mujibu wa Katiba hii; au
(d) atafariki dunia.
(2) Jaji aliyetimiza umri wa kustaafu atalazimika kuendelea kufanya kazi baada ya kutimiza umri huo hadi amalize kutayarisha na kutoa hukumu au hadi akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla hajatimiza umri wa kustaafu.
(3) Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (2), Mwenyekiti au Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani aliyetimiza umri wa kustaafu, ataachia nafasi ya madaraka ya Mwenyekiti au Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani, isipokuwa ataendelea kutekeleza shughuli ambazo hajazikamilisha akiwa katika nafasi ya madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Rufani hadi atakapokamilisha shughuli hizo.

Utaratibu wa kukaimu nafasi ya Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani
191.-(1) Iwapo itatokea kwamba:
(a) nafasi ya madaraka ya Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani ipo wazi;
(b) Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani hayupo katika Jamhuri ya Muungano; au
(c) Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani ameshindwa kutekeleza kazi kwa mujibu wa Katiba hii,
Makamu Mwenyekiti atatekeleza kazi za Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani hadi atakapoteuliwa Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani mwingine au hadi Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani ambaye alikuwa hayupo nchini au alikuwa hawezi kumudu kazi zake kutokana na maradhi atakaporejea kazini.
(2) Endapo ufanisi wa kazi za Mahakama ya Rufani utahitaji ateuliwe Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani, Tume ya Utumishi wa Mahakama itamshauri Rais kumteua Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani.
(3) Endapo Rais ataridhika na ushauri wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, atamteua Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani kutoka miongoni mwa watu wanaoweza kuteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani.
(4) Mtu atakayeteuliwa kuwa Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani atafanya kazi kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa muda wote utakaotajwa wakati wa kuteuliwa kwake, au kama muda haukutajwa, basi hadi uteuzi utakapofutwa na Rais.
(5) Bila kujali masharti ya ibara ndogo ya (4), mtu aliyeteuliwa kuwa Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani ataendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani hadi amalize kutayarisha na kutoa hukumu au hadi amalize shughuli nyingine yoyote inayohusika na rufani au mashauri mengine ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla ya muda wake wa kazi haujamalizika au uteuzi wake haujafutwa.
(6) Kwa madhumuni ya Ibara hii, Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani atakuwa na mamlaka kamili ya Jaji wa Mahakama ya Rufani na atatekeleza kazi zote za Jaji wa Mahakama ya Rufani.
Utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Rufani
192. Kwa mujibu wa Katiba hii, masharti kuhusu utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Rufani, utakuwa kama ulivyoainishwa katika Ibara ya 181 inayoweka masharti na utaratibu wa nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Juu.
(f) Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano
Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano na Mamlaka yake
193.-(1) Kutakuwa na Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano, itakayojulikana kwa kifupi kama “Mahakama Kuu”, ambayo mamlaka yake yatakuwa kama ilivyoelezwa katika Katiba hii au katika sheria nyingine yoyote.
(2) Iwapo Katiba hii au sheria nyingine yoyote haikutamka wazi kwamba shauri la aina iliyotajwa mahsusi litasikilizwa kwanza katika Mahakama ya ngazi iliyotajwa mahsusi kwa ajili hiyo, basi Mahakama Kuu itakuwa na mamlaka ya kusikiliza kila shauri la aina hiyo.
(3) Hali kadhalika, Mahakama Kuu itakuwa na uwezo wa kutekeleza shughuli yoyote ambayo kwa mujibu wa mila za kisheria zinazotumika Tanzania, shughuli ya aina hiyo kwa kawaida hutekelezwa na Mahakama Kuu:
Isipokuwa kwamba masharti ya ibara hii ndogo yatatumika bila kuathiri mamlaka ya Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano kama ilivyoelezwa katika Katiba hii au katika sheria nyingine yoyote.

Uteuzi wa Jaji wa Mahakama Kuu
194.-(1) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (2), mtu aweza tu kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ikiwa ana sifa maalum, kama ilivyofafanuliwa katika ibara ndogo ya (2), na awe mtu ambaye amekuwa na mojawapo ya sifa maalum kwa muda usiopungua miaka kumi.
(2) Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa ibara ndogo ya (3), (9) na (10), “sifa maalum” maana yake ni mtu aliye na shahada ya sheria toka chuo cha elimu ya juu kinachotambulika kwa mujibu wa sheria na:
(a) amekuwa hakimu;
(b) amefanya kazi katika utumishi wa umma akiwa na sifa za kufanya kazi ya uwakili au ni wakili wa kujitegemea;
(c) ana sifa ya kusajiliwa kuwa wakili; au
(d) amekuwa na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka kumi.
(3) Iwapo Rais ataridhika kwamba ijapokuwa mtu mwenye sifa mojawapo ya hizo sifa maalum hakuwa na sifa hiyo kwa muda usiopungua miaka kumi, lakini mtu huyo ana uwezo, ujuzi na kwa kila hali anafaa kukabidhiwa madaraka ya Jaji wa Mahakama Kuu na kuna sababu za kumfanya mtu huyo astahili kukabidhiwa madaraka hayo, basi Rais aweza kutengua lile sharti la kuwa na sifa maalum kwa muda usiopungua miaka kumi, na baada ya kushauriana na Tume ya Utumishi wa Mahakama, Rais aweza kumteua mtu huyo kuwa Jaji wa Mahakama Kuu.
(4) Ikitokea kwamba kiti cha Jaji yeyote kitakuwa wazi au ikiwa Jaji yeyote atateuliwa kuwa Kaimu Jaji au kama atashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, au kama Jaji Mkuu atamshauri Rais kuwa kazi za Mahakama Kuu zilivyo wakati huo zahitaji ateuliwe Kaimu Jaji, basi Rais aweza, baada ya kushauriana na Jaji Mkuu kama kawaida, kumteua Kaimu Jaji kutoka miongoni mwa watu wenye sifa maalum:
Isipokuwa kwamba:
(a) mtu hatahesabiwa kuwa hastahili kuteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo kwa sababu tu kwamba ametimiza umri uliotajwa katika ibara ndogo ya (1) ya Ibara ya 195; na
(b) kwa madhumuni ya kumteua Kaimu Jaji kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo, Rais aweza kutengua lile sharti la kuwa na sifa maalum kwa muda usiopungua miaka kumi kwa sababu kama zile zilizotajwa katika ibara ndogo ya (3).
(5) Mtu yeyote atakayeteuliwa kuwa Kaimu Jaji kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (4), ataendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji kwa muda wowote utakaotajwa wakati wa kuteuliwa kwake au, kama muda haukutajwa, mpaka uteuzi wake utakapofutwa na Rais, lakini bila ya kujali kwamba muda wake wa kazi umemalizika au kwamba uteuzi wake umefutwa, mtu huyo aweza kuendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwisha anza kuyasikiliza kabla muda wake wa kazi haujamalizika au kabla ya uteuzi wake haujafutwa.
(6) Kutakuwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu, ambaye katika ibara zifuatazo kwenye Katiba hii atatajwa tu kwa kifupi kama “Jaji Kiongozi”, na Majaji wengine wa Mahakama Kuu wasiopungua thelathini watakaoteuliwa na Rais baada ya kushauriana na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(7) Jaji Kiongozi atateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa majina ya Majaji watatu waliopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(8) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii au sheria nyingine yoyote kuhusu madaraka ya Jaji Mkuu aliyetajwa katika Ibara ya 175, Jaji Kiongozi atakuwa ndiye msaidizi maalum wa Jaji Mkuu katika utendaji wa kazi katika Mahakama Kuu na Mahakama nyinginezo zote za ngazi ya chini yake, na katika madaraka hayo Jaji Kiongozi atatekeleza kazi na shughuli atakazoagizwa au kuelekezwa mara kwa mara na Jaji Mkuu, na kwa madhumuni ya Ibara hii, Jaji Kiongozi atakuwa mkuu wa Mahakama Kuu.
(9) Mbali ya madaraka yake ya kawaida ya Jaji wa Mahakama Kuu kama Majaji wengine wote wa Mahakama Kuu, Jaji Kiongozi atakuwa pia na mamlaka ya kutekeleza kazi na shughuli zote zinazoambatana na mamlaka ya Mahakama Kuu ambazo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au ya sheria nyingine yoyote au kufuatana na mila za kisheria zinazotumika Tanzania hutakiwa zitekelezwe na Mkuu wa Mahakama Kuu:

Isipokuwa kwamba masharti ya ibara hii ndogo hayatatumika kwa ajili ya utekelezaji wa kazi au shughuli ambazo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au ya Sheria nyingine yoyote au kufuatana na mila za kisheria zinazotumika Tanzania zimetajwa mahsusi au zinafahamika kuwa ni kazi au shughuli zinazotakiwa kutekelezwa tu na Jaji Mkuu.
(10) Kwa madhumuni ya kuondoa mashaka juu ya ufafanuzi au utekelezaji wa masharti ya ibara ndogo ya (8) na (9), inatamkwa rasmi hapa kwamba isipokuwa kama masharti ya Katiba hii au ya sheria nyingine yoyote yameagiza vinginevyo, Jaji Mkuu aweza kutoa kwa Jaji Kiongozi maelekezo ya mara kwa mara kuhusu utendaji wa kazi na shughuli zake kama Mkuu wa Mahakama Kuu; vile vile, Jaji Mkuu atakuwa na uwezo wa kukasimu kwa Jaji Kiongozi baadhi ya madaraka yake ya uongozi na usimamizi juu ya utekelezaji wa kazi katika Mahakama Kuu na Mahakama nyinginezo zote za ngazi ya chini yake, na kila inapohitajika, Jaji Mkuu anaweza kutekeleza yeye mwenyewe moja kwa moja madaraka yake yoyote aliyoyakasimu kwa Jaji Kiongozi.
(11) Ikitokea kwamba kiti cha Jaji Kiongozi kitakuwa wazi au kwamba Jaji Kiongozi atashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, basi kazi hizo zitatekelezwa na Jaji mmojawapo atakayeteuliwa na Rais kwa ajili hiyo, na Jaji huyo atatekeleza kazi hizo mpaka atakapoteuliwa Jaji Kiongozi mwingine na kushika madaraka ya kiti cha Jaji Kiongozi au mpaka Jaji Kiongozi mwenyewe ambaye alikuwa hamudu kazi zake atakaporejea kazini.

Muda wa Jaji wa Mahakama Kuu kushika madaraka
195.-(1) Kila Jaji wa Mahakama Kuu atalazimika kuacha kazi yake atakapotimiza umri wa miaka sitini na tano, lakini masharti ya ibara hii ndogo yatatumika bila kuathiri masharti katika Ibara hii.
(2) Jaji yeyote wa Mahakama Kuu anaweza kustaafu kazi katika utumishi wa umma wa Jamhuri ya Muungano wakati wowote baada ya kutimiza umri wa miaka sitini, isipokuwa kama Rais ataagiza kwamba asistaafu na iwapo Rais ataagiza hivyo, basi huyo Jaji atakayehusika na maagizo hayo ya Rais hatakuwa na haki ya kustaafu mpaka upite kwanza muda wowote utakaotajwa na Rais kwa ajili hiyo.
(3) Iwapo Rais ataona kuwa kwa ajili ya manufaa ya umma inafaa Jaji aliyetimiza umri wa miaka sitini na tano aendelee kufanya kazi, na huyo Jaji mwenyewe anakubali kwa maandishi kuendelea kufanya kazi, basi Rais aweza kuagiza kuwa Jaji huyo aendelee kufanya kazi kwa muda wowote utakaotajwa na Rais.
(4) Bila ya kujali kwamba Jaji ametimiza umri ambao analazimika kuacha kazi kwa mujibu wa masharti ya Ibara hii, mtu anayefanya kazi ya Jaji wa Mahakama Kuu aweza kuendelea kufanya kazi baada ya kutimiza umri huo mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwishaanza kuyasikiliza kabla hajatimiza umri huo wa kuacha kazi.
Utaratibu wa kushughulikia nidhamu kwa Jaji wa Mahakama
196. Utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama Kuu, utakuwa kama ulivyoainishwa katika Ibara ya 181 inayoweka utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya Jaji wa Mahakama ya Juu.

Kiapo cha Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano
197.-(1) Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano atashika madaraka yake mara tu atakapokuwa ameapishwa na Rais kiapo cha uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), Jaji Kiongozi atashika madaraka yake atakapokuwa ameapishwa na Rais kiapo cha uaminifu kinachohusika na utendaji wa kazi za Jaji Kiongozi kitakachoweka kwa mujibu wa sheria.
(g) Mahakama Kuu ya Zanzibar
Mahakama Kuu ya Zanzibar
198.-(1) Kutakuwa na Mahakama Kuu ya Zanzibar itakayoanzishwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar.
(2) Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa Sura hii, ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika Sura hii hayazuii kuendelea kuwapo au kuanzishwa, kwa mujibu wa sheria zinazotumika Zanzibar, kwa Mahakama Kuu ya Zanzibar au mahakama zilizo chini ya Mahakama Kuu ya Zanzibar.

Mamlaka ya Mahakama Kuu ya Zanzibar
199.-(1) Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 144, mamlaka ya Mahakama Kuu ya Zanzibar yatakuwa kama itakavyoelezwa katika sheria zinazotumika Zanzibar.
(2) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii au sheria nyingine yoyote iliyotungwa na Bunge, iwapo sheria yoyote iliyotungwa na Bunge inayotumika Tanzania Bara na vile vile Zanzibar imekabidhi madaraka yoyote kwa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano, basi Mahakama Kuu ya Zanzibar yaweza kutekeleza madaraka hayo kwa kiasi kile kile inavyoweza kutekeleza Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano.
(h) Usimamizi wa Shughuli za Mahakama
Msajili Mkuu wa Mahakama
200.-(1) Kutakuwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano atakayeitwa “Msajili Mkuu wa Mahakama”, atakayeteuliwa na Rais kufuatia mapendekezo ya Tume ya Utumishi wa Mahakama.
(2) Mtu anaweza kuteuliwa kuwa Msajili Mkuu wa Mahakama endapo ni mwenye sifa ya uadilifu, tabia njema na uaminifu katika utekelezaji wa majukumu yake na awe:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano; na
(b) na shahada ya sheria kutoka chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na mamlaka inayoshughulikia elimu ya juu katika Jamhuri ya Muungano; na
(i) awe amefanya kazi ya uhakimu katika Mahakama za Jamhuri ya Muungano; au
(ii) amekuwa mtumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano,
na amekuwa na sifa hizo mfululizo kwa muda usiopungua miaka kumi.
Majukumu ya Msajili Mkuu wa Mahakama
201.-(1) Msajili Mkuu wa Mahakama atakuwa na majukumu yafuatayo:
(a) kusimamia utekelezaji wa shughuli za Mahakama;
(b) kuratibu masuala ya Mahakama; na
(c) majukumu mengine atakayopangiwa na Jaji Mkuu.
(2) Katika kutekeleza majukumu yake, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano atawajibika kwa Jaji Mkuu.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama
202.-(1) Kutakuwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama atakayeteuliwa na Rais.
(2) Mtu hatateuliwa kushika nafasi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama isipokuwa tu kama ni:
(a) mtumishi mwandamizi wa umma;
(b) mwenye weledi na uzoefu katika masuala ya utawala na mambo ya fedha; na
(c) mwadilifu na mwenye tabia na mwenendo usiotiliwa shaka na jamii.
Majukumu ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama
203.-(1) Mtendaji Mkuu wa Mahakama atakuwa na majukumu yafuatayo:
(a) Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama;
(b) Ofisa Masuuli wa Mahakama;
(c) msimamizi mkuu wa Mfuko wa Mahakama;
(d) msimamizi wa masuala ya utawala ya Mahakama; na
(e) kutekeleza kazi nyingine atakazopangiwa na Jaji Mkuu.
(2) Katika kutekeleza majukumu yake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama atawajibika kwa Jaji Mkuu.

SEHEMU YA TATU
TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA NA MFUKO WA MAHAKAMA
(a) Tume ya Utumishi wa Mahakama
Tume ya Utumishi wa Mahakama
204.-(1) Kutakuwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama ambayo itakuwa na wajumbe kumi na moja watakaoteuliwa na Rais kama ifuatavyo:
(a) Jaji Mkuu ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b) Mwanasheria Mkuu wa Serikali;
(c) Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani;
(d) Jaji Mkuu wa Zanzibar;
(e) Jaji mmoja wa Mahakama ya Juu;
(f) Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani;
(g) Jaji Kiongozi;
(h) Mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika;
(i) Mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Zanzibar;
(j) Wawakilishi wawili wa vitivo vya sheria kutoka vyuo vikuu, mmoja kutoka Tanzania Bara na mmoja kutoka Zanzibar watakaopendekezwa na vyuo vya elimu ya juu husika; na
(k) Mtendaji Mkuu wa Mahakama ambaye atakuwa Katibu.
(2) Tume ya Utumishi wa Mahakama inaweza kumualika mtu mwingine yeyote mwenye utaalamu mahsusi kushiriki katika kikao chochote cha Tume, isipokuwa mtu huyo hatakuwa na haki ya kupiga kura.
(3) Tume ya Utumishi wa Mahakama itaweka utaratibu wa kuendesha vikao vyake.
Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama
205.-(1) Tume ya Utumishi wa Mahakama itakuwa na wajibu wa kuendeleza na kuwezesha uhuru na uwajibikaji wa Mahakama na utoaji haki wenye ufanisi, mafanikio na uwazi.
(2) Tume ya Utumishi wa Mahakama itakuwa na wajibu wa:
(a) kupendekeza kwa Rais majina ya watu wanaofaa kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu, Naibu Jaji Mkuu, Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani, Makamu Mwenyekiti wa Mahakama ya Rufani, Majaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi na Majaji wa Mahakama Kuu;
(b) kupitia na kupendekeza masharti ya utumishi wa Majaji, Wasajili, Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama ikiwemo masuala yanayohusu maadili, nidhamu na maslahi yao;
(c) kupendekeza Serikalini hatua za kuimarisha Mahakama ili kuongeza ufanisi katika utoaji haki; na
(d) kutekeleza majukumu yoyote itakayopewa kwa mujibu wa Katiba hii au sheria.
(3) Katika kutekeleza majukumu yake, Tume ya Utumishi wa Mahakama inaweza kukasimu madaraka yake kwa kamati mbalimbali zitakazoundwa kwa mujibu wa sheria.
(4) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (2)(b), mapendekezo ya maslahi kwa Majaji, mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama yatawasilishwa kwenye chombo chenye jukumu la kusimamia maslahi ya watumishi wa umma.
(5) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti ya utekelezaji wa majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Uanachama katika vyama vya siasa
206. Itakuwa ni marufuku kwa Jaji wa Mahakama ya Juu, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Msajili Mkuu wa Mahakama, Hakimu, na Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa, isipokuwa atakuwa na haki ya kupiga kura kuchagua viongozi katika vyombo vya uwakilishi.

(b) Mfuko wa Mahakama
Mfuko wa Mahakama
207.-(1) Kutakuwa na Mfuko wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano ambao utakuwa chini ya usimamizi wa Mtendaji Mkuu wa Mahakama.
(2) Mfuko wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano utatumika kwa ajili ya kugharamia shughuli za utawala na uendeshaji wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano na shughuli nyingine muhimu katika utekelezaji wa majukumu ya Mahakama.
(3) Serikali itahakikisha kwamba katika kila bajeti ya mwaka wa fedha wa Serikali, inatenga kwa kiwango kinachotosha fedha ambazo zitaingizwa katika Mfuko wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano.
(4) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu uendeshaji wa Mfuko wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano.

SURA YA KUMI NA TATU
UTUMISHI WA UMMA KATIKA JAMHURI YA MUUNGANO
Misingi mikuu ya utumishi wa umma
208.-(1) Kutakuwa na utumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano utakaozingatia misingi mikuu ifuatayo:
(a) kwamba utumishi wa umma ni dhamana kutoka kwa wananchi na hivyo mtumishi anatakiwa kutumikia wananchi kwa uadilifu, uaminifu na unyenyekevu;
(b) kutoa huduma kwa umma kwa wakati, kwa njia ya haki, usawa na bila upendeleo; na
(c) kuhakikisha kwamba uteuzi na ajira katika nafasi mbalimbali unazingatia uwezo wa kitaaluma, weledi, maarifa, ujuzi, usawa wa kijinsia na uzoefu katika eneo husika na fursa kwa watu wenye ulemavu.
(2) Misingi ya utumishi wa umma iliyoainishwa katika Ibara hii itazingatiwa na kutumika katika uteuzi wa kushika nafasi za madaraka ya uongozi katika:
(a) mamlaka katika mihimili ya dola;
(b) taasisi na idara zote za Serikali; na
(c) mashirika, makampuni na wakala wa Serikali.
(3) Bunge litatunga sheria kuweka masharti ya utekelezaji wa misingi ya utumishi iliyoainishwa katika ibara ndogo ya (1).
Ajira na uteuzi wa kiongozi na mtumishi wa umma katika taasisi za Muungano
209.-(1) Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, ajira katika utumishi wa umma na uteuzi katika nafasi za madaraka ya uongozi na utumishi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano na taasisi zake, itatolewa na kufanyika kwa kuzingatia taaluma, uadilifu na weledi.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), uteuzi wa kiongozi na mtumishi katika taasisi au wizara ya Muungano utafanyika kwa kuzingatia uwakilishi wa pande mbili za Muungano, usawa wa jinsia na watu wenye ulemavu.

Tume ya Utumishi wa Umma
210.-(1) Kutakuwa na Tume ya Utumishi wa Umma itakayokuwa na Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wengine watano watakaoteuliwa na Rais.
(2) Katika kuteua wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Umma, Rais atazingatia misingi ya utumishi wa umma iliyoainishwa katika Ibara ya 208.
(3) Sifa za Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Umma zitakuwa kama ifuatavyo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) awe na shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambulika kwa mujibu wa sheria;
(c) awe na uzoefu wa utumishi wa umma, upeo mkubwa katika mambo ya utumishi, utawala na mambo ya jamii kwa kipindi kisichopungua miaka kumi, isipokuwa kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wawe na uzoefu huo kwa kipindi kisichopungua miaka kumi na tano; na
(d) awe na heshima, weledi, uaminifu, uadilifu na asiye na tabia au mwenendo wenye kutiliwa shaka na jamii.

Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma
211.-(1) Kutakuwa na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma ambaye atateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano.
(2) Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma atakuwa ndiye Mkuu wa Sekretarieti ya Utumishi wa Umma, Mtendaji Mkuu na mtekelezaji wa majukumu ya kila siku ya Tume.
Mamlaka na Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Umma
212.-(1) Tume ya Utumishi wa Umma itakuwa ni chombo cha juu chenye mamlaka ya nidhamu na uratibu wa mambo yote kuhusu utumishi wa umma.
(2) Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Umma yatakuwa ni:
(a) kuhamasisha utekelezaji wa misingi ya utumishi wa umma;
(b) kushughulikia rufaa zinazowasilishwa na watumishi wa umma dhidi ya uamuzi wa mamlaka mbalimbali za nidhamu katika utumishi wa umma; na
(c) kutekeleza majukumu mengine yoyote kwa kadri yatakavyoainishwa katika sheria kuhusu masuala ya utumishi wa umma.
(3) Bunge litatunga sheria itakayoainisha utaratibu wa kuweka masharti ya utekelezaji wa kazi za Tume ya Utumishi wa Umma.

Tume ya Mishahara
213.-(1) Kutakuwa na Tume ya Mishahara na maslahi ambayo itashughulikia mishahara na maslahi ya watumishi wa umma.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu muundo, majukumu na mambo mengine kuhusu utekelezaji wa Tume ya Mishahara.
Tume za kisekta
214. Kutakuwa na Tume mbalimbali za kisekta zitakazoanzishwa kwa mujibu wa sheria zitakazotungwa na Bunge kwa ajili ya usimamizi, uratibu na utoaji wa huduma za jamii.

SURA YA KUMI NA NNE
UCHAGUZI KATIKA VYOMBO VYA UWAKILISHI NA VYAMA VYA SIASA

SEHEMU YA KWANZA
UWAKILISHI WA WANANCHI
Ushiriki katika
215.-(1) Kila raia wa Jamhuri ya Muungano mwenye umri wa miaka kumi na nane au zaidi na mwenye akili timamu ana haki ya kupiga kura na haki ya kuandikishwa na kushiriki kupiga kura katika uchaguzi au kura ya maoni.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), mamlaka ya kusimamia uchaguzi itazingatia misingi kwamba:
(a) wananchi wanatumia haki ya kisiasa kwa mujibu wa Katiba hii;
(b) watu wenye ulemavu wanapewa fursa za uwakilishi;
(c) kunakuwa na haki ya kila raia kupiga kura kufuatana na utashi wa uwakilishi na kura sawa; na
(d) uchaguzi unakuwa huru na wa haki ambao-
(i) ni wa kura ya siri;
(ii) hauna matumizi ya nguvu, vitisho, vishawishi wala rushwa;
(iii) hauna matamshi au vitendo vinavyoashiria ukabila, ukanda, udini, dharau na kashfa kwa jinsi au unyanyapaa kwa watu wenye ulemavu au makundi madogo katika jamii;
(iv) unaendeshwa na kusimamiwa na chombo huru; na
(v) unaendeshwa bila upendeleo au kuegemea upande wowote, ulio makini na unaoonyesha uwajibikaji wa watendaji.
(3) Katika kutekeleza masharti ya ibara ndogo ya (1) na (2), mamlaka ya nchi itaweka utaratibu utakaowezesha:
(a) mamlaka zinazosimamia uchaguzi kutangaza majimbo kwa madhumuni ya uchaguzi wa Wabunge;
(b) uteuzi wa wagombea;
(c) uandikishaji wa wapiga kura;
(d) kuendesha na kusimamia uchaguzi na kura ya maoni; na
(e) utaratibu wa kufanya uchaguzi kuwa mwepesi, wazi na unaozingatia mahitaji ya watu wenye mahitaji maalum.
(4) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (2) na kwa kuzingatia masharti kuhusu kupinga matokeo ya uchaguzi wa Rais, mgombea urais ana haki ya kufungua shauri mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi, anayoamini yamekiuka masharti ya Katiba hii au sheria.
(5) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu utekelezaji wa masharti ya Ibara hii.

Mgombea huru
216.-(1) Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 88 na Ibara ya 140, mtu atakuwa na haki ya kuwa mgombea huru katika uchaguzi unaosimamiwa na Tume Huru ya Uchaguzi.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kwa mgombea huru kuhusu-
(a) idadi ya wapiga kura wanaohitajika kumdhamini kwa ngazi ya nafasi anayogombea;
(b) kipindi ambacho amekoma kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa kabla ya siku ya uchaguzi;
(c) kutojiunga na chama cha siasa katika kipindi ambacho atakuwa kiongozi baada ya kuchaguliwa;
(d) utaratibu wa kuainisha vyanzo vya ndani na nje vya mapato ya kugharamia kampeni za uchaguzi;
(e) utaratibu wa kuainisha vigezo na sifa zitakazotumiwa kuwapata viongozi wa ngazi za juu kitaifa;
(f) kuweka wazi ilani ya uchaguzi inayoonesha mipango ya uendeshaji wa nchi;
(g) kuweka masharti yanayozuia sera zenye mrengo wa kuligawa Taifa; na
(h) masharti mengine kwa kadri itakavyoonekana inafaa.

SEHEMU YA PILI
TUME HURU YA UCHAGUZI
(a) Tume Huru ya Uchaguzi
Kuundwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi
217.-(1) Kutakuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano itakayoitwa “Tume Huru ya Uchaguzi”.
(2) Tume Huru ya Uchaguzi itakuwa na Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wengine saba watakaoteuliwa na Rais baada ya kupendekezwa na Kamati ya Uteuzi.
(3) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi watashika madaraka mara baada ya kuapishwa na Rais.
(4) Uteuzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi utafanywa kwa misingi kwamba, endapo Mwenyekiti atateuliwa kutoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano, basi Makamu Mwenyekiti atateuliwa kutoka upande wa pili wa Jamhuri ya Muungano.
(5) Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi watakuwa na sifa zifuatazo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa, na angalau mmoja kati ya wazazi wake ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) awe ni mtu aliyewahi kushika nafasi ya madaraka ya Jaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu na ameshika nafasi ya madaraka hayo kwa kipindi kisichopungua miaka mitano;
(c) awe ni mwaminifu, mwadilifu na mwenye mwenendo usiotiliwa shaka na jamii;
(d) awe ni mtu ambaye hajawahi kushika nafasi ya madaraka ya juu katika chama cha siasa; na
(e) awe ni mtu ambaye hajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai.
(6) Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi atakuwa na sifa zifuatazo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa na angalau mmoja kati ya wazazi wake ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) awe ni mtu mwaminifu, mwadilifu, na mwenye mwenendo usiotiliwa shaka na jamii;
(c) awe ni mtu ambaye hajawahi kushika nafasi ya madaraka ya juu katika chama cha siasa;
(d) awe na shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa kwa mujibu wa sheria; na
(e) awe ni mtu ambaye hajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai.
(7) Kwa madhumuni ya Ibara hii, watu wafuatao hawatakuwa na sifa ya kuwa Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi:
(a) Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi au Diwani; au
(b) mtu ambaye ni mtumishi wa umma.
(8) Uteuzi wa Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi utazingatia uwakilishi wa kila upande wa Jamhuri ya Muungano.

Kamati ya Uteuzi
218.-(1) Kutakuwa na Kamati ya Uteuzi wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi itakayokuwa na Wajumbe wafuatao:
(a) Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano ambaye atakuwa ni Mwenyekiti;
(b) Jaji Mkuu wa Zanzibar ambaye atakuwa Makamu Mwenyekiti;
(c) Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano;
(d) Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar;
(e) Jaji Kiongozi; na
(f) Mwenyekiti wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
(2) Mkurugenzi wa Tume Huru ya Uchaguzi atakuwa Katibu wa Kamati ya Uteuzi.
(3) Kamati ya Uteuzi itakuwa na jukumu la kupokea na kuchambua majina ya watu walioomba kuwa Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi kwa mujibu wa utaratibu utakaoainishwa na sheria.
(4) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (3), Kamati ya Uteuzi mara baada ya kuchambua majina ya watu walioomba kuwa Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi, itapendekeza kwa Rais majina ya watu wanaofaa kuteuliwa kuwa wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi.
(5) Rais atateua Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi kutoka miongoni mwa majina yaliyowasilishwa na Kamati ya Uteuzi.
(6) Bunge litatunga sheria ambayo pamoja na mambo mengine itaweka masharti kuhusu kiapo cha Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wengine wa Tume Huru ya Uchaguzi.
Muda wa Mjumbe wa Tume kushika madaraka
219.-(1) Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi atashika nafasi ya madaraka kwa kipindi cha miaka mitano na anaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine kimoja cha miaka mitano.
(2) Mtu atakoma kuwa mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi endapo litatokea tukio lolote kati ya matukio yafuatayo:
(a) kujiuzulu;
(b) kutokuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa sababu ya maradhi;
(c) kukiuka Kanuni za Maadili ya Uongozi wa Umma;
(d) kutiwa hatiani kwa kosa ambalo adhabu yake ni kifungo gerezani kwa muda unaozidi siku saba;
(e) kupoteza sifa ya kuteuliwa kuwa mjumbe; au
(f) kufariki dunia.
(3) Kwa madhumuni ya utekelezaji bora wa majukumu ya Tume, kutakuwa na kanuni za maadili kama zitakavyoainishwa na sheria.
(4) Endapo suala la kumuondoa Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi kwa kukiuka kanuni za maadili litajitokeza, Rais atateua Kamati itakayoundwa na:
(a) Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b) Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora;
(c) Mjumbe wa Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji; na
(d) Mawakili, mmoja kutoka Tanzania Bara na mmoja kutoka Zanzibar watakaopendekezwa na Chama cha Wanasheria Tanganyika na Chama cha Wanasheria Zanzibar,
na Kamati hiyo itafanya uchunguzi wa suala hilo na kisha kutoa mapendekezo kwa Rais.
(6) Endapo, baada ya uchunguzi, Kamati itapendekeza kuwa mjumbe huyo aondolewe madarakani, Rais atamuondoa mjumbe huyo madarakani na endapo Kamati itapendekeza kuwa mjumbe huyo asiondolewe, suala la kumuondoa mjumbe huyo litakoma.
(7) Kamati itaweka utaratibu wa kufanya uchunguzi.
Wajibu wa Tume Huru ya Uchaguzi
220.-(1) Tume Huru ya Uchaguzi itakuwa na wajibu wa:
(a) kusimamia na kuendesha shughuli zote za uchaguzi wa Rais na Wabunge katika Jamhuri ya Muungano;
(b) kusimamia na kuendesha kura ya maoni;
(c) kusimamia na kuratibu uandikishaji wa wapiga kura katika Jamhuri ya Muungano;
(d) kugawa na kutangaza majimbo ya uchaguzi wa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano; na
(e) kutangaza matokeo ya uchaguzi wa Rais na Wabunge, au matokeo ya kura ya maoni.
(2) Tume Huru ya Uchaguzi itakuwa na wajibu wa kutoa elimu ya mpiga kura wakati wa uchaguzi au kura ya maoni na kuratibu utoaji wa elimu ya uraia kuhusu uchaguzi, au kura ya maoni na kusimamia asasi za kiraia, taasisi, jumuiya au makundi ya watu yatakayotoa elimu hiyo.
(3) Tume Huru ya Uchaguzi pia ina wajibu wa kuhakikisha kuwepo kwa:
(a) uhuru wa wananchi katika kutumia haki ya uchaguzi na kuchaguliwa kupitia vyama vya siasa au mgombea huru;
(b) uzingatiaji wa misingi ya upigaji kura wa mtu mmoja kura moja; na
(c) uchaguzi huru na wa haki.
(4) Tume Huru ya Uchaguzi inaweza kutekeleza shughuli zake bila kujali kwamba kuna nafasi ya madaraka ya mjumbe iliyo wazi miongoni mwa wajumbe au kwamba Mjumbe yeyote hayupo, lakini kila uamuzi wa Tume Huru ya Uchaguzi ni lazima uungwe mkono na wajumbe walio wengi kati ya idadi ya Wajumbe wote wa Tume Huru ya Uchaguzi.
(5) Katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, Tume Huru ya Uchaguzi haitalazimika kufuata amri, maagizo au maoni ya mtu yeyote, mamlaka yoyote ya Serikali, chama cha siasa, taasisi au asasi yoyote.
(6) Katika kugawa majimbo ya uchaguzi kwa mujibu wa Ibara hii, Tume Huru ya Uchaguzi itazingatia:
(a) idadi ya watu katika eneo husika;
(b) upatikanaji wa njia za mawasiliano katika eneo linalokusudiwa;
(c) mipaka ya kiutawala; na
(d) maeneo ya kijiografia katika eneo husika.
(7) Masharti mengine kuhusu mgawanyo wa Jamhuri ya Muungano katika majimbo wa uchaguzi yatakuwa kama yatakavyofafanuliwa katika sheria itakayotungwa na Bunge.
(8) Katika utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii, Tume Huru ya Uchaguzi itashauriana mara kwa mara na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.
(9) Itakuwa ni marufuku kwa watu wanaohusika na uchaguzi kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba kila mmoja wao atakuwa na haki ya kupiga kura katika uchaguzi au kura ya maoni.
(10) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (7), watu wanaohusika na uchaguzi au kura ya maoni ni:
(a) Mwenyekiti wa Tume;
(b) Makamu Mwenyekiti wa Tume;
(c) Wajumbe wote wa Tume;
(d) Mkurugenzi wa Uchaguzi pamoja na watumishi wote wa Tume; na
(e) wasimamizi wote wa uchaguzi.

Malalamiko kuhusu uchaguzi
221.-(1) Tume Huru ya Uchaguzi itasimamia na kutatua mapema iwezekanavyo malalamiko yanayohusu kuteuliwa kwa mgombea katika uchaguzi.
(2) Kesi za malalamiko kuhusu uchaguzi wa Wabunge zitafunguliwa Mahakama Kuu mapema iwezekanavyo baada ya Tume Huru ya Uchaguzi kutangaza matokeo na kwa vyovyote vile si zaidi ya muda ulioainishwa katika sheria za nchi.
(b) Mkurugenzi wa Uchaguzi

Uteuzi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi
222.-(1) Kutakuwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi atakayeteuliwa na Rais.
(2) Mkurugenzi wa Uchaguzi atakuwa na sifa zifuatazo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa na angalau mmoja kati ya wazazi wake ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) awe ni mtu mwaminifu, mwadilifu, na mwenye mwenendo usiotiliwa shaka na jamii;
(c) awe ni mtu ambaye hajawahi kushika nafasi ya madaraka ya juu katika chama cha siasa;
(d) awe na shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa kwa mujibu wa sheria; na
(e) awe ni mtu ambaye hajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai.
Majukumu ya Mkurugenzi wa Uchaguzi
223.-(1) Mkurugenzi wa Uchaguzi atakuwa ndiye msimamizi na mtekelezaji mkuu wa majukumu ya kila siku ya Tume Huru ya Uchaguzi kuhusiana na masuala ya uchaguzi, uandikishaji wa wapiga kura na uendeshaji wa kura ya maoni.
(2) Mkurugenzi wa Uchaguzi atatekeleza majukumu yake kwa kufuata utaratibu utakaoainishwa na sheria kuhusu masuala ya uchaguzi na kura ya maoni.
(3) Mkurugenzi wa Uchaguzi atatekeleza majukumu yake kwa kusaidiwa na watendaji ambao ni watumishi wa umma kwa kadri itakavyohitajika.
(4) Katika kutekeleza majukumu yake, Mkurugenzi wa Uchaguzi atawajibika kwa Tume Huru ya Uchaguzi.

SEHEMU YA TATU
USAJILI NA USIMAMIZI WA VYAMA VYA SIASA
(a) Vyama vya Siasa
Usajili wa vyama vya siasa
224.-(1) Chama cha siasa kinaweza kufanya shughuli za siasa endapo kitasajiliwa kwa mujibu wa sheria.
(2) Haitakuwa halali kwa chama chochote cha siasa kusajiliwa ambacho kutokana na katiba au sera yake:
(a) kinakusudia kukuza au kupigania maslahi ya:
(i) imani au kundi lolote la dini;
(ii) kundi lolote la kikabila, mahali watu watokeapo, rangi au jinsi;
(iii) eneo fulani tu katika sehemu yoyote ya Jamhuri ya Muungano;
(b) kinapigania kuvunjwa kwa Jamhuri ya Muungano;
(c) kinakubali au kupigania matumizi ya nguvu au mapambano kama njia za kufikia malengo yake ya kisiasa;
(d) kinapigania au kinakusudia kuendesha shughuli zake za kisiasa katika sehemu moja tu ya Jamhuri ya Muungano; au
(e) hakiruhusu uongozi wake kuchaguliwa kwa kuzingatia jinsi, watu wenye ulemavu na uwakilishi wa pande zote mbili za Muungano kwa njia za kidemokrasia.
(3) Bila kuathiri sheria zinazohusika ni marufuku kwa mtu yeyote kulazimishwa kujiunga na chama chochote au kwa chama cha siasa kukataliwa kusajiliwa kwa sababu tu ya itikadi au falsafa.
(4) Bunge linaweza kutunga sheria kuhusu mipaka na vigezo vilivyowekwa na masharti ya ibara ndogo ya (2) kuhusu uhuru na haki ya watu kushirikiana na kujumuika.
(5) Mambo yote yanayohusu uandikishaji na uendeshaji wa vyama vya siasa nchini yatasimamiwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(b) Msajili wa Vyama vya Siasa
Uteuzi wa Msajili wa Vyama vya Siasa
225.-(1) Kutakuwa na Msajili wa Vyama vya Siasa atakayeteuliwa na Rais.
(2) Msajili wa Vyama vya Siasa atakuwa na sifa zifuatazo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) awe ni mwaminifu, mwadilifu na mwenye mwenendo usiotiliwa shaka na jamii;
(c) awe ni mtu ambaye hajawahi kushika nafasi ya madaraka ya juu katika chama cha siasa; na
(d) awe na shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa kwa mujibu wa sheria.
Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa
226.-(1) Kutakuwa na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa atakayeteuliwa na Rais.
(2) Mtu atateuliwa kuwa Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa endapo ana sifa zilizotajwa katika Ibara ya 225(2).
(3) Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa atakuwa ndiye msaidizi mkuu wa Msajili wa Vyama vya Siasa katika kutekeleza majukumu yake.
Wajibu wa Msajili na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa
227.-(1) Msajili na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa watakuwa na wajibu wa:
(a) kusimamia na kuratibu uandikishaji na shughuli za vyama vya siasa kwa mujibu wa masharti ya Katiba na sheria;
(b) kutayarisha na kuchapisha taarifa za kila mwaka kuhusu ripoti za ukaguzi wa fedha kwa kila chama cha siasa; na
(c) kusimamia fedha za vyama vya siasa.
(2) Msajili na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa watatekeleza majukumu yao kwa mujibu wa Katiba hii na kwa kufuata utaratibu utakaoainishwa na sheria itakayotungwa na Bunge.

SURA YA KUMI NA TANO
TAASISI ZA UWAJIBIKAJI

SEHEMU YA KWANZA

TUME YA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA
Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma
228.-(1) Kutakuwa na Tume ambayo itaitwa “Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma” itakayokuwa na Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti na wajumbe wengine wasiozidi saba.
(2) Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma watateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa majina yatakayopendekezwa na Kamati ya Uteuzi.
(3) Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti watashika madaraka baada ya kuapishwa na Rais.
(4) Sifa za Mwenyekiti wa Tume zitakuwa kama ifuatavyo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano ambaye angalau mmoja kati ya wazazi wake ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) mtu mwenye shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambulika kwa mujibu wa sheria;
(c) mtu mwenye uzoefu katika utumishi wa umma kwa kipindi kisichopungua miaka kumi na tano;
(d) mtu mwenye heshima, weledi, uaminifu, uadilifu na asiye na tabia au mwenendo wenye kutiliwa shaka na jamii; na
(e) awe ni mtu ambaye hajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai.
(5) Sifa za Makamu Mwenyekiti zitakuwa kama zilivyoainishwa katika ibara ndogo ya (4).

Uteuzi na sifa za Mjumbe
229.-(1) Mjumbe wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma atateuliwa na Rais baada ya kupendekezwa na Kamati ya Uteuzi.
(2) Sifa za Mjumbe wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma zitakuwa kama ifuatavyo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) mtu mwenye shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambulika kwa mujibu wa sheria;
(c) mtu mwenye uzoefu kwenye uongozi kwa kipindi kisichopungua miaka kumi;
(d) mtu mwenye heshima, weledi, uaminifu, uadilifu na asiye na tabia au mwenendo wenye kutiliwa shaka na jamii; na
(e) awe ni mtu ambaye hajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai.

Kamati ya Uteuzi
230. Kutakuwa na Kamati ya Uteuzi ambayo itakuwa na Wajumbe wafuatao:
(a) Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano;
(b) Jaji Mkuu wa Zanzibar;
(c) Jaji Kiongozi;
(d) Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano; na
(e) Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Majukumu ya Tume
231.-(1) Majukumu ya Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma yatakuwa ni kufuatilia na kuchunguza tabia na mwenendo wa viongozi wa umma kwa madhumuni ya kusimamia na kuhakikisha kuwa maadili na miiko ya uongozi wa umma inazingatiwa, inalindwa na kuheshimiwa katika utumishi wa Serikali, Bunge, Mahakama, taasisi na idara nyingine zote za umma.
(2) Bila kuathiri masharti ya jumla ya ibara ndogo ya (1), majukumu mahsusi ya Tume yatakuwa ni:
(a) kusimamia maadili katika utumishi wa umma;
(b) kuchunguza tabia na mwenendo wa kiongozi wa umma na kuchukua hatua pale inapostahili; na
(c) kusimamia sheria kuhusu maadili ya viongozi wa umma.
(3) Bunge litatunga sheria kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya Ibara hii.
Muda wa Mjumbe wa Tume kushika
232.-(1) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wengine wote kila mmoja atashika madaraka yake kwa kipindi cha miaka mitatu au kipindi kingine cha chini ya miaka mitatu kama itakavyoainishwa katika barua ya uteuzi, ikizingatiwa kwamba uteuzi wa Wajumbe wa Tume utafanywa kwa namna ambayo Wajumbe wa Tume hawataanza au kumaliza muda wao kwa wakati mmoja.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Mjumbe wa Tume anaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine kimoja tu cha miaka mitatu.
(3) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wa Tume wakati watakapokuwa madarakani hawataruhusiwa kuteuliwa, kuchaguliwa au kushika nafasi nyingine yoyote ya madaraka.

Uhuru wa Tume
233.-(1) Tume itakuwa huru na kwa mantiki hiyo, haitaingiliwa na mtu au mamlaka yoyote katika utekelezaji wa majukumu yake.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu:
(a) utaratibu wa utekelezaji wa majukumu ya Tume;
(b) utayarishaji na utoaji wa taarifa za Tume;
(c) utaratibu wa utoaji wa mapendekezo na maamuzi ya Tume;
(d) muda wa kukaa madarakani na kuondolewa madarakani kwa mjumbe wa Tume;
(e) watumishi wa Tume; na
(f) masuala mengine muhimu yanayoihusu Tume.
Uwezeshaji wa nyenzo na rasilimali
234. Serikali itahakikisha kuwa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma inapatiwa fedha, nyenzo na rasilimali watu ili kutekeleza kazi na wajibu wake kwa ufanisi.

SEHEMU YA PILI
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
235.-(1) Kutakuwa na Tume itakayoitwa “Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora” itakayokuwa na Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wasiozidi saba.
(2) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora watateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa majina yaliyopendekezwa na Kamati ya Uteuzi.
(3) Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti watashika madaraka baada ya kuapishwa na Rais.
Sifa za Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Kamishna wa Tume
236.-(1) Sifa za Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora zitakuwa kama ifuatavyo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) mtu mwenye shahada ya sheria kutoka chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na sheria;
(c) mtu mwenye kuheshimu haki za binadamu;
(d) mtu mwenye uzoefu wa utumishi wa umma, upeo mkubwa katika mambo ya haki za binadamu, utawala au mambo ya jamii kwa
kipindi kisichopungua miaka kumi; na
(e) mtu mwenye heshima, weledi, uaminifu, uadilifu na asiye na tabia au mwenendo wenye kutiliwa shaka na jamii.
(2) Sifa za Kamishna wa Tume zitakuwa kama ifuatavyo:
(a) awe ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano na angalau mmoja kati ya wazazi wake ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) mtu mwenye shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na sheria;
(c) mtu mwenye kuheshimu haki za binadamu;
(d) mtu mwenye uzoefu usiopungua miaka kumi ikiwa angalau ana sifa ya masuala ya sheria, haki za binadamu, utawala, siasa au mambo ya jamii; na
(e) mtu mwenye heshima, weledi, uaminifu, uadilifu na asiye na tabia au mwenendo wenye kutiliwa shaka na jamii.

Kamati ya Uteuzi
237.-(1) Kutakuwa na Kamati ya Uteuzi wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora itakayokuwa na wajumbe wafuatao:
(a) Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano ambaye atakuwa ni Mwenyekiti;
(b) Jaji Mkuu wa Zanzibar ambaye atakuwa ni Makamu Mwenyekiti;
(c) Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano;
(d) Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar; na
(e) Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye atakuwa ni Katibu.
(2) Kamati ya Uteuzi itakuwa na jukumu la kupokea na kuchambua majina ya watu walioomba kuwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kwa mujibu wa utaratibu utakaoainishwa na sheria.
(3) Kutakuwa na Sekretarieti ya Tume itakayoongozwa na Katibu Mtendaji atakayeteuliwa na Rais kutokana na orodha ya majina ya watu watatu waliopendekezwa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Kazi na majukumu ya Tume
238.-(1) Kazi na majukumu ya Tume yatakuwa kama ifuatavyo:
(a) kuhamasisha hifadhi ya haki za binadamu na wajibu kwa jamii kwa mujibu wa katiba na sheria;
(b) kuhamasisha, kulinda na kufuatilia utekelezaji wa usawa wa jinsia na ulinganifu kwa ujumla katika maendeleo ya Taifa;
(c) kupokea malalamiko juu ya uvunjaji wa haki za binadamu kwa ujumla;
(d) kuchunguza uvunjaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora na kutoa mapendekezo yatakayowezesha kurekebisha kasoro zilizopo;
(e) kufanya utafiti na kutoa elimu kwa umma kuhusu haki za binadamu na utawala bora;
(f) kufungua mashauri mahakamani ili kuzuia vitendo vya uvunjaji wa haki za binadamu au kurekebisha haki inayotokana na uvunjwaji huo wa haki za binadamu au ukiukwaji wa misingi ya utawala bora;
(g) kuchunguza mwenendo wa mtu yeyote anayehusika au taasisi yoyote inayohusika na masharti ya Ibara hii katika utekelezaji wa kawaida wa madaraka ya kazi au majukumu yake au utekelezaji unaokiuka madaraka hayo;
(h) kutoa ushauri kwa Serikali na vyombo vingine vya umma kuhusu haki za binadamu na utawala bora; na
(i) kuchukua hatua zinazostahiki kwa ajili ya kukuza na kuendeleza usuluhishi miongoni mwa watu na taasisi mbalimbali wanaofika au kufikishwa mbele ya Tume.
(2) Bila kuathiri masharti mengine ya Ibara hii, Bunge laweza kutunga sheria kwa mujibu wa masharti ya Sura hii kwa ajili ya kuweka masharti kuhusu mamlaka ya Tume, utaratibu wa kuendesha shughuli zake na kuhusu kinga za kisheria watakazokuwa nazo Makamishna na watumishi wa Tume kwa makusudi ya kuwawezesha kutekeleza kazi zao bila ya kukiuka sheria.
(3) Kwa madhumuni ya kutekeleza majukumu yake, Tume haitachunguza mambo yafuatayo:
(a) jambo lolote ambalo liko mbele ya mahakama au chombo kingine cha kimahakama;
(b) jambo lolote linalohusu uhusiano au ushirikiano kati ya Serikali na Serikali ya nchi yoyote ya nje au shirika la kimataifa;
(c) jambo linalohusu madaraka ya Rais kutoa msamaha; au
(d) jambo jingine lolote lililotajwa na sheria yoyote.
Muda wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Kamishna wa Tume kushika madaraka
239.-(1) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Kamishna wa Tume kila mmoja atashika madaraka yake kwa kipindi cha miaka mitatu au kipindi kingine cha chini ya miaka mitatu kama itakavyoainishwa katika barua ya uteuzi, ikizingatiwa kwamba uteuzi wa Makamishna wa Tume utafanywa kwa namna ambayo hawataanza au kumaliza muda wao kwa wakati mmoja.
(2) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Kamishna wa Tume anaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine kimoja tu cha miaka mitatu.
(3) Mtu yeyote akiteuliwa kuwa Kamishna wa Tume atalazimika kuacha mara moja madaraka katika chama chochote cha siasa au madaraka ya aina nyingine yoyote yatakayotajwa kwa ajili hiyo na sheria itakayotungwa na Bunge.

Kuondolewa madarakani kwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Kamishna wa Tume
240.-(1) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Kamishna wa Tume anaweza kuondolewa madarakani kwa:
(a) kutokuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa sababu ya maradhi;
(b) kukiuka kanuni za maadili ya viongozi wa umma;
(c) kukiuka Miiko ya Uongozi wa Umma;
(d) kukosa weledi;
(e) utovu wa nidhamu; au
(f) kutiwa hatiani kwa makosa ya jinai yanayohusiana na kukosa maadili au kukosa uaminifu.
(2) Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Kamishna wa Tume hataweza
kuondolewa madarakani isipokuwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) na (4).
(3) Endapo Rais ataridhika kwamba suala la kumuondoa madarakani Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Kamishna wa Tume linahitaji kuchunguzwa, basi Rais ataunda Kamati Maalum itakayochunguza suala hilo.
(4) Kamati Maalum iliyoundwa na Rais itachunguza suala linalohitaji kuchunguzwa na kutoa mapendekezo yake kwa Rais kwa ajili ya uamuzi.

Uhuru wa Tume
241.-(1) Tume itakuwa huru na haitaingiliwa na mtu au mamlaka yoyote katika utekelezaji wa majukumu yake.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu:
(a) utaratibu wa utekelezaji wa majukumu ya Tume;
(b) utayarishaji na utoaji wa taarifa za Tume;
(c) utaratibu wa utoaji wa mapendekezo na maamuzi ya Tume;
(d) watumishi wa Tume; na
(e) masuala mengine muhimu yanayoihusu Tume.
Uwezeshaji wa nyenzo na rasilimali
242. Serikali itahakikisha kuwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inapatiwa fedha, nyenzo na rasilimali watu ili kutekeleza kazi na wajibu wake kwa ufanisi.

SEHEMU YA TATU
MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
Uteuzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
243.-(1) Kutakuwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambaye atateuliwa na Rais.
(2) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atashika nafasi ya madaraka yake baada ya kuapishwa na Rais.
Sifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
244. Mtu anaweza kuteuliwa kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ikiwa ana sifa zifuatazo:
(a) ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano;
(b) amefuzu mafunzo ya juu ya uhasibu na kusajiliwa na mamlaka husika;
(c) ana uzoefu usiopungua miaka kumi na tano katika masuala yanayohusu ukaguzi wa hesabu za Serikali;
(d) ni mtu ambaye hajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai; na
(e) ni mtu mwenye, weledi, uaminifu, uadilifu na asiye na mwenendo unaotiliwa shaka na jamii.
Kazi na majukumu ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
245.-(1) Kazi na majukumu ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali yatakuwa ni:
(a) kuhakikisha kwamba fedha zozote zinazokusudiwa kutolewa kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina matumizi yake yameidhinishwa na kwamba zitatolewa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, na iwapo ataridhika kwamba masharti hayo yatatekelezwa ipasavyo,
basi ataidhinisha fedha hizo zitolewe;
(b) kuhakikisha kwamba fedha zote ambazo matumizi yake yameidhinishwa yatokane na fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina au fedha ambazo matumizi yake yameidhinishwa na sheria, na kwamba zimetumika kwa ajili ya shughuli zilizohusika na matumizi ya fedha hizo na matumizi hayo yamefanywa kwa kufuata idhini iliyotolewa kuhusu matumizi hayo; na
(c) angalau mara moja kila mwaka, kufanya ukaguzi na kutoa taarifa kuhusu:
(i) hesabu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano, hesabu za vyama vya siasa na hesabu za Serikali za Mitaa;
(ii) hesabu zinazosimamiwa na taasisi na wakala wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano;
(iii) hesabu za Mahakama ya Jamhuri ya Muungano; na
(iv) hesabu za Bunge la Jamhuri ya Muungano.
(2) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atakuwa huru katika utekelezaji wa kazi na majukumu yake na hataingiliwa na mtu au mamlaka yoyote katika utekelezaji wa kazi zake.
(3) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali au mtu yeyote aliyeruhusiwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atakuwa na haki ya kuchunguza vitabu, kumbukumbu, hati nyingine zozote zinazohusika na hesabu za aina yoyote iliyotajwa katika ibara ndogo ya (1).
(4) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atawasilisha kwa Rais kila taarifa atakayotoa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(5) Baada ya kupokea taarifa hiyo, Rais atawaagiza watu wanaohusika wawasilishe taarifa hiyo kwenye kikao cha kwanza cha Bunge kitakachofanyika baada ya Rais kupokea taarifa hiyo na itabidi iwasilishwe katika kikao hicho kabla ya kupita siku saba tangu siku ile ulipoanza Mkutano huo, na iwapo Rais hatachukua hatua za kuwasilisha taarifa hiyo kwa Spika, basi Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atawasilisha taarifa hiyo kwa Spika, ambaye atawasilisha taarifa hiyo kwenye Bunge.
(6) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atakuwa pia na jukumu la kutekeleza kazi na shughuli nyingine, na atakuwa na madaraka mengine ya namna mbalimbali, kama itakavyoelezwa na sheria kuhusu hesabu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano, hesabu za vyombo vya umma au hesabu za mashirika.
(7) Katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (1), (3), (4) na (5), Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali hatalazimika kufuata amri au maagizo ya mtu mwingine yeyote au idara yoyote ya Serikali, lakini maelezo hayo ya ibara hii ndogo hayataizuia Mahakama nayo kutumia madaraka yake kwa ajili ya kuchunguza kama Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ametekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au sivyo.
(8) Bunge litatunga sheria itakayosimamia, pamoja na mambo mengine, mamlaka ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Muda wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kushika madaraka
246.-(1) Muda wa kukaa madarakani kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kushika madaraka utakuwa ni kipindi cha miaka saba.
(2) Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (1), Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali anaweza kujiuzulu nafasi ya madaraka yake kwa kutoa taarifa ya siku thelathini kwa Rais.
Kuondolewa madarakani kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
247.-(1) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali anaweza kuondolewa madarakani kwa:
(a) kutokuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa sababu ya maradhi;
(b) kukiuka kanuni za maadili ya uongozi wa umma;
(c) kukiuka miiko ya uongozi wa umma;
(d) kukosa weledi;
(e) utovu wa nidhamu; au
(f) kutiwa hatiani kwa makosa ya jinai yanayohusu kukosa maadili au uaminifu.
(2) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali hataweza kuondolewa madarakani isipokuwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) na (4).
(3) Endapo Rais ataridhika kwamba suala la kumuondoa madarakani Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali linahitaji kuchunguzwa:
(a) atateua Kamati Maalum ambayo itakuwa na Mwenyekiti na wajumbe wengine wasiopungua watatu, mjumbe mmoja kutoka mamlaka ya uhasibu nchini, wajumbe wawili ambao angalau mmoja kati yao awe ni jaji au mtu aliyepata kuwa jaji wa Mahakama ya Juu, Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar;
(b) wakati suala la kumwondoa madarakani Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali limepelekwa kwenye Kamati Maalum kwa ajili ya uchunguzi, Rais atamsimamisha kazi Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali; na
(c) Kamati Maalum itachunguza shauri na kutoa taarifa kwa Rais na itamshauri Rais kama Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali aondolewe madarakani au la.
(4) Endapo Kamati Maalum itamshauri Rais kwamba Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali aondolewe madarakani, basi Rais atamuondoa madarakani.
(5) Rais atafuta uamuzi wa kumsimamisha kazi Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali endapo Kamati Maalum itamshauri Rais kwamba Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali asiondolewe madarakani.
Uwezeshaji wa nyenzo na rasilimali
248. Serikali itaweka utaratibu utakaowezesha Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kupatiwa fedha, nyenzo na rasilimali watu kulingana na uwezo wa kibajeti wa Serikali ili kulinda uhuru wake katika kutekeleza kazi na majukumu yake kwa ufanisi.

SEHEMU YA NNE
CHOMBO CHA KUZUIA NA KUPAMBANA NA RUSHWA
Udhibiti wa rushwa
249.-(1) Kwa madhumuni ya kudhibiti rushwa, kutakuwa na chombo ambacho kitakuwa na jukumu la kuzuia na kupambana na rushwa.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu muundo, majukumu na mamlaka ya chombo kilichorejewa katika ibara ndogo ya (1).

SURA YA KUMI NA SITA
MASHARTI KUHUSU FEDHA ZA JAMHURI YA MUUNGANO
(a) Mfuko Mkuu wa Hazina na Fedha za Jamhuri ya Muungano
Misingi ya matumizi ya fedha za umma
250. Misingi ifuatayo itaongoza matumizi ya fedha za umma katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania:
(a) fedha za umma zitatumika kwa uwazi, umakini na kwa uwajibikaji pamoja na kuzingatia ushiriki wa wananchi kupitia wawakilishi wao;
(b) mfumo wa fedha za umma utalenga kuwepo kwa:
(i) utozwaji kodi usio wa upendeleo au ubaguzi;
(ii) bajeti ya Serikali inayoweka vipaumbele kwa makundi na maeneo yaliyo nyuma kimaendeleo;
(c) matumizi ya rasilimali na mikopo ya Taifa yatazingatia ustawi linganifu kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo; na
(d) taarifa za usimamizi wa fedha za umma zitatolewa katika lugha inayoeleweka kwa wananchi.
Akaunti ya Fedha ya Pamoja
251. Serikali ya Jamhuri ya Muungano itatunza akaunti maalum itakayoitwa “Akaunti ya Fedha ya Pamoja” na ambayo itakuwa ni sehemu ya Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, ambamo kutawekwa fedha yote itakayochangwa na Serikali mbili kwa kiasi kitakachoamuliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge, kwa madhumuni ya shughuli za Jamhuri ya Muungano kwa Mambo ya Muungano.
Tume ya Pamoja ya Fedha
252.-(1) Kutakuwa na Tume ya Pamoja ya Fedha yenye Wajumbe wasiozidi saba watakaoteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kushauriana na Rais wa Zanzibar ambapo wajumbe watatu watatoka Zanzibar na wajumbe wanne watatoka Tanzania Bara.
(2) Majukumu ya Tume ya Pamoja ya Fedha yatakuwa ni:
(a) kuchambua mapato na matumizi yanayotokana na, au yanayohusu utekelezaji wa mambo ya Muungano na kutoa mapendekezo kwa Serikali zote mbili kuhusu mchango na mgawo wa kila mojawapo ya Serikali hizo;
(b) kuchunguza kwa wakati wote mfumo wa shughuli za fedha wa Jamhuri ya Muungano na pia uhusiano katika mambo ya kifedha kati ya Serikali hizo mbili; na
(c) kutekeleza majukumu mengine ambayo Rais ataipatia Tume au kama Rais atakavyoagiza, na kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge.
(3) Kwa madhumuni ya Ibara hii, Bunge litatunga sheria itakayoainisha na kufafanua:
(a) masharti na taratibu za utekelezaji wa majukumu ya Tume ya Pamoja ya Fedha;
(b) masharti kuhusu wajumbe wa Tume ya Pamoja ya Fedha;
(c) muundo na majukumu ya Sekretarieti;
(d) taratibu za uwasilishaji wa taarifa za Akaunti ya Fedha ya Pamoja na taarifa nyingine za Tume ya Pamoja ya Fedha kuhusu utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii; na
(e) mambo mengine yote yanayohusu Tume ya Pamoja ya Fedha.
Mfuko Mkuu wa Hazina
253. Kutakuwa na Mfuko Mkuu wa Hazina wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano utakaoitwa “Mfuko Mkuu wa Hazina” ambamo fedha zote zitakazopatikana kwa njia mbalimbali zitawekwa, isipokuwa:
(a) fedha ambazo zimetajwa katika sheria kuwa zitumike kwa shughuli maalum au ziwekwe katika mfuko mwingine kwa ajili ya matumizi maalum; au
(b) fedha ambazo kwa mujibu wa sheria, taasisi za Serikali zimeruhusiwa kukusanya na kubaki nazo kwa ajili ya kugharamia uendeshaji wa taasisi hizo.
Masharti ya kutoa fedha za matumizi katika Mfuko Mkuu wa Hazina
254.-(1) Fedha zinaweza kutolewa kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina kwa ajili ya matumizi, kwa kuzingatia masharti yafuatayo:
(a) fedha hizo ziwe kwa ajili ya matumizi ambayo yameidhinishwa kuwa yatokane na fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina na idhini hiyo iwe imetolewa kwa mujibu wa Katiba hii au sheria; na
(b) fedha hizo ziwe kwa ajili ya matumizi ambayo yameidhinishwa na sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali itakayotungwa mahsusi na Bunge au sheria nyingine yoyote iliyotungwa na Bunge.
(2) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (1), fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina zitatolewa kutoka Mfuko huo kwa ajili ya matumizi kwa kuzingatia masharti kuwa matumizi hayo yawe yameidhinishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
(3) Fedha zilizomo katika mfuko maalum wowote wa Serikali, isipokuwa Mfuko Mkuu wa Hazina, hazitatolewa kutoka mfuko huo kwa ajili ya matumizi mengine isipokuwa kwa mujibu wa sheria inayoidhinisha matumizi hayo.
Utaratibu wa kuidhinisha matumizi ya fedha zilizomo katika
255.-(1) Rais atatoa maagizo kwa watu wanaohusika watayarishe na kuwasilisha kwenye Bunge, katika kila mwaka wa fedha wa Serikali, makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya kipindi cha mwaka wa fedha wa Serikali unaofuata.

Mfuko Mkuu wa Hazina

(2) Makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano yaliyotayarishwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1), yatawasilishwa kwanza kwenye Kamati husika ya Bunge kwa ajili ya kufanyiwa tathimini na uchambuzi.
(3) Kamati ya Bunge iliyopelekewa makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mujibu wa ibara ndogo ya (2), yaweza kukaribisha na kupokea maoni na ushauri kutoka kwa wadau mbalimbali kuhusu makadirio hayo, na baada ya kukamilisha tathmini na uchambuzi wa mapato na matumizi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Kamati itaandaa taarifa yake kuhusu makadirio ya Serikali na kisha kuiwasilisha Bungeni.
(4) Baada ya Bunge kujadili na kuyakubali makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali yaliyowasilishwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1), Serikali itawasilisha kwenye Bunge muswada wa sheria unaohusu matumizi ya fedha ya Serikali, kwa ajili ya kuidhinisha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina zitakazogharamia shughuli mbalimbali za Serikali zinazohusu makadirio hayo.
(5) Ikiwa katika mwaka wa fedha wowote inaonekana kwamba:
(a) fedha za matumizi zilizoidhinishwa na sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali kwa ajili ya kugharamia shughuli mahsusi hazitoshi;
(b) imekuwa lazima kulipa gharama za shughuli ambayo haikupangiwa fedha za matumizi kwa mujibu wa sheria za nchi;
(c) kuna fedha ambazo zimetumiwa kwa ajili ya shughuli mahsusi kwa kiasi kinachozidi kiwango cha matumizi kilichoidhinishwa na sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali kuhusu shughuli hiyo; au
(d) fedha zimetumiwa kulipia gharama za shughuli ambayo haikupangiwa fedha za matumizi kwa mujibu wa sheria za nchi,
kutawasilishwa kwenye Bunge makadirio ya matumizi ya nyongeza au, kadri itakavyokuwa, maelezo ya matumizi ya ziada, na baada ya Bunge kuyakubali makadirio ya matumizi ya nyongeza au maelezo ya matumizi ya ziada, kutawasilishwa kwenye Bunge muswada wa sheria ya matumizi ya fedha ya Serikali au muswada wa sheria unaohusu matumizi ya nyongeza ya fedha ya Serikali kwa ajili ya kuidhinisha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina, na fedha hizo zitagharamia shughuli zinazohusika na makadirio au maelezo hayo.
Utaratibu wa kuidhinisha matumizi ya fedha kabla ya sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali kuanza kutumika
256.-(1) Iwapo mwaka wa fedha wa Serikali umeanza na sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali inayohusika na mwaka huo haijaanza kutumika, Rais anaweza kuidhinisha fedha zitolewe kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina kwa ajili ya kugharamia shughuli za lazima za Serikali, na fedha hizo zitatumiwa ndani ya miezi minne tangu mwanzo wa mwaka wa fedha wa Serikali au hadi sheria inayohusu matumizi ya fedha ya Serikali itakapoanza kutumika, kutegemea ni lipi kati ya mambo hayo litatangulia kutokea.
(2) Bunge litatunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti ya kuidhinisha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina kwa kufuata utaratibu ulioelezwa katika ibara ndogo ya (1).Mfuko wa Matumizi ya Dharura
257.-(1) Kutakuwa na Mfuko wa Matumizi ya Dharura ambao matumizi yake yatawekewa masharti katika sheria.
(2) Sheria iliyotajwa katika ibara ndogo ya (1) itaruhusu Rais au Waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha, pale anaporidhika kuwa kuna:
(a) jambo la haraka na la dharura na ambalo halikutazamiwa kutokea na ambalo halikupangiwa fedha, kuazima fedha kutoka Mfuko wa Matumizi ya Dharura kwa ajili ya kugharamia jambo hilo; au
(b) jambo la haraka na la dharura kama ilivyoelezwa katika aya ya (a) ya ibara ndogo ya (2), kutumia fedha zilizotengwa mahsusi kwa ajili ya kugharamia shughuli fulani kulipia gharama za jambo hilo.
(3) Iwapo fedha zimeazimwa kutoka Mfuko wa Matumizi ya Dharura au fedha zilizotengwa mahsusi kwa ajili ya shughuli fulani zimetumiwa kugharamia jambo la haraka na la dharura, basi kutawasilishwa kwenye Bunge makadirio ya matumizi ya nyongeza, na baada ya Bunge kuyakubali makadirio hayo muswada wa sheria unaohusu matumizi ya fedha za Serikali utakaowasilishwa kwenye Bunge kwa ajili ya kuidhinisha matumizi hayo utahakikisha kwamba fedha zozote zilizoazimwa kwenye Mfuko wa Matumizi ya Dharura zitarudishwa kwenye Mfuko huo kutoka katika fedha za matumizi yatakayoidhinishwa na muswada huo.
Mishahara ya baadhi ya watumishi kudhaminiwa na Mfuko Mkuu wa Hazina
258.-(1) Kutakuwa na watumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambao watalipwa mishahara na posho kama itakavyoelezwa na sheria.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), fedha za malipo ya mishahara na posho za watumishi wa Serikali wanaohusika na masharti ya Ibara hii pamoja na fedha za malipo ya uzeeni na kiinua mgongo, zitatolewa kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina.
(3) Mshahara anaolipwa mtumishi wa Serikali anayehusika na masharti ya Ibara hii pamoja na masharti yake ya kazi havitabadilishwa kwa jinsi ambayo itapunguza maslahi ya mtumishi huyo baada ya kuteuliwa, isipokuwa kwamba masharti haya hayahusiki na posho anayolipwa mtumishi huyo.
(4) Endapo mtumishi wa Serikali anayehusika na masharti ya Ibara hii ana hiyari ya kuchagua kima cha mshahara au aina ya masharti ya kazi, basi kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya ibara ndogo ya (3), mshahara wa kima hicho atakaochagua na aina hiyo ya masharti ya kazi atakayochagua vitahesabiwa kuwa vina maslahi zaidi kwake kuliko kima cha mshahara kingine chochote ambacho anaweza kuchagua au aina ya masharti ya kazi nyingine yoyote ambayo angeweza kuchagua.
(5) Masharti ya Ibara hii yatatumika kwa Jaji wa Mahakama ya Juu, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano, Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na
watumishi wengine watakaoainishwa katika sheria za nchi.
(b) Deni la Taifa na Mikopo ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano

Deni la Taifa
259.-(1) Deni la Taifa litadhaminiwa na Mfuko Mkuu wa Hazina.
(2) Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa Ibara hii, deni la Taifa litajumuisha deni la Serikali ya Jamhuri ya Muungano pamoja na deni lolote litakalodhaminiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kukopa
260.-(1) Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na mamlaka ya kukopa fedha ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya kugharamia shughuli zilizo chini ya mamlaka yake.
(2) Bunge linaweza kutunga sheria ambayo:
(a) itaweka masharti ya kuzingatiwa na Serikali wakati wa kukopa;
(b) itaweka ukomo wa deni la Taifa na madhumuni ya deni hilo; na
(c) itaweka utaratibu wa Serikali kutoa taarifa kwenye Bunge kuhusu mikopo na deni la Taifa.
(3) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (2)(b), taarifa itakayowasilishwa Bungeni pamoja na mambo mengine itaeleza:
(a) kiasi cha deni lililopo na riba yake;
(b) matumizi yaliyofanywa au yatakayofanywa kutokana na fedha za mkopo husika;
(c) utaratibu uliowekwa wa kulipa deni husika; na
(d) hatua iliyofikiwa katika kulipa deni husika.
Mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kukopa
261.-(1) Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa na mamlaka ya kukopa fedha ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya kugharamia shughuli zilizo chini ya mamlaka yake.
(2) Endapo mkopo utahitaji dhamana, Serikali ya Jamhuri ya Muungano, baada ya kushauriana na kukubaliana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, itatoa dhamana kwa mkopo unaoombwa.
(3) Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 76, Bunge litatunga sheria itakayoweka utaratibu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kudhamini mikopo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Mamlaka ya kutoza kodi
262.-(1) Mamlaka ya kutoza kodi kwa mambo yote ya Muungano na kwa mambo yasiyo ya Muungano yanayoihusu Tanzania Bara yatakuwa chini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Mamlaka ya kutoza kodi kwa mambo yote yasiyo ya Muungano yanayoihusu Zanzibar yatakuwa chini ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
(3) Hakuna kodi ya aina yoyote itakayotozwa katika Jamhuri ya Muungano isipokuwa kwa mujibu wa sheria.

Ununuzi wa umma
263.-(1) Katika kufanya ununuzi wa umma, Serikali na taasisi zote za umma zitatakiwa kutumia mfumo na utaratibu utakaozingatia haki, uwazi, maslahi ya umma, uwajibikaji, ushindani na thamani halisi ya fedha.
(2) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti ya usimamizi na udhibiti wa manunuzi ya Serikali na taasisi zake ambayo itazingatia misingi ifuatayo:
(a) kununua bidhaa zinazozalishwa na huduma zinazotolewa nchini;
(b) makundi ambayo yatapewa kipaumbele katika utoaji wa mikataba;
(c) kuwapa fursa maalum watu au makundi yalioathiriwa na ushindani usio wa haki;
(d) adhabu kwa mkandarasi ambaye amefanya kazi chini ya kiwango na kukiuka taratibu za kitaaluma, mkataba husika au sheria; na
(e) adhabu kwa mtu aliyekwepa kulipa kodi au aliyehukumiwa kwa matendo au makosa ya rushwa au makosa makubwa ya kukiuka sheria na taratibu za kazi.
Benki Kuu ya Jamhuri ya Muungano
264.-(1) Kutakuwa na Benki Kuu ya Jamhuri ya Muungano itakayoitwa “Benki Kuu ya Tanzania”.
(2) Benki Kuu ya Tanzania itakuwa na majukumu yafuatayo:
(a) kutoa sarafu;
(b) kudhibiti na kusimamia mzunguko wa sarafu;
(c) kuandaa na kusimamia sera na mipango inayohusiana na sarafu;
(d) kudhibiti na kusimamia masuala ya fedha za kigeni;
(e) kusimamia benki za biashara na taasisi zote za fedha ndani ya Jamhuri ya Muungano; na
(f) kutunza akaunti ya fedha za Serikali.
(3) Katika utekelezaji wa majukumu yake, Benki Kuu ya Tanzania itakuwa huru na haitaingiliwa ama kwa kupewa maelekezo au kudhibitiwa na mtu au mamlaka yoyote.
(4) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu muundo, mamlaka, shughuli na utendaji wa Benki Kuu ya Tanzania.

SURA YA KUMI NA SABA
ULINZI NA USALAMA WA JAMHURI YA MUUNGANO
(a) Ulinzi na Usalama wa Taifa
Usalama wa Taifa
265.-(1) Jukumu la ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano ni la kila raia.
(2) Usalama wa Jamhuri ya Muungano unahusu ulinzi wa mipaka yote ya eneo la Jamhuri ya Muungano kama ilivyoanishwa katika Ibara ya 2 ikiwa ni pamoja na ardhi, anga, mito, maziwa, visiwa na bahari kuu, watu wake, mali zao, haki, uhuru na maslahi mengine ya kitaifa dhidi ya vitisho vya ndani na nje ya nchi.
(3) Ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano utaimarishwa kulingana na kanuni zifuatazo:
(a) ulinzi na usalama wa Taifa unaongozwa kwa mamlaka ya Katiba hii; na
(b) ulinzi na usalama wa Taifa utatekelezwa kwa kuzingatia sheria za nchi na za kimataifa, na kwa kuheshimu utawala wa sheria na haki za binadamu.

Vyombo vya Ulinzi na Usalama wa Taifa
266.-(1) Vyombo vya ulinzi na usalama wa Taifa vitakuwa ni:
(a) Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania;
(b) Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Muungano; na
(c) Idara ya Usalama wa Taifa.
(2) Wajibu wa vyombo vya ulinzi na usalama wa Taifa na mfumo wa usalama ni kulinda mipaka ya Jamhuri ya Muungano, rasilimali za nchi, maslahi ya raia na watu wengine, mali zao, haki na uhuru, mamlaka ya nchi, amani na umoja wa kitaifa.
(3) Katika utekelezaji wa majukumu yao, vyombo vya ulinzi na usalama wa Taifa na kila mtumishi wa vyombo hivyo hataruhusiwa:
(a) kuwa na upendeleo kwa njia yoyote;
(b) kujiunga na chama chochote cha siasa au kuendeleza maslahi ya chama chochote cha siasa au sera zake;
(c) kuhujumu maslahi ya kisiasa au mpango wa kisiasa ambao ni halali chini ya Katiba hii;
(d) kutishia, kudhulumu au kuwatendea ukatili raia na watu wengine; na
(e) kutii amri yoyote isiyokuwa halali.
(4) Mtu hataruhusiwa kuanzisha taasisi, kampuni, jumuiya au shirika linalohusiana na ulinzi na usalama wa Taifa au ushirika wa kijeshi, isipokuwa kama inavyoruhusiwa na Katiba hii au sheria.
(5) Vyombo vya ulinzi na usalama wa Taifa vitakuwa chini ya mamlaka ya Amiri Jeshi Mkuu.
(6) Bunge litatunga sheria kuweka masharti kuhusu utekelezaji wa majukumu, uratibu na usimamizi wa vyombo vya ulinzi na usalama wa Taifa.
Baraza la Usalama la Taifa
267.-(1) Kutakuwa na Baraza la Usalama la Taifa litakalokuwa na wajumbe wafuatao:
(a) Rais ambaye atakuwa ni Mwenyekiti;
(b) Makamu wa Kwanza wa Rais;
(c) Rais wa Zanzibar na Makamu wa Pili wa Rais;
(d) Waziri Mkuu na Makamu wa Tatu wa Rais.
(2) Mwenyekiti anaweza kumualika mtu yeyote kushiriki katika kikao cha Baraza la Usalama la Taifa.
(3) Kutakuwa na Sekretarieti ya Baraza la Usalama la Taifa itakayoongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi.
(4) Baraza la Usalama la Taifa litaweka utaratibu wa mwenendo wa vikao vyake.
(5) Bunge litatunga sheria itakayoweka masharti kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Baraza la Usalama la Taifa.
Majukumu ya Baraza la Usalama la Taifa
268. Baraza la Usalama la Taifa litakuwa na majukumu yafuatayo:
(a) kuunganisha sera za ndani, sera za nchi za nje na za kijeshi kuhusiana na usalama wa Taifa ili kuwezesha taasisi za ulinzi na usalama wa Taifa kushirikiana kikamilifu;
(b) kupokea na kutathmini taarifa kutoka katika vyombo vya ulinzi na Usalama wa Taifa na taasisi za Serikali kuhusiana na usalama wa nchi;
(c) kutekeleza majukumu mengine yoyote kama Rais atakavyoagiza.
(b) Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
Kuanzishwa kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
269.-(1) Kutakuwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania litakalokuwa na jukumu la kulinda uhuru na mipaka ya Jamhuri ya Muungano na kusimamia ulinzi na usalama wa wananchi.
(2) Rais anaweza kuanzisha vikosi vingine vya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kama atakavyoona inafaa.
Uteuzi wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi
270.-(1) Kutakuwa na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ambaye atakuwa raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano na atakayeteuliwa na Rais.
(2) Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi atatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi.
Madaraka ya Amiri Jeshi Mkuu
271.-(1) Bila kuathiri masharti yatakayowekwa na sheria, Rais kwa nafasi ya madaraka ya Amiri Jeshi Mkuu atakuwa na mamlaka ya kuyaamuru majeshi ya nchi:
(a) kutenda mambo yanayohusika na vita vya ulinzi wa Jamhuri ya Muungano;
(b) kuokoa maisha na mali za watu wakati wa hali ya hatari;
(c) kutoa msaada kwa jamii wakati wa dharura au majanga; na
(d) kutenda mambo mengineyo ambayo Amiri Jeshi Mkuu ataona yanahitajika,
na kwa ajili hiyo Amiri Jeshi Mkuu anaweza kuyaamuru majeshi hayo yatekeleze mambo hayo ndani au nje ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Katika utekelezaji wa masharti ya Ibara hii na kwa kuzingatia sheria, madaraka juu ya mambo yafuatayo yatakuwa mikononi mwa Amiri Jeshi Mkuu:
(a) kuwateua viongozi katika majeshi ya ulinzi ya Jamhuri ya Muungano;
(b) kuwatunuku kamisheni maafisa katika majeshi ya ulinzi;
(c) kuwateua wanajeshi watakaoongoza vikosi mbali mbali vya majeshi ya ulinzi;
(d) kumwamuru mwanajeshi yeyote asitumie madaraka yoyote aliyokabidhiwa na ambayo yanaambatana na kuwa kwake mwanajeshi; na
(e) kulinda uhuru na mipaka ya Jamhuri ya Muungano.
(3) Kwa madhumuni ya Ibara hii, jambo lolote atakalotenda mwanajeshi kinyume cha amri ya Amiri Jeshi Mkuu litakuwa batili.
(c) Jeshi la Polisi
Jeshi la Polisi la Jamhuri ya
272. Kutakuwa na Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Muungano litakalokuwa na jukumu la ulinzi na usalama wa watu na mali zao kwa mujibu wa masharti ya Muungano

Katiba hii.
Uteuzi wa Mkuu wa Jeshi la Polisi
273.-(1) Kutakuwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Muungano ambaye atakuwa raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano na atakayeteuliwa na Rais.
(2) Mkuu wa Jeshi la Polisi atatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi.
Uanzishwaji wa huduma nyingine za ulinzi
274. Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 266, Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti yatakayoruhusu kuanzisha, kudhibiti na kusimamia taasisi nyingine zinazotoa huduma za ulinzi.
(d) Idara ya Usalama wa Taifa ya Jamhuri ya Muungano
Kuanzishwa kwa Idara ya Usalama wa Taifa
275.-(1) Kutakuwa na Idara ya Usalama wa Taifa ya Jamhuri ya Muungano itakayoitwa “Idara ya Usalama wa Taifa”.
(2) Idara ya Usalama wa Taifa itahusika na shughuli za kuimarisha usalama wa Jamhuri ya Muungano na kulinda maslahi ya Taifa na ya watu wake na itatekeleza majukumu mengine kama yatakavyoainishwa na sheria.
Uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa
276.-(1) Kutakuwa na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa ambaye atakuwa raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano na atakayeteuliwa na Rais.
(2) Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa atatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi.

SURA YA KUMI NA NANE
MENGINEYO
Utaratibu wa kujiuzulu katika utumishi wa umma
277.-(1) Mtu yeyote mwenye dhamana ya kazi yoyote iliyoanzishwa na Katiba hii anaweza kujiuzulu kwa kutoa taarifa iliyoandikwa na kutiwa saini kwa mkono wake, kwa kufuata masharti yafuatayo:
(a) iwapo mtu huyo aliteuliwa au kuchaguliwa na mtu mmoja, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa mtu huyo aliyemteua au aliyemchagua, au iwapo aliteuliwa au kuchaguliwa na kikao cha watu, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwenye kikao hicho;
(b) iwapo mtu huyo ni Rais, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa Spika;
(c) iwapo mtu huyo ni Makamu wa Kwanza wa Rais, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa Rais;
(d) iwapo mtu huyo ni “Waziri Mkuu”, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa Rais na nakala kwa Spika; na
(e) iwapo mtu huyo ni Spika au Naibu Spika wa Bunge, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa Katibu wa Bunge.
98
(2) Mtu aliyetoa taarifa ya kujiuzulu kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (1), atahesabiwa kuwa amejiuzulu tangu siku ambayo taarifa yake ya kujiuzulu itakapopokelewa na mtu anayehusika au kikao kinachohusika au itakapopokelewa na mtu yeyote aliyeruhusiwa kuipokea taarifa hiyo na mtu anayehusika au kikao kinachohusika:
Isipokuwa kama taarifa hiyo ya kujiuzulu imeeleza kwamba mtu huyo atajiuzulu siku nyingine baada ya taarifa hiyo kupokelewa na mtu anayehusika au kikao kinachohusika, basi mtu huyo atahesabiwa kuwa amejiuzulu tangu siku hiyo nyingine iliyotajwa.
(3) Endapo mtu yeyote mwenye dhamana ya kazi yoyote iliyoanzishwa na Katiba hii amejiuzulu, ikiwa anazo sifa zote zinazohitajika na kwa kila hali anastahili, anaweza kuteuliwa au kuchaguliwa tena kushika madaraka ya kazi hiyo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
Masharti kuhusu kukabidhi madaraka
278.-(1) Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya Katiba hii kuhusu utaratibu wa kukabidhi madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, mtu yeyote mwenye mamlaka, kwa mujibu wa Katiba hii, ya kumteua mtu mwingine kushika madaraka, mtu huyo atakuwa na uwezo wa kumteua kaimu au mtu ambaye atashika kwa muda na kutekeleza madaraka hayo.
(2) Kanuni zifuatazo zitatumika pia kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya Katiba hii kuhusu utaratibu wa kukabidhi madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano:
(a) iwapo kuna mtu mwenye madaraka aliyokabidhiwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na mtu huyo yupo likizo na wakati huo huo anasubiri kuacha madaraka hayo, basi anaweza kuteuliwa mtu mwingine na kukabidhiwa madaraka hayo, bila ya kujali kuwepo kwa yule mtu anayesubiri kuacha madaraka hayo;
(b) iwapo kuna watu wawili au zaidi ambao kwa wakati mmoja wote wanashika madaraka kutokana na uteuzi wao uliofanywa kwa mujibu wa Kanuni iliyoelezwa katika aya ya (a), basi katika hali hiyo kukitokea umuhimu wa kutekeleza shughuli yoyote inayohusika na madaraka hayo yule mtu wa mwisho kuteuliwa ndiye atakayehesabiwa kuwa mtu pekee mwenye dhamana ya madaraka hayo; na
(c) iwapo mtu ameteuliwa, kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, kuwa kaimu au kushikilia madaraka wakati mtu aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka hayo ameshindwa kutekeleza shughuli zinazohusika na madaraka hayo, basi haitaruhusiwa kufanya uchunguzi wowote au kutoa hoja yoyote juu ya uteuzi wa huyo kaimu kwa sababu mtu aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka hayo ameshindwa kutelekeza shughuli zinazohusika na madaraka hayo.
Ufafanuzi
279.-(1) Katika Katiba hii, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo:
“amri ya jeshi” maana yake ni sheria au amri iliyotolewa kwa mujibu wa sheria ya kusimamia nidhamu katika Jeshi;
“Baraza la Wawakilishi” maana yake ni Baraza la Wawakilishi la Zanzibar lililotajwa na Katiba hii;
“Bunge” maana yake ni Bunge la Jamhuri ya Muungano lililotajwa kwa mujibu wa Ibara ya 129;
“chama cha siasa” maana yake ni chama cha siasa kilichosajiliwa kwa mujibu wa sheria inayohusu vyama vya siasa;
“Idara ya Usalama wa Taifa” maana yake ni Idara ya Usalama wa Taifa iliyoundwa kwa mujibu wa Ibara 275;
“Jaji Kiongozi” maana yake ni Jaji wa Mahakama Kuu ambaye ameteuliwa kwa mujibu wa Ibara ya 194;
“Jaji Mkuu” maana yake ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano ambaye ameteuliwa kwa mujibu wa Ibara ya 175 na ndiye Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano;
“Jaji Mkuu wa Zanzibar” maana yake ni Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Zanzibar ambaye kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya 1984 ndiye mkuu wa Mahakama ya Zanzibar;
“Jamhuri ya Muungano” maana yake ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
“Jeshi” maana yake ni jeshi lolote kati ya majeshi ya ulinzi na ni pamoja na jeshi lolote jingine lililoundwa na Katiba hii au kwa mujibu wa sheria na linalotawaliwa kwa amri ya jeshi;
“Jeshi la Polisi” maana yake ni Jeshi la Polisi lililoundwa kwa mujibu wa Ibara 272;
“kiapo” maana yake ni tamko rasmi la namna yoyote linaloruhusiwa kutumiwa kisheria;
“kiapo cha uaminifu” maana yake ni kiapo cha kuwa mwaminifu kwa nchi na kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano;
“Mahakama” maana yake ni Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar, kwa kadri itakavyokuwa;
“Makamu wa Rais” maana yake ni mtu yeyote aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Rais kwa mujibu wa Katiba hii;
“Mambo ya Muungano” maana yake ni mambo yote ambayo yametajwa katika Nyongeza ya Kwanza ya Katiba hii kuwa ni Mambo ya Muungano;
“Mamlaka ya nchi” maana yake ni mamlaka ya nchi iliyotajwa katika Ibara ya 74;
“Mkurugenzi wa Mashtaka” maana yake ni mtu aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya Mkurugenzi wa Mashtaka kwa mujibu wa Ibara ya 120;
“mtumishi wa umma” maana yake ni mtu aliyeajiriwa katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kama itakavyofafanuliwa na sheria itakayotungwa na Bunge;
“Mwanasheria Mkuu” maana yake ni mtu yeyote aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Ibara ya 118;
“nafasi ya madaraka” maana yake ni wadhifa, cheo, hadhi, madaraka ya uongozi au mamlaka ya utendaji katika utumishi wa umma;
“Naibu Jaji Mkuu” maana yake ni mtu ambaye ameteuliwa kushika nafasi ya madaraka kuwa Naibu Jaji Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 176;
“Naibu Mwanasheria Mkuu” maana yake ni mtu yeyote aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya Naibu Mwanasheria Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 119;
“Serikali” maana yake ni pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar au Halmashauri ya Wilaya au ya Mji na pia mtu yeyote anayetekeleza madaraka au mamlaka yoyote kwa niaba ya Serikali;
“Serikali za Mitaa” maana yake ni Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizoanzishwa kwa mujibu wa Ibara ya 124;
“Tanzania Bara” maana yake ni eneo la Jamhuri ya Muungano ambalo kabla ya Muungano wa mwaka 1964 lilikuwa eneo la Jamhuri ya Tanganyika;
“Tanzania Zanzibar” maana yake ni eneo la Jamhuri ya Muungano ambalo kabla ya Muungano wa mwaka 1964, lilikuwa eneo la Jamhuri ya Watu wa Zanzibar;
“Uchaguzi Mkuu” maana yake ni uchaguzi wa Rais na uchaguzi wa Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi utakaofanywa kwa mujibu wa Katiba hii;
“Waziri” maana yake ni mtu yeyote aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya Waziri na wadhifa wa “Naibu Waziri” utatafsiriwa kwa muktadha huo;
“Waziri Mkuu” maana yake ni mtu yeyote aliyeteuliwa kushika nafasi ya madaraka ya Waziri Mkuu kwa mujibu wa Katiba hii;
“Zanzibar” maana yake ni sawa na maana ya Tanzania Zanzibar.
(2) Kanuni zifuatazo zitatumika kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya Katiba hii:
(a) kila yanapotajwa madaraka ya Rais, ifahamike kuwa madaraka yanayohusika ni pamoja na mamlaka ya kutekeleza shughuli za kazi mbalimbali na vile vile wajibu wa kutekeleza shughuli na kazi mbali mbali kama Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu na pia mamlaka mengine kama hayo au wajibu mwingine kama huo ikiwa imeelezwa katika Katiba hii au katika sheria nyingine yoyote kwamba mamlaka hayo mengine ni ya Rais au kwamba wajibu huo mwingine ni wa Rais;
(b) kila yanapotajwa madaraka ya kazi katika utumishi wa Serikali, ifahamike kuwa kazi inayohusika ni kazi katika Utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Mungano isipokuwa kama imeelezwa vinginevyo, na kila inapotajwa Idara ya Serikali ifahamike kuwa idara inayohusika ni idara ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, isipokuwa kama imeelezwa vinginevyo;
(c) iwapo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii kuna jambo lolote linalotakiwa litekelezwe au lishughulikiwe na chama chochote cha siasa, basi, jambo hilo litatekelezwa au litashughulikiwa na chama hicho kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa na chama hicho kwa ajili hiyo, na pia kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii au sheria ya nchi iliyotungwa kwa ajili hiyo;
(d) mtu hatahesabiwa kuwa ana madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa sababu tu kwamba anapokea malipo ya uzeeni au malipo mengine ya aina hiyo kwa ajili ya utumishi wake wa zamani katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Muungano na Idara ya Usalama wa Taifa:
Isipokuwa kama muktadha utaelekeza vinginevyo, kila anapotajwa mtu mwenye dhamana ya madaraka kwa kutaja madaraka yake, mtu anayehusika atakuwa ni pamoja na mtu yeyote ambaye ni kaimu au aliyeteuliwa kihalali kushikilia dhamana ya madaraka hayo;
(e) kila yalipotajwa mamlaka ya kumwondoa mtu katika nafasi ya madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, mamlaka yanayohusika ni pamoja na mamlaka yaliyotolewa kwa mujibu wa masharti ya sheria yoyote yanayomtaka mtu huyo au yanayomruhusu mtu huyo kustaafu:
Isipokuwa kwamba masharti haya hayatamhusu Jaji wa Mahakama ya Juu, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali; na
(f) kila ilipotajwa sheria ambayo inabadilisha au kufuta sheria nyingine, ifahamike kuwa sheria inayohusika ni pamoja na sheria ambayo inarekebisha sheria hiyo nyingine au ambayo inaendeleza kutumika kwa hiyo sheria nyingine, ama bila mabadiliko au baada ya kubadilishwa au kurekebishwa; au sheria ambayo inaweka masharti mapya katika sheria nyingine.
Jina la Katiba, kuanza kutumika na matumizi
280.-(1) Katiba hii itaitwa “Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014”.
(2) Katiba hii itaanza kutumika tarehe itakayozinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
(3) Katiba hii itatumika Tanzania Bara na Zanzibar.
Kufutwa kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977
Sura ya 2
281. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 inafutwa na, isipokuwa kwa masuala yaliyoelekezwa katika Masharti Yatokanayo na Masharti ya Mpito, haitakuwa na nguvu ya kisheria mara baada ya kuanza kutumika kwa Katiba hii.

SURA YA KUMI NA TISA
MASHARTI YATOKANAYO NA MASHARTI YA MPITO
SEHEMU YA KWANZA
MASHARTI YATOKANAYO
Matumizi ya baadhi ya masharti ya Katiba
Sura ya 2
282.-(1) Masharti Yatokanayo na Masharti ya Mpito yaliyoainishwa katika Sura hii ya Katiba yataanza kutumika tarehe ambayo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014 itakapoanza kutumika.
(2) Kwa kuondoa shaka, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 itakuwa imefutwa na, isipokuwa kwa masuala yaliyoainishwa katika Sehemu ya Pili ya Sura hii, haitakuwa na nguvu ya sheria kuanzia tarehe ya kuanza kutumika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014.

SEHEMU YA PILI
MASHARTI YA KIKATIBA NA SHERIA ZA NCHI
Kuendelea kutumika kwa masharti ya Katiba
283.-(1) Masharti Yatokanayo na Masharti ya Mpito katika Sura hii ya Katiba na yale yaliyowekwa katika Mabadiliko ya “Sheria Maalum” ambayo bado yanaendelea kutumika katika Katiba zilizoainishwa katika Ibara hii, yataendelea kutumika.
(2) Kwa madhumuni ya Ibara hii, “Sheria Maalum” maana yake ni:
(a) the Republic of Tanganyika (Consequential, Transitional and Temporary Provisions) Act, 1962;
(b) the Interim Constitution (Consequential, Transition and Temporary Provisions) Act, 1965;
(c) the Constitution (Consequential, Transitional and Temporary Provisions) Act, 1977;
(d) the Constitution (Consequential, Transitional and Temporary Provisions) Act, 1984; na
(e) the Constitution (Consequential, Transitional and Temporary Provisions) Act, 1992.
Kuendelea kutumika kwa sheria za nchi
284.-(1) Masharti ya sheria zilizoainishwa katika ibara ndogo ya (2) na ambazo zimekuwa zinatumika kabla ya tarehe ya kuanza kutumika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014, zitaendelea kutumika kwa namna ambayo imeelekezwa katika Ibara hii.
(2) Sheria za nchi ambazo:
(a) zimetungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano kabla ya kuanza kutumika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014 zitaendelea kutumika kwa madhumuni ya masuala yaliyoelekezwa katika sheria hizo; na
(b) zimetungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano ambazo zinatumika Tanzania Bara zitaendelea kutumika Tanzania Bara kwa madhumuni ya masuala yaliyoelekezwa katika sheria hizo.
(3) Kwa madhumuni ya masharti ya ibara ndogo ya (2), wakati na baada ya Muda wa Mpito:
(a) sheria zote zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano ambazo zinatumika Tanzania Bara na Zanzibar na kwa kuzingatia marekebisho yatakayohitajika, zitakuwa sheria za nchi ambazo zitatumika katika Jamhuri ya Muungano kwa Mambo ya Muungano;
(b) kwa kuzingatia mgawanyo wa Mambo ya Muungano na mambo yasiyo ya Muungano yaliyoelekezwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014, sheria zote zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano ambazo zinatumika Tanzania Bara na Zanzibar, kwa kuzingatia marekebisho yatakayohitajika, zitatumika Tanzania Bara au Zanzibar kwa Mambo yasiyo ya Muungano hadi hapo Tanzania Bara au Zanzibar itakapotunga sheria kuhusu mambo hayo; na
(c) sheria zote zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano ambazo zinatumika Tanzania Bara na kwa kuzingatia marekebisho yatakayohitajika, zitakuwa sheria ambazo zitatumika Tanzania Bara.

SEHEMU YA TATU
UTUMISHI WA UMMA
Serikali ya Jamhuri ya Muungano
Kuendelea kuwepo kwa Rais madarakani
285. Mtu aliyekuwa anashika nafasi ya madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano kabla ya kuanza kutumika kwa Katiba hii, ataendelea kushika nafasi ya madaraka ya Rais kwa masharti ya Katiba hii hadi mtu mwingine atakapochaguliwa badala yake katika Uchaguzi Mkuu wa kushika nafasi ya madaraka ya Rais kwa mujibu wa Katiba hii.
Kuendelea kuwepo kwa Makamu wa Rais madarakani
286. Mtu aliyekuwa anashika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kabla ya kuanza kutumika kwa Katiba hii, ataendelea kushika nafasi ya madaraka ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa masharti ya Katiba hii hadi Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano atakapochaguliwa badala yake katika Uchaguzi Mkuu.
Kuendelea kwa Waziri Mkuu, Mawaziri na Naibu Mawaziri
287.-(1) Mtu anayeshika nafasi ya Waziri Mkuu ataendelea kuwa katika nafasi ya madaraka ya Waziri Mkuu hadi Uchaguzi Mkuu utakapofanyika, na Rais mteule wa Jamhuri ya Muungano ameapishwa kushika madaraka.
(2) Mtu anayeshika nafasi ya madaraka ya Waziri au Naibu Waziri ataendelea kushika nafasi hiyo ya madaraka hadi Uchaguzi Mkuu utakapofanyika na nafasi hiyo ya madaraka itakoma saa ishirini na nne kabla ya Rais mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuapishwa kushika nafasi ya madaraka ya Rais.
(3) Masharti ya ibara ndogo ya (1) na (2), hayatatafsiriwa kwamba yanaondoa au kufifisha madaraka aliyonayo Rais kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 au sheria za nchi kufuta nafasi ya madaraka ya kumvua madaraka au kumwachisha kazi mtu anayeshika au kukaimu nafasi ya madaraka au kumwachisha kazi mtu anayeshika au kukaimu nafasi ya madaraka ya Waziri Mkuu, Waziri au Naibu Waziri kujiuzulu.
Kuendelea kwa utumishi wa umma
288.-(1) Kila mtu aliyeshika au kukaimu nafasi ya madaraka ya utumishi wa umma katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Bunge la Jamhuri ya Muungano au Mahakama ya Jamhuri ya Muungano kabla ya tarehe ya kuanza kutumika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014, ataendelea na atatambuliwa kuwa amechaguliwa, kuteuliwa au kuajiriwa kushika au kukaimu nafasi ya madaraka ya utumishi wa umma katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Bunge la Jamhuri ya Muungano au Mahakama ya Jamhuri ya Muungano na kwamba masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 2014 au sheria za nchi kuhusiana na kuchaguliwa, uteuzi, ajira na kula kiapo au yamini yamezingatiwa na kutekelezwa.
Sura ya 2
(2) Kila mtu ambaye kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 au sheria za nchi, atahitajika kuondoka katika nafasi ya madaraka baada ya muda maalum kupita au atakapotimiza umri wa kustaafu, ataacha kushika nafasi ya madaraka katika utumishi wa umma baada ya kufika mwisho wa muda huo maalum au atakapofika umri wa kustaafu.
(3) Masharti ya ibara ndogo ya (1) na (2), hayatatafsiriwa kwamba yanaondoa au kufifisha madaraka aliyonayo mtu au yaliyowekwa kwa mamlaka kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 au sheria za nchi kufuta nafasi ya madaraka na kumvua madaraka au kumwachisha kazi mtu anayeshika au kukaimu nafasi ya madaraka au kumtaka mtumishi wa umma kujiuzulu.
(4) Kwa madhumuni ya malipo ya kiinua mgongo au malipo mengine ya uzeeni, muda wa utumishi wa mtumishi wa umma anayehusika na masharti ya Ibara hii, utahesabika kuwa ni pamoja na muda wa utumishi aliokuwa nao kabla ya kuanza kutumika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014.
(5) Isipokuwa kama itaelekezwa vinginevyo, masharti ya kazi ya mtumishi wa umma ambaye masharti ya Ibara hii yanamhusu hayatakuwa duni au hafifu ukiliganisha na masharti ya kazi aliyokuwa nayo kabla ya kuanza kutumika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014 au sheria za nchi zitakazotungwa kwa ajili hiyo.

SEHEMU YA NNE
BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO
Kuendelea kwa Ubunge na Uongozi wa Bunge
289.-(1) Kwa kuzingatia masharti ya ibara ndogo ya (2), na sheria za nchi kuhusu masuala ya uchaguzi wa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano na uchaguzi wa Spika, Naibu Spika, Viongozi wa Kamati za Bunge na Wabunge
wataendelea na nyadhifa hizo hadi tarehe ya mwisho wa Maisha ya Bunge kwa mujibu wa Katiba hii.
Sura ya 2 na 343
(2) Masharti ya ibara ndogo ya (1) hayatatafsiriwa kwamba yanazuia kuondolewa kwa Spika, Naibu Spika, Viongozi wa Kamati za Bunge au Mbunge, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 1977, Sheria ya Uchaguzi ya Taifa na Kanuni za Kudumu za Bunge.
Kuvunjwa kwa Bunge
290.-(1) Endapo, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 au sheria za nchi, jambo au suala lolote linahitaji kufanyika au linaweza kufanyika, jambo au suala hilo linaweza kufanyika kutokana au kufuatia kuvunjwa kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
(2) Ikiwa umuhimu wa kuliitisha Bunge utatokea kabla ya kutangazwa kwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu ambao utafanyika baada ya kuvunjwa kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano:
Sura ya 2
(a) kwa madhumuni ya kuliitisha Bunge, Spika, Naibu Spika na Wabunge waliochaguliwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 1977, sheria za nchi na Kanuni za Bunge wanaweza kuitwa na watakuwa Spika, Naibu Spika na Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano litakaloitishwa; na
Sura ya 2
(b) kwa madhumuni ya uteuzi katika nafasi ya madaraka wakati Bunge limevunjwa, uteuzi unaweza kufanywa wa mtu ambaye alikuwa Mbunge kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 na Sheria za nchi zinazohusika.
SEHEMU YA TANO
MAHAKAMA YA JAMHURI YA MUUNGANO
Kuendelea kwa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu
Sura ya 2
291.-(1) Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano na Mahakama Kuu zitaendelea na zitakuwa na mamlaka ya kusikiliza mashauri na kutoa uamuzi au amri kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 na sheria za nchi.
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), Majaji wa Mahakama ya Rufani na Majaji wa Mahakama Kuu watakuwa na madaraka ya kusikiliza mashauri, kutoa hukumu au amri kutokana na mashauri yaliyofunguliwa au yatakayofunguliwa katika Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu.
Kuendelea kwa mashauri yaliyopo mahakamani
292.-(1) Shauri lolote ambalo halijakamilika au limekamilika katika Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu litaendelea kusikilizwa hadi kukamilika; na hukumu, hati ya kukazia hukumu na amri iliyotolewa au itakayotolewa katika shauri hilo inaweza kutolewa na kutekelezwa na Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu
Sura ya 2
(2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), kila hukumu, hati ya kukazia hukumu na amri iliyotolewa na Mahakama ya Rufani au Mahakama Kuu ambayo haijatekelezwa kikamilifu kabla ya kufutwa kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 inaweza kutekelezwa kikamilifu baada ya kuanza kutumika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014.
(3) Uamuzi wowote wa Mahakama ya Rufani uliotolewa kuhusu shauri lolote lililofunguliwa kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 2014, hautakatiwa rufaa katika Mahakama ya Juu.

SEHEMU YA SITA
MASHARTI YA MPITO
Muda wa Mpito
293.-(1) Muda wa Mpito utakuwa muda wote kuanzia tarehe ya kuanza kutumika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014 hadi kupita miaka minne baada ya kuanza kutumika kwa Katiba hii.
(2) Bunge linaweza, kwa azimio litakaloungwa mkono na theluthi mbili ya Wabunge wote, kuongeza muda wa mpito uliotajwa katika ibara ndogo ya (1) kwa kipindi kisichozidi miaka miwili ili kukamilisha Mambo ya Mpito yatakayokuwa hayajafanyika au kukamilika.
Utekelezaji wa masharti ya Katiba Mpya
294. Mambo yafuatayo yatafanyika na kukamilika katika Muda wa Mpito:
(a) kurekebisha Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984 ili kuwiana na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014;
(b) kutunga na kurekebisha sheria mbalimbali za Jamhuri ya Muungano, sheria ambazo si za Muungano zinazohusu Tanzania Bara na sheria za Zanzibar ili kuwiana na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014;
(c) kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu;
(d) kuundwa kwa Tume na Taasisi nyingine za kikatiba zilizoainishwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014 na kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii;
(e) kufanya uteuzi katika nafasi za madaraka kwa utaratibu ulioainishwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014; na
(f) kufanya maandalizi na mambo yote muhimu kwa ajili ya utekelezaji bora wa masharti ya kikatiba yaliyomo kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2014.
Kamati ya Utekelezaji wa Katiba
295.-(1) Kwa madhumuni ya utekelezaji wa masharti ya Sura hii, Rais kupitia Hati ya Uteuzi atateua Kamati ya Utekelezaji wa Katiba katika muda wa mpito.
(2) Majukumu ya Kamati ya Utekelezaji wa Katiba yatakuwa kama yatakavyoainishwa katika Hati ya Uteuzi.
Kufutwa kwa Masharti Yatokanayo na Masharti ya Mpito
296. Baada ya kumalizika kwa Muda wa Mpito, masharti ya Sura ya Kumi na tisa yatakoma na hayatakuwa na nguvu ya kisheria.
107
_____________
NYONGEZA YA KWANZA
______________
(Imetajwa katika Ibara ya 74(3))
Mambo ya Muungano
1. Katiba na Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
2. Mambo ya nje.
3. Ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
4. Polisi.
5. Mamlaka juu ya mambo yanayohusika na hali ya hatari.
6. Uraia na uhamiaji.
7. Utumishi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
8. Kodi ya Mapato inayolipwa na watu binafsi na Mashirika, ushuru wa forodha na ushuru wa bidhaa zinazotengenezwa nchini Tanzania na zinazosimamiwa na Idara ya Forodha.
9. Mawasiliano.
10. Sarafu na Benki Kuu.
11. Elimu ya Juu.
12. Baraza la Taifa la Mitihani.
13. Usalama na usafiri wa anga.
14. Utabiri wa hali ya hewa.
15. Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani.
16. Usajili wa vyama vya siasa.
______________
NYONGEZA YA PILI
_____________
(Imetajwa katika Ibara ya 134(1)(b))
(Sheria ambazo mabadiliko yake yanahitaji kuungwa mkono na theluthi mbili ya
Wabunge wote kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya Wabunge
wote kutoka Zanzibar)
1. Muswada wa sheria wa kubadili masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano yanayohusu Mambo ya Muungano.
2. Kuongeza au kupunguza jambo lolote la Muungano.
108
___________
NYONGEZA YA TATU
_____________
(Imetajwa katika Ibara ya 134(1)(c))
(Mambo ambayo mabadiliko yake yanahitaji kuungwa mkono kwa zaidi ya nusu ya kura halali zilizopigwa na wananchi wa Tanzania Bara, na zaidi ya nusu ya kura halali zilizopigwa na wananchi wa Tanzania Zanzibar katika kura ya maoni)
1. Muundo wa Jamhuri ya Muungano.
2. Kuwepo kwa Jamhuri ya Muungano.
3. Kubadilisha masharti ya Ibara ya 134(1)(c) ya Katiba hii.

Dodoma, SAMUEL J. SITTA
2 Oktoba, 2014 Mwenyekiti wa Bunge Maalum

0 comments:

Post a Comment