MKAKATI WA USAMBAZAJI WA MAJI SAFI NA SALAMA KATIKA MKOA WA KILIMANJARO

Posted by Arusha by day and by night On 10:52 No comments

 Naibu waziri akipanda katika moja ya tenki la kuhifadhia maji katika mkoa wa Kilimanjaro
Naibu waziri akiwa na viongozi wa wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro

MAJUMUISHO YA ZIARA YA NAIBU WAZIRI WA MAJI,
MHE. DKT. BINILITH S. MAHENGE (MB) - MKOANI KILIMANJARO
TAREHE 23 – 30 JULAI 2013

Leo hii ni siku ya nane nipo kwenye Mkoa huu wa Kilimanjaro nikikagua utekelezaji na uendeshaji wa miradi ya maji. Nilianza ziara yangu tarehe 23 Julai na leo tarehe 30 Julai nahitimisha ziara hiyo ikiwa na mafanikio makubwa katika kujionea hali halisi ya Sekta ya Maji katika mkoa wa Kilimanjaro.

Ziara hiyo isingefanikiwa bila ushirikiano wa viongozi wa mkoa wa Kilimanjaro, viongozi wa Halmashauri za mkoa wa Kilimanjaro, viongozi wa kata, vijiji na wataalam mbalimbali. Wote kwa pamoja mmefanikisha ziara yangu na Nawashukuru sana!!!!!!!!!!!!!

Kwa kweli nimejifunza mambo mengi katika Sekta ya Maji na pia nimejionea mwenyewe tofauti ya jiografia ya maeneo mbalimbali mfano pale Same, hali ya milima ni tofauti sana na maeneo mengine ambayo inasababisha ugumu wa kupeleka huduma ya maji. Kwa kweli nimejifunza mengi na nitakuwa balozi wa kupeleka ujumbe mbalimbali kuhusu mkoa huu wa Kilimanjaro.

Sasa naomba nizungumzie kuhusu utekelezaji wa programu ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini.

Naomba nianze kwa kuuliza, mnakumbuka ahadi mliyoitoa na makubaliano mliyoyaweka? Kila mmoja wetu ajitathmini mwenyewe katika kipindi hiki cha kutekeleza kauli mbiu ya “Tekeleza sasa kwa matokeo makubwa” yaani “Big result now”. Majibu yatakayopatikana ni tofauti na makubaliano ambayo mmesaini pale Arusha na Dodoma. Tafsiri yake ni kuwa, wapo wenzetu ambao wamedhihirisha wazi kuwa kasi ya utekelezaji ni ndogo na wapo ambao.

HALI YA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA VIJIJI 10
•    Halmashauri zitakazofikisha lengo la kukamilisha wastani wa vijiji 5 ifikapo Septemba 2013.
Katika mkoa wa Kilimanjaro, ni Halmashauri 4 tu za Mwanga, Same, Siha na Hai ndizo zitakazofikia lengo la kuwa na wastani wa vijiji 5 ifikapo mwezi Septemba 2013. Naomba nichukue fursa hii kuzipongeza Halmashauri hizo, kwa kweli mmetimiza wajibu wenu wa kuwahudumia watanzania.

•    Halmashauri nyingine ziko chini ya lengo lililowekwa mfano:
i.    Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Vijijini inatekeleza mradi katika vijiji 2 vya Korini Kaskazini na Korini Kusini ambavyo vitakamilika mwezi Oktoba 2013. Lakini kukamilika kwa mradi huo kunategemea kupitishwa kwa gharama za nyongeza za milioni 265 za kubadilisha bomba na kuweka bomba za chuma.

Naagiza kuwa, Halmashauri ya Moshi Vijijini kwa kushirikiana na Sekretarieti ya Mkoa zifanye mapitio ya gharama hizo za nyongeza na kufanya maamuzi ili mradi katika vijiji hivyo 2 ukamilike mwezi Oktoba 2013 kama ulivyopangwa.

ii.    Halmashauri ya Wilaya za Manispaa ya Moshi Manispaa imesaini mkatabawa ujenzi katika kijiji cha Languo B na ujenzi bado haujaanza. Hilo si jambo la kuvumiliana hata kidogo, na ni kutowatendea haki watanzania.

Naagiza kuwa, Halmashauri ya Manispaa ya Moshi ihakikishe inaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya vijiji 10.

iii.    Halmashauri ya Wilaya ya Rombo haina mradi hata mmoja ambao mkataba wake wa ujenzi umesainiwa pamoja na kuwa na vijiji 2 vyenye vyanzo vya maji. Kijiji cha Ushiri kina chanzo cha chemchem na kijiji cha Kahe kisima kirefu kimepatikana tangu mwaka 2010. Halmashauri imesema mbele yangu kuwa isingeweza kuanza na vijiji 2 kwa kuwa Mtaalam Mshauri alikuwa anasubiri vijiji vyote vipate vyanzo ili avisimamie kwa pamoja. Huku ni kuwacheleweshea wananchi huduma ya maji bila sababu ya msingi.

Naagiza kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo iharakishe utekelezaji wa haraka wa miradi hiyo ikiwa ni pamoja na kutumia force account. Aidha, kwa vijiji ambavyo vimekosa vyanzo, Halmashauri ziharakishe kutafuta vyanzo mbadala mapema ikkiwemo matumizi ya teknolojia ya uchimbaji wa mabwawa.

Naipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga kwa kutekeleza vizuri miradi ya vijiji 10. Halmashauri hiyo itakamilisha jumla ya vijiji 6 ifikapo mwezi Septemba 2013. Nawapongeza sana.

iv.    Miradi mingine Vijijini
Mwezi Aprili 2013, Serikali imekamilisha uchimbaji wa kisima kimoja katika kijiji cha Mruma katika Halmashauri ya Mwanga. Kisima hicho kina uwezo wa lita za ujazo 8,000  kwa saa na kinalenga kuhudumia watu 4,000 wa vijiji vya Mruma na Mamba. Usanifu wa miundombinu ya kusambaza maji bado haujafanyika.

Agizo: Mhandisi wa wilaya ya Mwanga kwa kushirikiana na Mhandisi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Kilimanjaro, wakamilishe usanifu wa mradi ndani ya mwezi mmoja. Wizara inaahidi kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji.

HALI YA HUDUMA YA MAJI MKOANI NA MIJI MIDOGO.

Mamlaka    Maji yanayozalishwa M3/siku    Mahitaji M3/siku    NRW
%    Idadi ya Wateja    Wateja wenye mita    Makusanyo kwa mwezi
Moshi Mjini    25,156    38,485    39    21,000    21,000    302,000,000
Mwanga    1,532    3,000    51    1,534    687    6,000,000
Same    1,196    4,500    45    1,298    825    12,000,000
Kiliwater    27,000    40,000    78    18,657    12,674    65,000,000
Lawate Fuka water Supply Board (Siha DC)    45,625    45,625    16.7    3,268    3,268    21,886,341
Magadini Makiwaru water supply Board of Trustee (Siha DC)    48,619    48,619    12
    1,937    1,937    25,553,250

•    Nachukua fursa hii kuipongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Moshi (MUWSA) kwa kazi nzuri katika manispaa. Nimeona mipango yao ya uondoaji tatizo la maji katika Manispaa. Naamini mipango hii itatekelezwa.

•    Huduma ya Maji katika Mji mdogo wa Himo inaridhisha kwa sababu maji yanapatikana, Hali iliyopo sasa Himo ni shida ya utawala.  Hakuna Pesa inayokusanywa. Naigiza mamlaka ya Moshi (MUWSA) kumaliza mchakato wa kuunganisha Himo na mtandao wa (MUWSA) kabla ya Mwezi Septemba 2013. Watumiaji maji waanze mara moja kuchangia huduma ya maji.

•    Hali ya maji katika wilaya ya Rombo inayosimamiwa na Kampuni ya Kiliwater hairidhishi, kiwango cha maji kinachopotea ni asilimia 78%, kiwango hiki ni kikubwa sana. Naziagiza halmashauri za wilaya ya Rombo na Moshi  ziwasiliane na Uongozi wa Mamlaka ya Maji na usafi wa mazingira Moshi (MUWSA)  kwa ajili ushauri wa kitaalam kuhusu uendeshaji wa huduma ya maji. Aidha, Mchakato wa Kiliwater kuwa Mamlaka ukamilike mapema ili Mamlaka ijiendeshe yenyewe kwa asilimia 100.

•    Hali ya huduma ya maji katika mji wa Mwanga sio ya kuridhisha. Mamlaka ya Maji katika mji mdogo wa Mwanga ina changamoto nyingi. Moja ikiwa ni kukosekana kwa  ratiba ya migawo ya Maji, wateja wengi hawajafungiwa Dira hivyo kupelekea upotevu wa maji kufikia asilimia  51%, mamlaka inakusanya kiwango cha wastani wa shilingi milioni 6 kwa mwezi. Kiwango hicho ni kidogo.

Naagiza ufanyike ukaguzi wa ndani ili kubaini mapato na matumizi ya mamlaka. Katika kuboresha huduma ya maji Mwanga, namwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mwanga kukamilisha ujenzi wa kisima kipya cha maji  kilichopo mjini ambacho gharama yake ni shilingi milioni 30 kwa ajiliya kutoa maji kwenye kisima na kuingiza kwenye mtandao uliopo. Gharama hizo zinaweza kupunguakama zitapitiwa kwa umakini. Aidha, Deni la umeme nimelichukua na Wizara italifanyia kazi.

Mamlaka ya mji wa Mwanga haina Bodi na meneja na meneja wa mamlaka ameshindwa kazi ya kuboresha huduma ya maji katika mji huo. Meneja wa Mamlaka ya Mwanga anapewa muda wa miezi 6 ya uangalizi, asipojirekebisha kiutendaji, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mwanga amwondoe kwenye cheo hicho na kumpatia afisa mwingine atakayesaidia kuboresha huduma ya maji.

•    Hali ya upatikanaji wa maji katika mji ya Same bado sio nzuri. Mamlaka inazalisha maji kwa kiwango cha asilimia 27%, natambua juhudi za selikai za kuboresha hali ya maji katika miji ya Mwanga, Same Korogwe, pamoja na juhudi hizi bado malamaka ina jukumu la kuboresha huduama ya maji katika mji huu.

Naagiza wateja wote ambao hawajafungiwa dira za maji wafungiwe katika kipindi cha miezi mitatu. Naagiza pia kuwa, Kisima kilichopo mjini Same kikamilishwe haraka iwezekanavyo.

Nampongeza meneja wa Mamlaka ya maji mji wa Same kwa kuwa na makusanyo ya shilingi milioni 12 kwa mwezi ingawa maji aliyonayo ni kidogo.

•    Hali ya huduma ya maji katika wilaya za Siha na Hai inaridhisha. Nazipongeza Bodi za watumia maji za Magadini Makiwaru na Lawate Fuka kwa wilaya ya Siha na Losa-KIA, Uroki Bomang’ombe, Lyamungo Umbwe, Machame na Mkarama kwa walaya ya Hai kwa kazi nzuri. Nashauri vyombo vya watumia maji na mamlaka za maji katika miji midogo kwenda kupata uzoefu katika bodi hizi. 

Katika ziara yangu mkoani Kilimanjaro, napenda kusisitiza mambo yafuatayo:
•    Mamlaka za maji katika miji midogo zipo chini ya Halmashauri kwa mujibu wa sheria Na. 12 ya Huduma za Maji na Usafi wa Mazingira ya mwaka 2009.
•    Halmashauri zote zitenge sehemu ya mapato yake kwa ajili ya kuboresha huduma za maji.
•    Mamlaka zote zihakikishe zinapunguza upotevu wa maji katika maeneo yao hasa kwa kufunga dira kwa wateja wote.
•    Nampongeza mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro kwa juhudi zake za kuboresha zoezi la upandaji wa miti, aidha viongozi wote wa mkoa nawaomba kuongeza juhudi katika zoezi la kuboresha mazingira ili kutunza vyanzo vya maji.
•    Ratiba za migawo ya maji iwekwe wazi na ibandikwe katika mbao za matangazo katika ofisi zote za serikali.
•    Taarifa za Mapato na matumizi ya vyombo vya watumia maji ziwekwe wazi kwa wananchi.
•    Gharama ya mradi wa maji katika wilaya ya Rombo Kijiji cha Kahe ipitiwe upya, kwani gharama hii ni kubwa sana.
•    Elimu itolewe kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuchangia huduma ya maji.
•    Ofisi ya Bonde la Pangani na mabonde mengine nchini wasimamie vibali wanavyovitoa na kukagua matumizi ya maji ili kujiridhisha na matumizi ya vibali hivyo.
•    Taasisi za serikali ambazo zinadaiwa ni muhimu kulipa madeni yao ili kuziwezesha mamlaka za maji kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji.

Hitimisho

    Kwa ujumla hali ya utekelezaji wa miradi ya vijiji 10 inaendelea vizuri na inaridhisha. Isipokua Wilaya ya Rombo na Moshi manispaa. Vile vile hali ya huduma ya maji katika miji midogo inahitaji kuboreshwa zaidi.

Kama nilivyoeleza kwenye Hotuba yangu, kasi ya utekelezaji na usimamizi wa miradi ya maji inahitaji kuongezwa kwa kiwango kikubwa. Naomba kila mmoja wetu aboreshe utendaji kazi katika eneo lake ili kutimiza adhma ya serikali ya kuwasambazia maji wananchi wake.

Kwa kumalizia, naomba tena niwashukuru viongozi wa mkoa, viongozi wa Wilaya, Wataalam wetu, Waandishi wa Habari na wote waliofanikisha ziara yangu mkoani Kilimanjaro. Nasema Asanteni Sana.

Nawatakia mafanikio katika kutekeleza mambo ambayo nimeelekeza kwenye Hotuba yangu ya Majumuisho.



Nashukuru kwa kunisikiliza

Asanteni Sana.




0 comments:

Post a Comment